Mtunzi: Nyemo Chilongani
SEHEMU YA KWANZA
KWA jina ninaitwa Zakia Ramadhani, ni mtoto wa kwanza katika familia yenye watoto kumi, mama yangu aliyeitwa Zubeda Hassani na baba yetu aliyeitwa Saidi Ramadhani ambaye hapo tulipokuwa tukiishi alijulikana zaidi kwa jina la Mzee Mkude.
Familia yetu ilikuwa miongoni mwa familia masikini zilizokuwa zikiishi katika Kijiji cha Mbingu kilichokuwa katika Wilaya ya Ifakara mkoani Morogoro. Hatukuwa na fedha, baba alikuwa mkulima mzuri wa mpunga, mara kwa mara aliamka asubuhi sana na kuelekea shambani kulima huku mama akibaki nyumbani akiandaa uji, unapoiva, ninaondoka naye na kuelekea huko shambani.
Maisha yalikuwa magumu, yalituumiza lakini hatukuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima kupambana usiku na mchana ili tupate angalau fedha za kufanya mambo yetu mengine. Maisha hayo ya kimasikini, niliyachukia sana, nilitamani kuwa na fedha na kuyabadilisha maisha hayo, baba yangu atembelee gari, awe na nyumba nzuri na kufanya biashara zitakazomuingizia fedha nyingi.
Hizo zilikuwa ndoto nilizoota kila siku, ndoto za utajiri lakini kwenye maisha halisi, bado tulikuwa masikini wa kutupwa. Kula kwetu haikuwa ya uhakika, kidogo maisha yanakuwa na ahueni wakati wa mavuno, hapo, tutakula na kushiba, tutanunuliwa nguo na kufanya mambo mengine lakini kwenye kipindi cha upandaji mpunga, tulikuwa kwenye wakati mgumu sana.
Wazazi wetu hawakujua kitu chochote kuhusu uzazi wa mpango na ndiyo maana walizaa watoto wengi tena waliokuwa na utofauti wa umri mdogo, mimi ambaye ndiye nilikuwa mtoto wa kwanza, nilikuwa na miaka ishirini, aliyenifuata ambaye ni mvulana aliyeitwa Husseni alikuwa na miaka kumi na tisa, yaani watoto wote kumi tulipishana kwa mwaka mmojammoja.
Sikuwa na elimu, sikubahatika kuingia darasani, wazazi wetu hawakuwa wamesoma na hawakuamini kama elimu inaweza kumsaidia mtu kupata mafanikio. Kipindi cha nyuma waliambiwa sana watupeleke shule kujifunza lakini wakakataa kwa kuamini kwamba hata usipokuwa na elimu, ukitafuta fedha, utazipata tu, cha msingi uwe na moyo wa kutafuta.
JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈
SASA TUENDELEE...
“Unaweza kwenda shule, ukapoteza fedha kumbe Mungu amekwishakuandikia maisha ya kitajiri hapo baadaye, uje kuolewa na milionea au hata wewe kupata fedha kupitia biashara nyingine,” aliniambia baba, tena kwa ujasiri huku akiniangalia machoni.
Nilichokigundua ni kwamba baba hakuwa na fedha, hakuwa na uwezo wa kutulipia ada na ndiyo maana hata sababu alizozitoa hazikuwa na msingihata kidogo. Sikutaka kuingilia, niliendelea kubaki nyumbani mpaka nilipofikia umri huo, sikuwahi hata kuingia darasani kusoma.
Miaka ishirini lakini bado niliendelea kuishi kwa wazazi. Sijui kama nilirogwa au la lakini ukweli ni kwamba kila mwanaume niliyekuwa naye aliniacha siku chache kabla ya ndoa kisha kumuoa mwanamke mwingine.
Nakumbuka nilikuwa na mwanaume aliyeitwa Hamisi Sultan. Huyu mwanaume alinipenda sana, alikuwa mkulima mzuri, alijituma sana kijijini kiasi cha kumiliki mashamba yake ya mpunga, wazazi wangu walimpenda lakini kitu cha ajabu kabisa kilichotushangaza, wiki mbili kabla ya kufunga ndoa, akaniacha na kumuoa mwanamke mwingine.
Iliniumiza moyoni, sikuwa na jinsi, nililia sana na mwisho wa siku nikasahau na kuendelea na maisha yangu. Mwanaume wa pili aliyefuata aliitwa Abdul Maliki. Alikuwa mzuri wa sura, nilimpenda sana na wiki tatu kabla ya kufunga ndoa, akaniacha na kumuoa mwanamke mwingine.
Hayo yote yaliyotokea, yaliniumiza mno, sikuamini kama mimi ndiye niliyekuwa nikipitia maisha hayo. Hawakuishia wanaume hao tu, walikuja wengine kama watatu lakini matokeo yalikuwa yaleyale, kila aliyetaka kuniona, wiki chache kabla ya kufunga ndoa, aliniacha.
Sikutaka kukubali, nilichokifanya ni kufanya uchunguzi wa kujua tatizo lilikuwa nini, nilichogundua ni kwamba sababu kubwa ilikuwa ni umasikini na pia familia kuwa kubwa ilisababisha. Wanaume waliogopa kunioa kwa kuwa walijua kwamba sisi ni masikini, familia ya watoto kumi ilikuwa kubwa kiasi kwamba wakaona kama wangenioa, basi wangebebeshwa mzigo mkubwa wa kuitunza familia.
Nikakata tamaa ya kuolewa, sikuona kama kuna mwanaume mwingine angekuja na kunioa. Nililia usiku kucha, nilimlaumu Mungu lakini pamoja na kulia kote, lawama zote nilizozitoa, ukweli ukabaki palepale kwamba hakukuwa na mwanaume aliyetaka kunioa.
“Yaani sababu ya umasikini tu? Yaani sababu ya kuwa na familia kubwa tu?” nilijiuliza maswali mawili, majibu yake yalikuwa yenye kuumiza mno.
Maisha yaliendelea, hapo kijijini kulikuwa na familia nyingine zilizokuwa na uwezo kifedha, zilikuwa na nyumba zenye mabati, nyumba zao zilijengwa kwa matofali, hizohizo familia ndizo zilizotuletea dharau sisi masikini.
Kulikuwa na mambo mengi yaliyoniumiza, ila hili, lilikuwa la kwanza. Sikuona sababu ya kudharaulika kwa kuwa hatukuwa na fedha, sikuona sababu ya wazazi wangu kudharaulika kwa kuwa tu kila siku walivaa mavazi yaliyochakaa. Nilitaka na sisi tupewe heshima kama watu wengine, tupendwe na kuthaminiwa kama watu wengine ila hayo yote, yasingewezekana bila kuwa na fedha.
“Baba, hizi dharau zitakwisha lini?” nilimuuliza baba.
“Mpaka tutakapokuwa na fedha Zakia,” alinijibu.
“Na hizo fedha tutazipata lini?”
“Sijui, cha msingi tuvumilie, kuna siku Allah atafanikisha jambo,” aliniambia baba, uso wake ukajawa na tabasamu pana, tabasamu la kuniridhisha, ila kwa kupitia macho yake, niliona ni jinsi gani alikuwa na maumivu moyoni mwake.
Siku ziliendelea kwenda mbele. Maisha yalizidi kutupiga na kila siku iliyoingia nilisema afadhali ya jana. Moyo wangu ulikuwa kwenye maumivu makali kwa ajili ya vitu viwili tu, kitu cha kwanza ni kwa jinsii famiulia yetu ilivyotafunwa na umasikini lakini kitu cha pili kilikuwa ni jinsi wanaume waliotaka kunioa kuniachana na kuwafuata wanawake wengine.
Baada ya kuona kwamba maisha yanakuwa magumu sana ndipo nilipoamua kuwaita wazazi wangu na kuwaambia kwamba nisingeweza kuishi kijijini kwa sababu hakukuwa na kitu kilichobadilika kwa miaka yote, hivyo nilitaka kuondoka kuelekea jijini Dar es Salaam.
Wazazi wangu hawakukubali kabisa, waliniambia kwamba mjini hakukuwa kuzuri, kulikuwa na wanawake wengi waliokwenda huko lakini kutokana na ugumu wa maisha waliishia kujiuza tu. Niliwaambia kwamba nisingeweza kufanya hivyo bali nilitaka kwenda huko na kutafuta fedha kwa njia halali kabisa.
“Haiwezekani…” alisema baba huku akionekana kukasirika.
“Baba! Siendi kufanya biashara ya kujiuza, nakwenda kutafuta fedha,” nilimwambia kwa sauti ya kulalamika.
“Utafikia wapi? Mjini hatuna ndugu yeyote, wewe utaishi kwa nani?” aliniuliza huku akiniangalia machoni.
“Nitafikia kwa rafiki yangu!”
“Nani?”
“Sikujua…”
Japokuwa niliwaambia hivyo lakini hawakutaka kuniruhusu kabisa. Moyo wangu ukakosa furaha, nilikasirika sana kwani niliamini kwamba nilikuwa binti mkubwa ambaye nilitakiwa kuondoka nyumbani na kwenda kutafuta maisha yangu.
“Baki nyumbani Zakia, mbona hapa unakula na kulala bure, huko mjini hakuna maisha. Mwenzako Zubeda alikwenda huko, kilichomtokea nadhani unakijua, achana na huyo, kuna Hawa, Mwamvita, wote walitokewa na mabaya, kwa nini uende huko?” aliuliza mama huku naye akiniangalia usoni kwa macho yaliyoonyesha dhahiri hawakutaka niondoke kijijini hapo.
Sikuzungumza kitu chochote kile, kama kuomba, niliwaomba ila walinikatalia hivyo nilichokifanya ni kusuka mipango yangu ya kutoroka. Sikutaka kuonekana mnyonge, wangeweza kushtuka kile kilichokuwa akilini mwangu wakati huo, niliwaonyeshea tabasamu pana huku nikiwa mchangamfu kana kwamba hakukuwa na kitu kilichoniumiza.
Baada ya siku nne tu, sikutaka kubaki kijijini hapo, umasikini ulitutesa na hivyo njia ya kupata fedha na kuwa milionea niliiona ni kutoroka tu, hivyo nikafanya hivyo. Siku ambayo nilitoroka, niliamka saa kumi alfajiri hata kabla ya mtu yeyote kuamka nyumbani, nikachukua nguo zangu chache na kuziweka katika begi langu chakavu, nikaanza kunyata, nilipoufikia mlango, nikaufungua na kuanza kukimbia.
“Ninaondoka nikiwa masikini, nitarudi nikiwa tajiri…” nilisema huku nikikimbia kwa kasi kuelekea porini.
Kulikuwa na giza lakini sikuogopa hata kidogo, nilikuwa nikikimbia kuelekea upande wa Kusini kulipokuwa na Lupiro. Kulikuwa na umbali kama kilometa ishirini kutoka kijijini kwetu lakini sikutaka kukata tamaa, niliendelea kukimbia, nilipochoka, nilipumzika na kuendelea na safari.
Baada ya saa kama nne, nikaanza kuingia katika kijiji hicho ambapo kulikuwa na kituo cha daladala ndogo (hiace) zilizokuwa zikielekea Ifakara Mjini. Sikuwa na pesa yoyote mfukoni mwangu ila niliamini kwa kutumia jinsi yangu, ingekuwa kazi rahisi sana kumlaghai hata utingo.
“Za saa hizi kaka!” nilimsalimia utingo.
“Poa! Karibu mrembo!” aliniambia.
Kitendo cha kuniita mrembo tu kilinipa uhakika wa kufanikiwa kile nilichokuwa nikikitaka. Nilikuwa mzuri wa sura na hata umbo langu lilivutia, akawa ananiangalia kwa macho niliyoyaelewa nini alihitaji, na nilichokifanya ni kuanza kuunyonganyonga mwili wangu.
“Mbona huongei jamani? Tatizo nini?” aliniuliza huku akinisogelea.
“Nataka kufika Ifakara mpenzi!” nilimwambia kwa sauti ndogo.
“Hakuna tatizo! Mbona poa tu…”
“Ila kuna tatizo!”
“Tatizo gani?”
“Sina nauli!’ nilimwambia.
Kwanza akatoa tabasamu pana, nilihisi kwamba alifurahia sana kusikia hivyo kwani ndiyo ilikuwa njia nyepesi kwake kukamilisha adhma yake. Akaniambia kwamba hakuna tatizo lolote lile, angenisaidia mpaka kufika huko Ifakara kwani ndipo anapoishi.
“Nitakupeleka bure kabisa….una ndugu huko?” aliniuliza.
“Sina.” Nikamjibu, akaongeza tabasamu zaidi.
Alichokifanya ni kunipokea begi langu na kunipeleka ndani ya daladala lile. Nilikaa huku nikiwa najifikiria ni kitu gani kingetokea mara baada ya kufika Ifakara. Nilipomwangalia utingo ambaye nilimsikia dereva akimuita kwa jina la Mudi, muda wote alionekana kuwa mwenye furaha tele, abiria walipojaa ndani ya gari, dereva akaliwasha na kuanza safari ya kuelekea huko.
Utingo huyo alikuwa akifikiria ngono, ila kichwa changu kilikuwa kikifikiria utajiri tu ambao niliamini kwamba ningeweza kuupata baada ya kufika jijini Dar es Salaam.
Bado akili yangu ilikuwa ikimfikiriaMudi, alionekana kuwa mwenye furaha tele kwani alijua kwamba siku hiyo mambo yake yangekwenda vizuri kabisa.
USIKOSE SEHEMU IJAYO
Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi
