BABA KIUMBE WA AJABU (12)

Zephiline F Ezekiel
Mtunzi: Ally Mbetu

SEHEMU YA KUMI NA MBILI
TULIPOISHIA...
“Mimi na ninyi nani kaamua kumuua mwenzake?”

Masalu kumbuka baba yetu ni huyuhuyu, akifa hatutampata mwingine.”

“Kwani kuna mbadala wa dada Monika, baba ni huyo huyo, dada Monika mwingine yupo wapi?”

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI

SASA TUENDELEE...
“Masalu makosa yamekwisha fanyika rudisha moyo uokoe maisha ya baba.”

“Kwanza mnaniambia hivyo mimi nimemfanya nini baba?” niliwauliza swali gumu.

“Inaonekana umekwenda kwa mganga kurudisha nguvu zako za kiume.”

“Mlitaka niwe hivihivi milele kwa raha zenu, mbona ninyi mna watoto na wanaume?”

“Kwani Masalu upo wapi?”

“Tokea lini mlinitafuta?”

“Basi zungumza na mama,” baada ya muda nilimsikia mama akiniita.

“Masalu.”

“Naam mama, shikamoo.”

“Marahaba mwanangu upo wapi? hali ya baba yako ni mbaya sana.”

“Anaumwa nini?”

“Ameanguka kwenye mishughuliko yake, kama ni kweli umefanya wewe njoo umsaidie baba yako, hali inatisha hajitambui anakoroma tu.”

“Mama sihusiani na lolote kuhusiana na matatizo ya baba, naomba mumpeleke hospitali.”

“Ugonjwa huu si wa hospitali.”

“Kwa hiyo mimi ndiye niliyemroga?”

“Hapana Masalu, ila inawezekana ulichokifanya ndicho kilichomuathiri baba yako.”

“Kipi hicho?”

“Unakijua Masalu, hebu rudi haraka nyumbani.”

“Mama ni nani kwako?”

“Mtoto.”

“Nina haki gani kama mmoja wa watoto wako?”

“Haki zote kama walizonazo wenzako.”

“Sasa kama kila mtu ana haki hiyo kwa nini unataka kushiriki katika kunigeuza ndondocha wa familia?”

“Masalu! Wakugeuze kivipi?” mama alishtuka.

“Mama, unajua vizuri sana si suala la siri, mpango wenu wa kunimaliza nimeugundua lakini nawahakikishia kila atakayenigusa nitampoteza.”

“Upo tayari baba yako afe?”

“Mimi situnzi uhai wake bali Mungu aliyetuumba wote, kama wakati wake umefika basi atakufa, kama alivyokufa mtoto wa dada na dada Monika.”

“Kwa nini umekosa huruma?”

“Kwa vile ninyi mnanionea huruma eeeh.”

“Kama ulivyosikia hali ya baba yako ni mbaya kifo chake kitakuhusu.”

“Sishangai hata wewe mama niliyekuwa nakutegemea ni mmoja wapo. Asante sana nashukuru, Mungu yupo atanilinda.”

“Masalu...Masa..,” nilikata simu na kuizima kabisa.

                                                   ******

Baada ya mazungumzo nilijikuta nikilia peke yangu jinsi familia yangu ilivyokuwa ikijijali yenyewe na kuwa tayari kupoteza uhai wa mtu ili tu ipate mali. 

“Masalu nyamaza mpenzi wangu,” mpenzi wangu alinibembeleza, kipindi kile yeye ndiye aliyekuwa mfariji wangu.

“Inaniuma.”

“Kweli inauma, lakini kwa nini umekubali kuzungumza nao? Ungezima simu yote haya yasingetokea.”

“Ilikuwa lazima nizungumze nao ili wajue kuwa naelewa kila kitu, pia hata kujua kama kweli hali ya baba ikoje.”

“Kwa hiyo utakwenda kumuona baba yako?”

“Nikitoka kwa mganga nitakwenda.”

“Pole sana inasikitisha, familia yako ina dhambi kubwa.”

“Wee waache sijui kwa Mungu watasema nini?”

“Ulisema wewe ndiye chanzo cha utajiri kilichoachwa na marehemu dada yako Monika, ukipona itakuwaje?”

“Sijui, watajua wenyewe, mimi nitaangalia afya yangu.”

“Mmh! Pole sana mpenzi wangu, kupona lazima uwe na roho ngumu ili umeze mfupa.”

“Nimekwisha umeza lolote na liwe, siwapendi mashetani wale.”

Kwa vile muda ulikuwa umekwenda tulipanda kitandani kulala, usiku nilijikuta nikipatwa na hamu ya mapenzi. Lakini nilikumbuka kauli ya mganga kuwa nikikutana kimwili na mwenzangu ndiyo kifo cha baba, hawezi kuomba hata maji.

Pamoja na hasira kutokana na roho mbaya ya familia yangu juu ya mambo waliyotaka kunifanyia nilijikuta nikiingiwa na imani ya kutofanya tendo lile kuokoa maisha ya baba. Tulilala mpaka asubuhi bila kufanya tendo la ndoa, asubuhi tuliamkia kwa mganga.

Hatukuchelewa kufika kwa vile hapakuwa  mbali kutoka tulipokuwa tumepanga, ulikuwa mwendo wa dakika ishrini. Ilionesha sisi ndiyo tulikuwa wateja wa kwanza toka nje kufika pale kwa siku ile, tuliowakuta pale ni wale waliokuwa wakitibiwa na kulala palepale.

Mganga alitukaribisha, kama kawaida niliingia ndani peke yangu na mpenzi wangu alibakia nje. Nilipofika hakunisemesha lolote, aliendelea na kutoa chupa za dawa kwenye kikapu na kuziweka juu ya ngozi kisha alichukua karatasi ya kaki na kuanza kumiminia unga wa dawa kidogo kidogo kutoka katika kila chupa.

Zilikuwa chupa zaidi ya tano, baada ya kuukusanya unga wa dawa katika karatasi moja, alichukua chupa iliyokuwa na mafuta kama sikosei ya ng’ombe, yalikuwa meupe na mazito. Aliyamiminia yale mafuta na kuyachanganya na mchanganyiko wa dawa kisha alitoka nje.

Baada ya muda alirudi na kunionesha kwa ishara nimfuate, nilimfuata mpaka kwenye kichuguu kimoja ambacho alinielekeza. Kabla ya kupanda juu ya kichuguu alinielekeza kwa ishara nivue shati. Nami nilifanya kama alivyonielekeza.

Baada ya kupanda juu ya kichuguu kifua wazi, alipanda na yeye na kuanza kunichanja kila kona ya mwili huku akinipaka ile dawa aliyochanganya na mafuta mazito. Alipomaliza tuliteremka na kurudi hadi ndani ya kilinge, ndipo aliponisemesha.

”Habari za toka jana?”

“Nzuri mzee wangu, shikamoo.”

“Marahaba, kuna habari gani mpya?”

“Jana walinipigia simu usiku na kuniomba ninusuru maisha ya baba.”

“Uliwajibu nini?”

“Niliwaambia siwezi kujiteketeza mwenyewe.”

“Wao walisemaje?”

“Walinitishia kama baba akifa nitamla nyama.”

“Akawajibu nini?”

“Niliwaeleza kama walivyokula nyama ya dada Monika.”

“Wakasemaje?”

“Walishtuka na kunieleza kuwa habari nimezijulia wapi?”

“Mh, ukawajibu nini?”

“Niliwambia nitawapeleka polisi na kuwafungulia mashtaka ya uuaji na kukaa na maiti za watu ndani?”

“Enhee! Wakasemaje?”

“Walishtuka na kuniomba ninusuru maisha ya baba.”

“Ukawajibu nini?”

“Niliwaeleza sipo tayari.”

”Wakasemaje?”

“Waliendelea kunibembeleza niende kwa vile uliniahidi nikitoka hapa nitakuwa kamili, nimewaeleza nitakwenda leo.”

“Wakasemaje?”

“Tumekubaliana, nikitoka hapa niende.”

“Sikiliza, una bahati kama usingekuja hapa na kujipendekeza jana ukaenda ungekwisha palepale.”

“He!” Nilishtuka kusikia vile.

“Unashtuka, kama nilivyokueleza familia yako haina mapenzi na wewe kwa ajili ya mali.”

“Mmh! Sasa nikienda leo itakuwaje?”

“Leo usiende, nenda keshokutwa ila kuna kitu kitatokea si cha kawaida, kuwa tayari kukabiliana nacho.”

“Kitu gani hicho?”

“Wee nenda, ila majibu utayapata kujua kinga niliyokukinga inafanya kazi kiasi gani.”

“Niambie ili nijue ikiwezekana nisiende.”

“Lazima uende ili kuwaumbua wabaya wako.”

“Mmh! Sawa.”

“Baada ya kesho kwenda rudi tumalizie tiba, kwa vile hawatakubali kuona umewashinda.”

“Sawa nimekuelewa.”

“Nilitaka kusahau kitu kimoja, leo usioge wala kukutana na mwanamke kimwili ikiwezekana leo kila mmoja alale chumba chake au kitanda chake.”

“Sawa nimekuelewa.”

“Ndoto utakayoiota ndilo jibu la safari yako.”

“Nashukuru kwa msaada wako.”

                                              ******

Baada ya mazungumzo, tulirudi hoteli tuliyokuwa tumepanga kwa ajili ya mapumziko, siku ile sikukaa kutokana na kuwa na alama nyeusi za kuchanjwa na mganga.

Kwa vile hatukuruhusiwa kulala pamoja, tulichukua chumba cha vitanda viwili na kila mtu alilala kitanda chake. Usiku niliota ndoto nafukuzwa na kichaa mmoja ambaye katika kunifukuza aligongwa na gari, hapohapo nilishtuka usingizini na kujiuliza kichaa yule ni nani na ndoto ile inaashiria kitu gani.

Siku ya pili nilimueleza mpenzi wangu ambaye alinishauri heri nisiende nyumbani ili kuepusha nilichokiota.

“Masalu kama mganga alikuambia utakachokiota ndicho kitakachotokea, kwa nini uende?”

“Hilo wazo hata mimi nilikuwa nalo lakini mganga alisema lazima niende, ili nirudi na kupata dawa ya mwisho.”

“Kwa nini asikupe hiyo dawa?”

“Alisema lazima niende ili kuonesha uwezo wa kile alichokifanya jana.”

“Mmh! Mtihani mzito kweli.”

“Lakini kwetu hatuna kichaa.”

“Basi inawezekana utakutana naye njiani.”

“Kama ni hivyo bora nikodi gari mpaka mlangoni.”

“Bora ufanye hivyo.”

“Sawa, basi tuongozane, wewe uende kwenu najua wamekutafuta sana.”

“Hata wakinitafuta mimi mtu mzima, kuna mdogo wangu anajua kila kitu sidhani kama watasumbuka sana. Mbona tuliishasafiri zaidi ya wiki hakuna kilichoharibika?”

“Si uliaga?”

“Basi taarifa zangu watazipata kwa mdogo wangu na leo nikifika watapata jibu.”

“Mmh! Haya.”

Niliongozana na mpenzi wangu hadi kwao, nilimteresha na mimi kuendelea na safari yangu. Nilikwenda na gari hadi mlangoni na kuteremka, wote waliokuwepo walishtuka. Baba aliyekuwa amelazwa sebuleni aliponiona alipiga kelele.

“Mtoeni...mtoeni  ataniua...ataniua.”

“Baba siwezi kukuua, utajiua mwenyewe,” nilimjibu baba.

“Jamani mtoeni ataniua,” baba alizidi kupiga kelele.

“Masalu hebu toka nje,” dada alinifokea.

Niligeuka kutoka nje, kaka yangu alikuja kwa nyuma na kunishika kisogoni, mara alianza kupiga kelele kama mtu aliyepagawa, akachukua jembe na kutaka kunipiga nalo, alinikosakosa mara mbili, nilipoona hatanii nilitimua mbio, alinikimbiza mpaka barabarani huku akidhamiria kuniumiza.

Ilinibidi nivuke barabara bila kuangalia baada ya kuona nakufa najiona, baada ya kuvuka nilisikia kishindo nyuma yangu na kelele za watu. Nilipogeuka nilimuona kaka yangu akiwa chini akivuja damu kichwani.

Japo ajali ile ilifanya moyo uume na kupatwa na huruma, lakini sikutaka kurudi kuangalia, wakati huo watu walikuwa wakijaa kwenye tukio la ajali na kumzunguka kaka. Nilikodi teksi iliyokuwa ikipita kuwahi nyumbani. Nilipofika nyumbani nilimpigia simu mpenzi wangu.

“Vipi Masalu mbona kama kuna tatizo?”

“Ndiyo.”

“Tatizo gani?”

“Si la kulizungumzia kwenye simu.”

“Upo wapi?”

“Nyumbani.”

“Nakuja sasa hivi.”

Baada ya kukata simu nilibaki nimejilaza kwenye kochi nilijiuliza vita nzito niliyoelezwa na mganga ndani ya familia yangu nini hatima yake. Nilijiuliza kaka yangu bila kugongwa na gari alitaka kunifanya nini. Au alikusudia kuniua?

Njozi ile baada ya kuuona ukweli nilijuliza nini kitafuata.

Niliamini kama vita ya nguvu za giza itashindikana basi watatumia nguvu za kawaida ili kunitokomeza duniani. Nilijiuliza kama itakuwa hivyo nitawezaje kuwaepuka? Nilipanga kuukimbia Mji wa Mwanza ili kuokoa maisha yangu kwa kuliuza duka langu.

Wazo lile nilitaka nishauriane na mwenzangu kabla ya kutoa uamuzi, nilipanga akija nitamgusia suala lile ambalo kwa upande wangu lilichukua sura mpya ya kutishia maisha yangu. Wakati nikiwa kwenye dimbwi la mawazo mpenzi wangu aliingia kwa hali aliyonikuta nayo ya kujilaza mikono kichwani ilimshtua sana.

USIKOSE SEHEMU IJAYO

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni