BABA KIUMBE WA AJABU (9)

Zephiline F Ezekiel
Mtunzi: Ally Mbetu

SEHEMU YA TISA
TULIPOISHIA...
Nilishindwa tena kumueleza kitu chochote, nilibakia kupelekwa kama mkokoteni usio na breki. Tulipoingia ndani mpenzi wangu alionekana na shauku kwa kunivamia kutaka mapenzi. Nilijiuliza nitawezaje kumkatalia tusifanye mapenzi ikiwa tayari ameishalipia chumba?

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

SASA TUENDELEE...
Nilijiuliza kama nikifanya mapenzi itakuwaje, nilijikuta nikisemea mwenyewe “Liwalo na liwe” niliamua kufanya mapenzi siku ile. Kilichomshtua mpenzi wangu ni kitambaa nilichokuwa nimejifunga mguuni.

Masalu nini hiki?”

“Niliumia,” nilidanganya.

“Sasa mbona umejifunga kitambaa badala ya dawa?”

“Natumia dawa za asili.”

“Ulifanya nini?”

“Niliumwa na nyoka wa maajabu.”

“Una maana gani?”

“Nilikuwa nimelala ndani nikaota naumwa na nyoka.”

“Enhee.”

“Nilipoamka si ndiyo nikakuta natokwa damu.”

“Mungu wangu, baada ya hapo ikawaje?”

“Nilikimbizwa hospitali, lakini kila dawa niliyowekewa ilizidi kulifanya donda kuzidi kuchimba.”

“Jamani ni nyoka gani huyo akuume kitandani?”

“Hata sijui.”

“Mmekwenda kwa wataalamu wa jadi?”

“Nilikwenda ndiyo natumia tiba yao kidogo sasa sijambo.”

“Walikuambia nini kuhusiana na tatizo lako?”

“Nilielezwa kuwa nitatibiwa hadi nipone.”

“Mmh! Masalu pole sana mpenzi wangu, mbona hukuniambia mapema?”

“Sikupenda kukuumiza moyo mpenzi wangu, nilijua tatizo ni dogo kumbe kubwa.”

“Mmh! Pole sana,” mpenzi wangu aliniambia kwa sauti ya huruma.

“Asante.”

Pamoja na mazungumzo yale, mpenzi wangu alilazimisha tufanye mapenzi kwa vile alikuwa na hamu na mimi sana. Nilijikuta sina jinsi zaidi ya kukubali kufanya naye mapenzi na kukiuka masharti ya baba. Siku hiyo sikurudi nyumbani, nilala hotelini na mpenzi wangu mpaka asubuhi.

Siku ya pili nilirudi nyumbani majira ya saa tatu, mara moja kwenda kubadili nguo kisha niende dukani kwangu. Mama aliponiona alishtuka na kuniuliza:

“Masalu ulikuwa wapi?”

“Nilikwenda kwenye sherehe ya rafiki yangu.”

“Kwa nini hukurudi?”

“Iliisha muda mbaya.”

“Mmh! Sawa baba yako leo hajalala, ninavyozungumza na wewe, ameondoka asubuhi kwenda kukutafuta.”

“Sasa ananitafuta mimi mtoto?”

“Hayo hayajui baba yako, si unajua wewe ndiye mtoto wake wa mwisho.”

“Naelewa, lakini mimi sasa hivi ni mtu mzima.”

“Ina maana jana ulilala na mwanamke?”

“Mama kusema mtu mzima namaanisha kulala na mwanamke?”

“Sina maana hiyo, kulala nje siyo tija, wasiwasi wangu pengine ulimaanisha hivyo.”

“Lakini kumbukeni mnaninyima haki yangu ya msingi.”

“Ni kweli, lakini ndivyo ilivyo, unatakiwa kuvumilia.”

“Hayavumiliki.”

“Tutafanyaje?”

“Ipo siku nami nitapata ufumbuzi wa tatizo langu kama dada Monika.”

“Unataka kufanya kama dada yako? Usifanye hivyo bado tunakuhitaji.”

“Hamna shida na mimi, wenye thamini kwenu ni hao wanaoishi maisha mazuri yasiyo na masharti.”

“Hapana Masalu, utanifanya mama yako nife kwa mawazo. Hujui kiasi gani nilivyokuwa nawapenda wewe na Monika, ndiyo watoto pekee mnaonijali. Baada ya kifo cha Monika umebakia wewe na wewe ukifa nami sitachelewa kufa, sitakuwa na mtetezi wangu wa karibu.”

“Mama nakupenda sana, lakini baba hatutendei haki.”

“Najua tuvumilie, hata wewe si unajua maisha yangu yalivyo?”

”Nayajua mama.”

“Sasa kwa nini unakuwa hivyo, hebu tuvumilie.”

”Sawa mama.”

Nilimkubalia mama lakini moyoni nikiwa na siri nzito ya kitendo nilichokifanya na mpenzi wangu usiku kucha.

Baada ya kujiandaa nilikwenda zangu dukani kwangu, nilipofika nilikuwa tayari wameishafungua. Wahudumu wangu waliponiona walinieleza:

“Bosi mzee alikuja kukutafuta.”

“Amesemaje?”

“Kwa kweli haeleweki, sijui hukulala nyumbani?”

“Kama sikulala nyumbani mimi mtoto?”

“Tutajuaje, tumemkuta kabla ya kufungua duka, alipotuona tu alituuliza upo wapi, sisi tukamjibu tangu jana tulipoachana hatujui upo wapi?”

“Mzee yule anazeeka vibaya, sasa kasemaje?”

“Tumemuona akitembea kona moja hadi nyingine kisha alitoweka bila kuaga.”

“Achaneni naye.”

Nilisema huku nikikaa kwenye kiti changu, ajabu wafanyakazi walinishangaa jinsi nilivyoonesha sijali lolote. Haikuchukua muda baba aliingia huku akitweta.

“Masalu.”

“Naam baba, shikamoo.”

“Marahaba, hebu njoo nje mara moja.”

Nilitoka nje kuzungumza na baba, baada ya kusogea pembeni baba aliniuliza.

“Masalu jana ulilala wapi?”

“Kwenye sherehe.”

“Sherehe ya nani?”

“Ya rafiki yangu.”

“Masalu kuna sherehe gani katikati ya wiki?”

“Birthday.”

“Hukulala na mwanamke wewe?”

“Mbona unaniuliza hivyo?”

“Masalu umelala na mwanamke,” baba alinilazimisha.

“Baba nimekueleza nilikuwa kwenye pati unanilazimisha nimelala na mwanamke,” nilijitia kujitetea.

“Masalu tusije kulaumiana, ukirudia tena shauri yako.”

“Hivi baba kwa nini unanilazimisha kitu nisichokifanya, ulinikataza nisitembee na mwanamke si kufanya mambo mengine kama hili la jana, nakushangaa unanitafuta kama mwizi.”

“Mmh sawa.”

“Baba mbona unataka kuninyima uhuru, niliyajua haya toka mwanzo ukabisha, ona sasa unanifuata kila kona,” nilijifanya kulalamika.

“Siyo hivyo, sipendi uingie kwenye matatizo.”

“Baba mi mtu mzima sasa, vilevile najijali.”

“Kama ni hivyo itakuwa vizuri, nisamehe kama nimekukwaza.”

“Nimekusamehe ila naomba uhuru sipendi nifuatwefuatwe.”

Kauli yangu ilimfanya baba azidi kuomba msamaha, tulikubaliana asinifuatilie mambo yangu kwa vile nitajilinda mwenyewe.

                                                          *****

Tangu siku ile hata nilipolala nje baba hakunifuatilia, aliniacha niishi nitakavyo, mpenzi wangu alinishawishi nihame nyumbani ili tuweze kuwa naye siku zote. Nilifikisha wazo kwa baba ambaye mwanzo alipinga lakini baada ya kumlazimisha alinikubalia kwa shingo upande. Nilipanga chumba maeneo ya Isamilo ambako nilipanga nyumba nzima. Niliendelea na tabia zangu za kufanya mapenzi na mchumba wangu ambaye alihamia kwangu kwa siri.

Siku moja baba alinifuata dukani na kuniita pembeni, baada ya kusogea pembeni aliniuliza:

“Masalu kwa nini hujihurumii?”

“Kivipi?”

“Hebu nione kidonda chako.”

Nilimuonesha, kidonda changu, baada ya kukiangalia alisema:

“Si unaona!”

Nilishangaa, sikujua alisema vile kumaanisha nini? Nilijikuta nikijiuliza kipi kilichomuonesha kitu kilichomshangaza.

“Kuona nini baba?”

“Ina maana huoni kidonda chako kinaonesha hujionei huruma maisha yako.”

“Bado sijakuelewa.”

“Kidonda chako kinatoa maji?”

“Hapana.”

“Unajua kwa nini?”

“Hata sijui.”

“Masalu unatembea na mwanamke wewe.”

“Baba mbona unang’ang’ania neno hilo?”

“Nakuomba uache, shauri zako.”

“Niache vipi wakati sifanyi?”

“Masalu mimi baba yako nimewahi kuona jua kabla yako najua kila kitu, na sababu kubwa ya kuhama nyumbani ni kufanya uchafu wako. Huoni hata biashara sasa hivi zinadoda?”

“Baba tafuteni tatizo lingine siyo mimi.”

“Mmh, haya mama yako asiye kunililia.”

Baba aliondoka akiwa amechanganyikiwa, nami sikuwa tayari kuachana na mpenzi wangu, katika maisha niliamini raha ya mwanaume ni mwanamke na si wingi wa pesa. Siku hiyo hiyo ndugu zangu wote walikuja na kuniweka chini juu ya mimi kuwa na mwanamke.

“Masalu kwa nini hutaki kumsikiliza baba?”

“Nimsikilize kwa lipi?”

“Juu ya wewe kuwa na mwanamke.”

“Mna uhakika gani?”

“Sisi hatuna uhakika ila kasema mwenyewe.”

“Ninyi mna wapenzi?” Niliwauliza.

“Tunao.”

“Sasa mimi nazuiwa na nini?”

“Si unajua hali yako haitaki uwe na mwanamke?”

“Kwa hiyo kidonda niwe nacho mimi maisha mazuri muwe nayo ninyi, sikilizeni kila mtu ataubeba mzigo wake mwenyewe.”

“Masalu utakuja kuijutia kauli yako.”

“Sijutii, mbona dada Monika hakuijutia na mkiniua na ninyi mnafilisika, kazi kwenu.”

Maneno yangu yaliwazima midomo, waliondoka na kuniacha wakiwa hawana hamu na mimi. Tangu siku ile nikawa adui yao mkubwa, niliwashangaa kunikasirikia mimi kuwa na mwanamke wakati wao walikuwa na kila kitu. Kama mateso ya kidonda nimeyakubali bado hawaridhiki walitaka nikose na raha za dunia.

Ukali wa baba uligonga mwamba, akamtumia mama kunibembeleza, nani msimamo wangu ulikuwa palepale wa kukataa kuwa nalala na mwanamke.

“Masalu jihurumie usije kufa kama dada yako Monika.”

“Mama mkiniua nani atakayebeba kidonda? Dada Monika alinieleza kuwa wote mliotaka kuwapa kidonda mizimu iliwakataa.”

“Ni kweli, lakini unatakiwa uionee huruma familia yako.”

“Mama ninyi hamnionei huruma, mimi nitawaonea vipi?”

“Kumbuka kama utaendelea kufanya kama usipokufa wewe basi utampoteza baba yako.”

“Mama kila mwanadamu hufa kwa ahadi ya Mungu na wala si kwa ajili yangu.”

“Kwa hiyo una mwanamke?”

“Nilikuwa naye lakini sasa hivi kabakia rafiki.”

“Mbona baba yako kaelezwa kuwa unautia mwili wako uchafu ndicho chanzo wa kidonda chako kukauka na kufanya mambo yote yaanze kusimama?”

“Lakini mama kama kidonda nimekubali kwa nini mniwekee vikwazo kwenye maisha yangu?”

“Si vikwanzo bali masharti ya mizimu.”

“Kama ni masharti ya kunyanyasana mimi siyawezi, kama mali zenu chukueni na mimi niacheni na maisha yangu.”

“Masalu unajiamini nini mwanangu?”

“Sina cha kujiamini bali ukweli ndiyo huo.”

“Basi baba nakuomba, nipo chini ya miguu yako, kama una mwanamke achana naye.”

“Nikueleze mara ngapi kuwa sina?”

“Najua tumekufanyia kitu kibaya lakini mabadiliko ya kidonda chako ni hayohayo.”

Niliachana na mama ambaye niliona na yeye ananizingua, sikutaka kukosa vyote, mavazi nilibadilika kuvaa siku zote nilivaa suruali za kitambaa ili kuogopa kukitonesha kidonda, sikuruhusiwa tena kuvaa viatu zaidi ya sandozi. Kila mmoja alinihoji uwezo wangu wa kifedha na mavazi yangu.

Nilikuwa na duka kubwa kuliko ndugu zangu, lakini wao ndiyo walionekana wana maisha mazuri. Nami sikutaka kushindana nao, kwa vile kidonda nilijua hakitoki mwilini mwangu nami niliamua kutumia kilicho ndani ya uwezo wangu.

Nilianzisha tabia ya kumhonga pesa mpenzi wangu ili naye afaidi kama ndugu zangu kutokana na kuonekana wao ndiyo wenye thamani. Siku moja niliamka asubuhi nyumbani kwangu kama kawaida na kushangazwa kukuta baba yangu na ndugu zangu wakiwa nje ya nyumba yangu.

Eti shida yao kubwa ilikuwa ni kunifumania na mwanamke, niliwashangaa watu wazima kama wale kuacha kazi zao za msingi kutaka kunifumania mimi. Ajabu ya Mungu siku ile mpenzi wangu hakulala nyumbani, sikutaka kupigizana nao kelele. Niliwaruhusu wamtafute, walifanya upekuzi bila kuona lolote.

“Jamani kama bado hamjaridhika semeni niwafungulie wapi mkatafute?”

“Wee chonga lakini lazima utakumbuka siku moja kuwa sisi tulitangulia kuzaliwa.”

“Hilo ni dua la kuku ambalo halitanipa asilani.”

USIKOSE SEHEMU IJAYO

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni