
Mtunzi: George Iron Mosenya
SEHEMU YA KUMI NA TANO
ILIPOISHIA...
ILIPOISHIA...
Baba yangu mzazi ambaye alipigana vita ya Majimaji huko Songea alikuwa akiniongezea ujasiri, ni kweli alikuwa akinyanyaswa na wazungu na aliwaogopa kweli lakini alikuwa akinieleza kuwa katika vita ile kwa mkono wake wa kuume akiwa na rungu kubwa aliwauawa wazungu watano.
JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈
ENDELEA...
Kwake ulikuwa ni ushindi mkubwa sana kumtandika mkoloni na bunduki yake mkononi.
Ni kweli watanganyika wengi walipoteza maisha lakini hii ilikuwa alama kubwa sana kuwa waliutaka uhuru kwa namna yoyote.
Baba alinieleza kuwa baba yake ambaye ni babu yangu alipoteza maisha kwa kunyongwa, na ni yeye ndiye alikuwa mmiliki wa jina la Nguzu ambalo maana yake ni NGUVU.
Jina Florian nilipewa na hawa ngozi nyeupe waliojifanya miungu katika ardhi yetu, silipendi jina hilo.
Naitwa Ngengekuzenza Nguzu. Yaani ‘Aliyerithi Nguvu’.
Baba yangu alinipatia jina lile kwa sababu aliniamini sana, nami nikajikuta najiamini mno.
Maisha magumu hayakuiathiri akili yangu, sijui mnaitaje kwa kizazi chenu hiki cha Tanzania, lakini wakati wa Tanganyika tulisema akili zinachaji, akili zangu zilikuwa zinachaji mno.
Nilifanikiwa kulimaliza darasa la nne la mkoloni.
Wakoloni bwana licha ya unyanyasaji wao lakini walikuwa makini sana, wakiona mtu ana akili sana wanamuwahi ili baadaye aje kuwa upande wao na aseme mazuri tu juu yao. Mkoloni akupatie elimu utaanzaje kumsema kwa mabaya angali tayari unaweza kusema’yes no’ kwa sababu yake!!
Hata mimi waliniwahi na hapa ndipo nilikutana na Joseph Kazeze.
Na upinzani ukaanza rasmi.
Wakatupeleka shule ya upili ambayo kwa sasa mnaiita Tabora boys lakini wakati ule iliitwa Tabora Central school. Ilikuwa shule ya vipaji maalumu haswa. Wanafunzi wengi walikuwa ni watoto wa machifu, ni baadaye sana walianza kuchukua wanafunzi wa kawaida.
Kwa wakati ule nadhani ni mimi na wengine wachache sana tuliokuwa tunasoma pale lakini si watoto wa machifu.
Mitihani ya hapa ilikuwa ni kutoka vyuo vya uingereza. Hawakutufundisha kuhusu yetu bali walitaka tuyajue yao.
Hata hayo yao bado nilipata alama za juu.
Urafiki kati yangu na Joseph Kazeze ukaanza kuyeyuka, hakutaka kupitwa alama na mtoto wa kimasikini kama mimi.
Tulipoenda jeshini mwisho wa kidato cha tatu kama ilivyokuwa ada nilikuwa bora zaidi yake katika kila kitu.
Hakupenda kabisa, ila mimi sikujua kama ni kwa kiasi kikubwa vile.
Tukarejea tena kumalizia kidato.
Katika uchaguzi nikateuliwa kuwania uongozi, Joseph naye akawania.
NIkamwangusha na kuwa kiongozi wake!
Wakati ananipa mkono wa hongera ndipo niliiona chuki katika macho yake.
Nikapuuzia.
Nikasema ikiwa wote tunatoka Mwanza, ya nini kuchukiana sasa. Nikadhani yale yataisha...
Kutingwa na uongozi nikasahau kabisa kuketi na Joseph tuzungumze.
Chuki ikakomaa!
Baadaye yakaibuka mapenzi, nadhani hapa ndipo chuki ilibalehe na kuota mapembe!
Joseph alimpenda binti ambaye alikuwa akinipenda mimi. Kuzidiwa huku kete Joseph akaleta ubabe na kunivimbishia kifua.
Mara ya kwanza nilimwacha, ya pili akanifuata tena akinitaka ugomvi, nikamweleza bayana kuwa sisi ni ndugu wa mji mmoja asiwe vile.
Akanipuuzia na siku hii akanisukuma nikaanguka.
Nilipoinuka nilimfundisha kuhesabu moja mpaka kumi kwa lugha ya kirusi.
Somo lilikuwa gumu na kila mara alianguka chini, kila akijaribu kunyanyuka namtandika ngumi ya uso. Akapasuka juu ya jicho lake, nami nikawa napiga palepale.
Siku hii nikatambua kuwa majina yana maana yake.
Ngengekuzenza Nguzu (Aliyerithi Nguvu)
Nilikuwa nimerithi haswa.
Ugomvi huu ulitikisa shule.
Ajabu yake ilikuja katika maamuzi, tulipigana na mgomvi alikuwa Jose lakini katika adhabu nikachukuliwa mimi.
Tabora Central School ilikuwa shule ya kijeshi wakati wetu, hata sare zetu zilikuwa za kijeshijeshi, tulivalia kombati za kaki kama wanazovaa wanamgambo, kila kitu kiliendeshwa kikakamavu, hapakuwa na adhabu za viboko.
Nilivyoadhibiwa nikikusimulia unaweza ukahisi huyu bwana kachanganyikiwa na sasa ananidanganya.
Niliingizwa katika chumba chenye giza nene na hapo nikaanza kulazimishwa kwenda mbele, kadri ninavyokwenda mbele ninazidi kuinama chini kutokana na muundo wa kile chumba, hatimaye paji la uso likayakaribia magoti.
Chumba kikabanwa nikawa siwezi kusogea mbele wala kurudi nyuma.
Niliumia mno, nikaamini kuwa sasa ninakufa.
Waliniacha kwa masaa mengi sikumbuki hata.
Waliponitoa nilikuwa nyang’anyang’a.
Wakanipelekaq msituni, huko sasa niliadhibiwa na wazungu. Walimwachia mbwa wao anikimbize na nilipewa ruhusa ya kukimbia kumzidi.
Nilivyochoka vile ningeweza vipi, si waliutaka uhai wangu tu wapuuzi wale.
Basi kama ni mchezo basi mbwa alipata wa kucheza naye, nakimbia hatua kadhaa naanguka mbwa anafika na kuning'ata wanamfukuza.
Wananiambia nisimame tena ninakimbia wanamwamuru mbwa anikimbize, ananifikia na kuniangusha ananing'ata.
Niliteseka mno!
Baada ya hapo nikapokea viboko kumi na viwili vya mkoloni.
Nilinyooka.
Joseph hakuadhibiwa nilipotoka kule kwenye adhabu nyinginyingi za kutisha nikaelezwa kuwa nimefukuzwa shule na wakati huohuo aliyechukua nafasi yangu katika uongozi ni Joseph Kazeze.
Nililia! Nililia sana.
Nikapakiwa katika gari moshi, elimu yangu ikaishia pale nikarejea kuwa mtumwa.
Nilipambana hivyohivyo hadi siku ile mwalimu Julius Kambarage Nyerere alivyokabidhiwa nchi huru.
Walau hali ikaanza kuwa ya heri, sikutamani kusoma tena.
Tayari nilikuwa nina familia ya mtoto mmoja niliyempa nikiwa Mwanza baada ya kufukuzwa shuleni.
Sikupata mtoto huyu na yule mwanamke aliyetuletea uhasama baina yangu na Jose. Nilizaa na maskini mwenzangu tukalea kimaskini hivyohivyo.
Niliamua kuanzisha familia kwa sababu sikuwa na familia tena, baba yangu alifariki na mama vilevile.
Halikuwa jambo la ajabu kwa wakati ile kupoteza familia yako.
Nikamsahau Joseph Kazeze katika kichwa changu. Niliamini yote yaliyotokea Tabora Central School ni mambo ya ujana tu.
Nilikuja kulisikia jina hili katika siasa.
Eti Joseph Kazeze ni mjumbe sijui wa kamati gani katika chama tawala. Hii ilikuwa mnamo mwaka 1977. Niliamua nisijihusishe na habari zozote kuhusu Jose kwa sababu kwa kufanya hivyo nilikuwa nakumbuka chanzo cha mimi kuishia kati katika masomo yangu na sasa sina thamani yoyote katika jamii.
Miaka mitatu baadaye yule mwanaharamu akaanza kunizongazonga tena.
Alinibomolea nyumba yangu. Japokuwa hakuja yeye moja kwa moja lakini nilijua kupitia waliokuja, akanibambikiza kesi kadhaa bahati nzuri ilikuwa upande wangu nikawa natoka salama.
Huwezi kuamini, akavuka mipaka baada ya kuona kila analofanya si kitu kwangu.
Hivi unaweza ukaamini Jose Kazeze akaamua kumposa upya mke wangu!
Andika kila ninachokueleza usiache walau neno moja, yote yana maana sana.
Nd’o hivyo bwana Joseph akamlaghai mke wangu ajuavyo yeye, alikuwa na gari lake aina ya Land Rover ya chama tawala basi aliitumia hii kuishika akili ya mke wangu.
Yule mwanamke naye alikuwa mjinga kweli, ujue nilishamweleza kinagaubaga kuhusu uhuni wa Jose lakini akashawishika akaniacha eti.
Hivi kama sio kuumizana nafsi ni nini hiki, kweli Joseph ambaye alikuwa ana pesa tayari anaamua kuniingilia anga zangu, tena bora ingekuwa kwa mwanamke ambaye ni kigoli, mwanamke huyu alikuwa amecharazwa bakora za mkoloni haswa hatamaniki, alikuwa amechanjwa mwili mzima chanjo za kinga ambazo ziliaminiwa na makabila mbalimbali. Haya yote akajifanya hayaoni.... akaamua kuniadhibu.
Alifanikiwa!
Nilimwambia mwanangu juu ya alichonifanyia mama yake. Nilimweleza huku ninalia.
Akatangaza kumchukia milele!
Basi rafiki yangu akabaki kuwa huyo mwanangu wa pekee, niliyemuita jina Salama.
Mama Salama akahamia katika maisha ya Joseph Kazeze.Iliniuma mno, huyu bwana katumia cheo chake kulipiza kisasi angali mimi sikufanya lolote enzi zile Tabora kwa kumkomesha.
Sasa mwanamke nikamuachia, sifa zote nikamuachia lakini yule bwana kumbe hajaridhika.
Hapo sasa zile jazba za enzi za shule zikarejea nikajisema kuwa nchi hii ni huru kabisa, tena sio uhuru wa bendera. Hakuna utumwa tena labda ukusudie mwenyewe. Ajabu anajitokeza mjinga mmoja mwenye ngozi kama yangu ananirudisha utumwani.
Siku ya tukio sikumuaga Salama!
“Naomba kwa leo tuishie hapo mzee wangu Majenga..... sitaki kusikia kilichotokea. Nakuomba sana alfajiri tutaendelea na mkasa huu. Nimefurahi sana kukukuta ukiwa hai mzee. Na badi nashangaa uliweza vipi kutunza karatasi hizi kila ulipoenda na kutarajia siko moja utamsomea mtu” Martin Nguzu lizungumza kwa hisia kali, sauti yake ilikuwa baridi mno. Alikuwa ameguswa mno na maandishi yale.
“Niliwahi kumsomea mama yako, sijui hata kama alinisikiliza kwa makini maana alikuwa analia kila akisikia lolote kuhusu hayati Ngengekuzenza Nguzu ambaye ni baba yake mzazi.” Alijibu Majenga kwa utulivu.
Na hapo akaitoa miwani yake usoni.
Akajifuta machozi.
“Babu yako alikuwa mtu wa aina yake sana. Namuona hai ndani ya macho yako...” Akaongezea huku akimshika begani Martin Nguzu.
Nguzu akamsaidia kuinuka, akamkokota mpaka ndani akamsaidia kukiandaa kitanda chake akamwacha akilala. Naye akaenda katika chumba kingine akalala.
Wakati Martin Nguzu na mzee Majenga wanakubaliana kulala ili siku inayofuata waendelee kusoma maandishi yale ambayo Nguzu aliamini kuwa si haba yatampa mwanga kidogo juu ya matukio yote yanayotokea. Upande mwingine palikuwa panapambazuka.
Inspekta Kobo akiwa na pingu miguuni na mikononi mwake alikuwa katika mahojiano mazito sana.
Mdomo wake ulikuwa umeanguka na na kubaki wazi kutokana na kipigo kikali alichopokea, midomo hii iliyokosa ushirikiano ilisababisha udenda ulioambatana na damu umwagike katika namna ya kusikitisha sana.
Mguu wake uliokuwa umeunganishwa kwa vyuma ulikuwa umepigwa na sasa baadhi ya vyuma vilikuwa vinachungulia nje.
Damu nzito iliyoganda katika chuma kile ilisaidia kuficha ukweli wa mambo.
Inspekta hakuwa na uwezo wa kutembea na hakulazimishwa kutembea badala yake aliburuzwa hadi akafika mahali alipohitajika.
Macho yake mekundu yalikuwa makubwa sana, na yalikuwa yakiviringika huku na kule katika namna ya kuomba huruma ya yeyote yule mwenye mamlaka ya juu yake.
Hakutokea japo mmoja wa kumtetea.
Maelezo aliyokuwa ameyatoa waliosikiliza hayakuwakuna kabisa na hivyo wakaona suluhu ni kumbana vyema kwa kumuumiza ili aweze kutapika siri zote alizomeza.
"Inspekta Kobo, hili ni agizo la mwisho kabisa la kukubembeleza wewe kusema ukweli wote ili ubaki kuwa salama ama la tutatumia nguvu.
USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA
Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi