Machapisho

BABA KIUMBE WA AJABU (4)

Zephiline F Ezekiel
Mtunzi: Ally Mbetu

SEHEMU YA NNE
TULIPOISHIA...
Nilimuhadithia baadhi ya mambo kisha nilimueleza ya yeye kulima wakati tuna pesa.

“Eti mama hata kulima kwako amesema ni imani za kishirikina iweje tuwe na pesa wewe ulime wakati ungewalipa watu wakatulimia?”

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

SASA TUENDELEE...
“Mmh, mbona makubwa!” Mama alizidi kushangaa.

Mama alisema huku akitoka shambani na kunisogeza chini ya mwembe.

“Masalu wewe hayo unayaamini?”

“Siwezi kuyaamini japo kuna mengine yana ukweli.”

“Nakuomba asikubaliane na maneno ya Monika ni ya uongo.”

“Mama mbona baba alisema jana litakalomtokea asilaumiwe, nini kitamtokea dada Monika?”

“Wee Masalu!” Mama alizidi kushtuka kuona ninajua vitu vingi.

Ilionesha mama aliamini siyajui mengi kuhusiana na mambo yaliyokuwa yakitendeka nyumbani. Nilimuona akifuta jasho kwenye paji la uso kisha alinipandisha na kunishusha na kusema.

“Masalu wewe ni mtoto, hujui kitu hata nikikueleza hutanielewa, nakuomba uachane na hayo, swali hili ungemuuliza baba yako mngekosana.”

“Mama hujanijibu, jibu si kukosana bali kupata ukweli nilioelezwa na dada Monika juu ya kukataa kwake kidonda na baba kumtishia kuyakatisha maisha yake.”

“Hilo si kweli, ni ujinga wa dada yako kama kufa atakufa na yake.”

“Mama, baba aliposema kuwa asilaumiwe na wewe kusema shauri yake alikuwa na maana gani?”

“Masalu naomba usiniulize swali kama hilo tena,” mama alikuwa mkali.

Niliona nibadili mada kwa kumuuliza swali lingine.

“Halafu mama kwa nini tusitafute mtu atulimie na wewe kupumzika, tuna faida gani kuwa na pesa na wewe mama unaendelea kuteseka?”

“Masalu nakuomba uondoke, nakuona umekosa maneno ya kuzungumza,” mama alikuwa mkali.

Kila neno nililolisema kwa mama lilimuudhi, sikutaka kuendelea kulumbana naye, niliamua kurudi zangu nyumbani nikiwa bado nipo njia panda. Wazo la haraka lilikuwa kwenda kwa dada Monika kumueleza akubaliane na matakwa ya wazazi ili asije kujutia maisha yake. Nilipofika nyumbani nilijawa na mawazo mengi sana kuhusiana na majibu ya mama.

*****

Nilipanga siku ya pili nitaaga na kwenda shule lakini kituo changu cha kwanza kingekuwa kwa dada Monika kumueleza hali halisi kutokana maneno ya baba. Siku ile sikushinda na furaha kila nilipokumbuka ndoto nilizoota usiku na majibu ya mama.

Japo niliamini mama hawezi kumueleza baba niliyomuuliza, bado nilikuwa na wasiwasi kama atamueleza basi lazima baba angenishikisha adabu kufuatilia mambo yasiyonihusu. Lakini siku ilikatika bila kuulizwa swali lolote na baba zaidi ya mama kuniita na kunionya nisirudie tena kuuliza mambo yale wala kumueleza mtu yoyote.

Nilimuahidi mama sitarudia kumueleza mtu maneno yale, kwa furaha ya mama alinipa pesa za kula shule kitu ambacho hakuwahi kukifanya zaidi ya kila siku kunipa nauli tu. Niliamini ile itanisaidia kuongeza nauli ya kwenda kwa dada. Usiku nilipolala ndoto ya jana yake ilijirudia.

Nilijikuta nikikesha kwa mara nyingine mpaka asubuhi kwa kuogopa kila nilipofumba macho njozi mbaya zilinifuata. Chumba nilikiogopa na kujiuliza njozi zile mbaya za dada Monika kuliwa nyama huku familia yote ikifurahia zilikuwa na maana gani? Kingine kilichonitisha mguu wangu kuoza na kutoa wadudu.

Nilijikuta nikiogopa kufumba macho na kubaki macho mpaka kunakucha, alfajiri nilisikia habari zilizonishtua sana. Nilimsikia baba akimwambia mama:

“Aliyoyataka mwanao yametimia.”

“Unataka kuniambia Monika ame...”

“Ishia hapohapo na sitaki utoe chozi unajua nini tuliambiwa.”

Nilishtuka na kutoka nje na kuwakuta baba na mama sebuleni, mama aliponiona alishtuka tofauti na baba.

“Mama dada Monika kafanya nini?”

“Kwani umesikia nini?” Baba aliniuliza.

“Sijui...ame..”

“Amefanya nini?”

“A..me..mee,” nilijikuta nikipata kigugumizi.

“Hebu ondoka hapa asubuhi yote nini kimekuamsha,” baba alinifokea.

Nilirudi chumbani kwangu nikiwa bado sielewi dada Monika kafanya nini japo bado wasiwasi wangu ulikuwa labda amefariki kutokana na maelezo ya dada Monika na kauli ya baba juu ya dada Monika. Kwa kauli ya baba ambayo aliifunga, niliamini kabisa dada Monika huenda kweli amefariki. Kwa vile muda wa kujiandaa kwenda shule ulikuwa umekaribia nilikwenda kuoga ili nijiandae na shule.

Baada ya kuoga nilirudi chumbani kwangu kujiandaa kwenda shule, nikiwa bado nipo katika maandalizi nilishtuka kusikia sauti za ndugu zangu, ujio wao wa asubuhi ile ulinishtua sana.Niijiuliza kuna kitu gani kimetokea au ndiyo niliyokuwa nayafikiria ya kifo cha dada Monika? Sikutaka kutoka haraka, nilimalizia kuvaa nguo za shule, baada ya kuvaa nilitoka ili nijiandae.

Nilishtuka kuwaona dada na kaka zangu wamekaa sebuleni, waliponiona walishtuka na kuniuliza:

“Masalu unakwenda wapi?”

”Shule.”

“Unakwenda shule hujui hapa nyumbani kumetokea nini?”

”Sijui.”

“Mmh, makubwa, Monika amefariki.”

“Eti?

“Monika amefariki.”

“Dada Monika?” Bado sikuamini.

“Eeeh, huyo huyo.”

“Siamini …siamini.”

Bila kujielewa nilijizoa mzimamzima na kujipiga chini na kupoteza fahamu, baada ya huduma ya kwanza nilipata fahamu na kuangua kilio tofauti na wenzangu ambao hakuna hata mtu mmoja aliyemwaga chozi. Juhudi za kunibembeleza zilishindikana. Bila kujielewa nilijikuta nikisema kwa sauti ya juu:

“Yote uliyonieleza dada yangu nilifikiri utani kumbe kweli wamekuua.”

“Alikueleza nini?”

”Baba kwa nini umemuua dada Monika?”

“Wee Msalu maneno gani hayo?”

“Maskini dada yangu kumbe ulikuwa na siri nzito moyoni mwako ambayo imenifumbua leo, ungekufa dada yangu bila kujua lakini Mungu mkubwa.”

“Masalu hebu ondoa uchuro hapa.”

“Siwezi… siwezi, kwa nini lakini umemuua dada Monika?” Niliendelea kulia kwa uchungu huku nikijipigiza chini.

“Nani kamuua Monika?”

“Nyinyi wote kwa tamaa za mali.”

“Masalu unatukosea adabu.”

“Siwakosei adabu bali ukweli ni huo.”

Kaka mkubwa alinichukua na kutoka na mimi uani huku nikiendelea kulia, roho iliniuma kumpoteza kipenzi dada yangu Monika mtu aliyenipenda kuliko yeyote. Kutokuonesha ndugu zangu kuguswa na kifo cha Monika niliamini ndoto niliyoota ilikuwa na maana kubwa. Kama dada Monika wamemla nyama nini maana ya kidonda mguuni kwangu chenye kutoa wadudu?

****

Tulipofika nje kaka alinibembeleza na kunieleza maneno ya busara kuhusiana na kifo cha Monika kuwa kilitokana na uzazi wala hakihusiani na masuala ya ushirikina. Na kutokuonesha kuguswa kila mmoja alikuwa akililia moyoni kwa vile hakuna aliyetegemea.

Kwa vile nilikuwa namheshimu nilimkubalia ili kumridhisha lakini siri ilibakia moyoni mwangu. Wengi walishtuka maneno yangu na kunionya nisiyasikilize ya Monika kwa vile alikuwa ni muongo na mgombanishi, nao nilikubaliana nao ili yaishe.

Ajabu ya mwaka ambayo baada ya akili ya ufahamu kukomaa niligundua kuna kitu kilitendeka mpaka leo hii sijui. Baada ya taarifa za msiba wa dada Monika ambao hakuna aliyefunua mdomo wake kulia zaidi yangu mwenyewe.

Taarifa za msiba ule hata majirani hawakujua nyumbani kulitokea msiba. Mwili wa dada ulifuatwa na kurudishwa nyumbani. Gari lililouleta mwili wa dada ilipita mpaka uani. Waliuteremsha na kuuingiza chumbani kisha ndugu wote walitawanyika kwenda kuendelea na kazi zao kama kawaida. Kitu kile kilinishtua iweje kuwepo na msiba hakuna mtu aliyeguswa wala taarifa kuwafikia majirani.

Usiku nilipelekwa kwa kaka ambako nililala siku mbili na kurudishwa nyumbani, niliporudi hali ilikuwa ileile na kunifanya niwe na mawazo ni kweli dada alikufa au taarifa zile zilikuwa mgonjwa mahututi? Kwa hiyo yupo hospitali, sikutaka kuhoji haraka baada ya wiki sikuona mabadiliko wala taarifa zozote za dada Monika.

Hata majirani waliotuzunguka hawakujua kitu zaidi ya ndugu wa mpenzi wa dada Monika kuulizia dada alizikwa wapi. Maswali yale kwa kweli yalinichanganya sana. Kila nilivyojitahidi kuchunguza sikupata taarifa zozote zaidi ya watu kufurahia maisha.

Mwezi ulikatika nikiwa bado njia panda kuhusu maswali dada Monika wakiulizia mazishi yake yalifanyika lini na kwa nini baba hakuwataarifu kama kuna msiba, kama majirani wajumuike pamoja katika msiba ule. Siku moja nilikwenda hadi Mkuyuni kwenye nyumba aliyokuwa akikaa dada Monika.

Nilikuta mlango umefungwa, kuuliza nilishindwa kutokana na kuogopa maswali huenda amekufa na kunifahamu mimi ni nani. Niliamua kurudi bila kupata jibu kuhusiana na kupotea kwa dada Monika kwamba amekufa kweli au hali yake ni mbaya. Lakini nilikumbuka kaka mkubwa aliniambia kuwa Monika alikufa kutokana na uzazi.

Nilijiuliza kama alikufa alizikwa wapi na kwa nini majirani hawajui lolote, na kama kweli alikuwa amekufa mazishi yake yalifanyika wapi. Kutokana na kuja mjini muda mrefu mazishi yote tuliyafanyia mjini. Ingekuwa kama wengine mazishi huyafanyia vijiji walikozaliwa lakini dhana ile baba aliikataa.

Bado sikutaka kukubali, nilizunguka kwenye makaburi labda nitaliona kaburi jipya la dada Monika, lakini sikuona kitu chochote zaidi ya makaburi mapya yenye majina tofauti na la dada Monika. Nilibakia njia panda siku zote kujiuliza ni kweli dada Monika alikufa au yupo kwa mganga.

Siku moja nilikutana na shemeji aliyekuwa akikaa na dada Monika, nilimuulizia kitu ambacho kilionekana kituko mbele yake.

“Shemu za siku?”

“Nzuri sijui zako?”

“Eti shemu dada Monika yupo wapi?”

“Masalu swali gani hilo? Ina maana mtu akifa huwa anakwenda wapi?”

“Una maana ni kweli dada Monika amekufa?”

“Masalu kioja gani unataka kunionesha, ina maana wakati Monika anakufa wewe ulikuwa wapi?”

“Sasa kama amekufa maiti yake imezikwa wapi?”

“Mimi nitajua wapi, wakati nilifukuzwa?”

“Kama kazikwa mbona hakuna kaburi lake?”

“Masalu upo sawa?”

“Kwani wewe unanionaje?”

“Nakuona haupo sawa.”

“Nipo sawa na akili timamu.”

“Kama kweli una akili timamu usingeniuliza suala la kifo cha Monika.”

“Shemu kama dada alikufa mbona wewe mumewe haukuwepo msibani?”

“Masalu, nilifukuzwa kama mbwa na kutishiwa maisha, kwanza nikionekana nimesimama na wewe nitajitafutia balaa.”

“Shemu una uhakika Monika amekufa?”

“Ndiyo.”

“Ulimshuhudia kabisa amekufa?”

“Monika amefia mikononi mwangu na kuna mengi alinieleza ya kukueleza lakini sikupata muda wa kuonana na wewe. Kama ni kweli aliyosema Monika basi familia yetu itakuwa ina hatari kubwa.”

“Kuhusu utajiri?” Nijikuta naropoka.

“Nalo hilo alilizungumzia, ila wamemtesa sana mke wangu mpaka kifo chake. Kibaya wamemuua hata mtoto wangu aliyekuwa tumboni bila kosa, yaani siamini familia yako kuna na roho mbaya kiasi hicho. Kama mtu kawapatia utajiri akisema amechoka na yeye anataka maisha yake kuna ubaya gani?”

USIKOSE SEHEMU IJAYO

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni