BABA KIUMBE WA AJABU (7)

Zephiline F Ezekiel
Mtunzi: Ally Mbetu

SEHEMU YA SABA
TULIPOISHIA...
“Nimekuelewa mama yangu, nimekuelewa sina budi kukusikiliza.”

“Asante Masalu, siku zote niliamini wewe na Monika ndiyo watoto wangu wanaonijali,

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI

SASA TUENDELEE...
endelea kunijali mwanangu wewe ndiye tegemeo langu, soma unikomboe.”

“Nitafanya hivyo mama yangu, nakuahidi kuwa kimbilio lako.”

“Asante mwanangu.”

Baada ya mazungumzo marefu tulirudi nyumbani, lakini bado aliniacha na maswali lukuki moyoni mwangu, nilijikuta nakubaliana na shemeji, bwana wa Monika kuwa mwili wa dada umefichwa ndani pamoja na mtoto wa dada Mihayo.

                                            SIKU TATU BAADAYE

Siku tatu baadaye nilipata taarifa za kusikitisha za kifo cha utata cha shemeji aliyekuwa bwana wa Monika. Taarifa zilizonitisha na kuamini mazungumzo yangu na mama juu ya taarifa zinazosambazwa na shemeji zilimfikia baba na kuamua kufanya umaruhuni wake.

Ndugu walisema aliporudi nyumbani alianza kusema anasumbuliwa na kichwa huku akisema kama akifa atakuwa ni baba. Na usiku alipiga kelele akilitaja jina la baba, kitu kilichozidi kuaminisha kwamba anahusika moja kwa moja ili kumkomoa baada ya kusikia akitutangazia sifa mbaya familia yetu.

Kifo kile kiliongeza sifa mbaya kufikia hatua familia ya aliyekuwa mpenzi wa marehemu dada Monika kuja kutushambulia kwa maneno ya kutuita wachawi. Siku hiyo nilikuwepo, mama wa marehemu alikuja nyumbani na kuanza kutoa shutuma nzito kwa sauti ya juu huku watu wakisikiliza.”

“Mmeniulia mwanangu kwa imani zenu za kichawi ili muwe matajiri, kumuua mtoto wa Mihayo hamkuridhika mmemuua Monika na kumficha ndani bado tu mmeona haitoshi mmemuua mwanangu. Nawaambia damu ya mwanangu haiendi bure.”

Taarifa zile zilipelekwa kwa baba ambaye aliita polisi na kumchukua yule mama na kumpeleka kituoni. Kwa kweli kilichoendelea sikujua zaidi ya kumsikia baba akitamba atamuonesha. Pamoja na yule mama kupelekwa polisi familia yetu ilitawaliwa na sifa mbaya ambazo wengi walizisikia na kuzisambaza kwa watu kuwa maisha yetu yametawaliwa na utajiri wa kishirikina ambao ulikuwa ukipitia kwenye kidonda cha marehemu dada.

Nilijikuta nikiishi maisha ya kukosa amani, hata tembea yangu ilikuwa ya mashaka kwa kuhofia maneno ya watu. Siku zilikatika walisema mchana, usiku wakalala. Walizungumza sana mwisho wakanyamaza na kusahaulika na maisha yakaendelea.

Katika maisha yetu hakuna kilichobadilika, nilimaliza kidato cha nne kwa kupata matokeo mabaya. Niliamini kufanya vibaya kulitokana na migongano ya mawazo iliyotokana na kuchanganywa na mambo yote yaliyotokea yakihusu familia yetu, na taarifa nilizopewa na dada Monika juu ya kifo chake na matukio mengi ya kishirikina yaliyoilenga familia yetu.

Wazo la kurudia mtihani wa kidato cha nne, lilipingwa na baba na kusema atanipatia shughuli nyingine. Roho iliniuma kwani ndoto zangu zilikuwa kusoma kwa bidii ili siku moja nimkomboe mama kwenye mateso ya kuwekwa kifungoni na baba.

Miezi sita baada ya matokeo mabaya ya kidato cha nne, baba alionesha mapenzi makubwa kwangu tofauti na zamani. Alifikia hatua ya kuzunguka nami kila kona kwenye shughuli zake. Siku nyingine alinipa pesa za matumizi ambazo alinieleza ninunue kitu chochote nikitakacho.

Kwa akili za kitoto nilianza kubadilika na kuyaona yote niliyoelezwa juu ya ukatili wa baba ni uongo. Baba alikuwa mtu mzuri kwa kuninunulia nguo za thamani, nilionekana kweli mtoto wa mtu mwenye pesa tofauti na mwanzo nilivyokuwa nasoma shule.

Baba siku zote alinisifia kuwa mimi ndiye mtoto anipendaye kuliko wote, kauli zile za baba zilinifanya nisahau hata wazo la kumuuliza juu ya dada Monika. Siku moja tulikuwa tumekaa kwenye moja ya hoteli ya baba huku akiniruhusu kula nikitakacho, baada ya chakula baba alinichukua na kuingia naye kwenye ofisi yake iliyokuwa ndani ya hoteli ile ambayo sikuwahi kuingia siku za nyuma.

Baada ya kuingia ofisini baba aliendelea kunimwagia sifa.

“Masalu unajua nakupenda sana kuliko watoto wangu wote.”

“Najua baba.”

“Hebu niambie unataka nini nikufanyie ili ujue napenda sana.”

“Cha kwanza kunipa nafasi ya kurudia masomo niliyoanguka katika mtihani wangu ili nifanye vizuri, bado nina hamu ya kuendelea kusoma.”

“Tofauti na hilo?”

“Siwezi kusema kwa sasa mpaka nitakapofanya mtihani wangu wa marudio.”

“Masalu, kusoma si muhimu sana kwako, kama pesa zipo nitakufungulia mradi wako ili uendeleze maisha yako.”

“Lakini…”

“Masalu hakuna haja ya kubishana, naomba ujiandae kuna duka moja nimelifungua na kuanza kazi wewe ndiye msimamizi mkubwa.“

Nilijikuta nakosa cha kuzungumza na kukubaliana na baba japo nafsi yangu ilitaka kusoma ili nimkomboe mama yangu. Nilijua kukubali mradi ule japo utakuwa chini yangu bado utakuwa wa nguvu za kishirikina kwa kuhofia huenda siku za mbele baada ya kuoa na kupata mtoto akatolewa kafara.

Baba alinitolea hati za kumiliki duka lile lenye jina langu na kunionesha sehemu ya kusaini. Nilisaini na kuniahidi kunifanyia mambo makubwa kuliko ndugu zangu wote. Baada ya kutoka pale aliniingiza kwenye gari lake na kunipeleka mjini Barabara ya Pamba kwenye duka langu.

Nililikuta duka lipo wazi na watu wakiendelea na mauzo ya vitu, lilikuwa duka kubwa la kuuza vitu vya jumla na rejareja. Tulipofika dada mmoja ambaye alikuwa akinifahamu aliniuliza:

“Leo Masalu ndiyo umeamua kuja?”

“Alikuwa anamalizia masomo,” baba alijibu.

“Karibu bosi.”

“Asante.”

Nilijibu huku nikiingia dukani na kwenda kukaa kwenye kiti changu kilichoandaliwa kwa ajili ya kukalia niwapo kazini. Baada ya kukagua duka lililokuwa likilingana na maduka ya ndugu zangu, baba aliondoka na kuniacha nisimamie duka langu.

Alinipitia jioni na kunirudisha nyumbani, nilipofika nyumbani nilimueleza mama kuwa nimepewa duka na baba. Ajabu mama badala ya kufurahi alitokwa na machozi, kwa vile tulikuwa peke yetu nilimuuliza:

“Mama unalilia nini?”

“Mmh, najua hukufurahi na unaweza usifurahi.”

“Kwa nini mama?”

“Ni vigumu kunielewa kwa sasa lakini tumuombe Mungu aepushe mbali.”

“Mama mbona sikuelewi?”

“Suala la shule limeishia wapi?”

“Baba amekataa na kusema tayari ameishanifungulia duka, na leo ndiyo nimekabidhiwa rasmi.”

“Mmh! Haya”

“Kwani kuna nini?”

“Hakuna ubaya.”

“Mama kuna kitu hutaki kuniambia.”

“Hakuna kitu kikubwa zaidi ya kukatika kwa ndoto yako ya kusoma.”

“Mama nitasoma tu.”

“Kwa duka lako, si unawaona ndugu zako walivyo bize na maduka yao hata muda wa kunikumbuka hawana.”

“Mama nitajipanga, siku hizi kuna masomo ya jioni.”

Siku zilikatika, biashara nayo ilizidi kushika kasi, hata mwili wangu ulibadilika na kuonekana mtu mzima kutokana na kunenepa, hata sauti yangu ilibadilika. Lakini ilikuwa tofauti na wenzangu, mimi nilibakia nyumbani na mama pamoja na mfanyakazi mmoja, niliamua kumpumzisha mama kazi za shamba, lakini mama aling’ang’ania kwa kusema kama akiacha kwenda shamba atafukuzwa na baba.

Nilipomuuliza baba naye alinijia juu na kunionya nisiingilie mambo yake, sikuwa na jinsi, nilimuacha mama aendelee kulima huku nikitumia vijana kumsaidia mama, ambaye alifanya kazi ndogondogo. Kingine ambacho sikukubaliana na baba ni kuhusu mavazi ya mama yaliyokuwa yamechoka.

Hapo sikukubali hata kidogo na nilikuwa tayari kwa lolote.

“Masalu unataka tubishane?” baba alinikaripia.

“Kwa hili baba sikubaliani nawe hata kidogo.”

“Umeanza kuvimba kichwa kwa vipesa unavyopata?”

“Si kuvimba kichwa, nipo sahihi, kama mali zako chukua lakini nimechoka kuiona hali hii mpaka lini?”

Sikuogopa chochote cha baba mpaka tulipokubaliana kumnunulia mama nguo mpya, pamoja na mzozano huo bado baba hakuonekana kukasirika sana. Mama alibadilika na kuanza kuvaa vitenge vya gharama, hata kandambili alivaa mpya.

Ndugu zangu walipokuja nyumbani hawakuamini kumkuta mama yetu kapendeza. Walipomuuliza aliwaeleza ni kwa ajili yangu, walinifuata kutaka kujua nimewezaje kumbadili baba kukubali mama kuvaa nguo mpya. Niliwaeleza ni msimamo hakuna kitu kingine, maisha yaliendelea.

Katika vitu ambavyo baba alinionya ni kutembea na wanawake, nilikumbuka kauli za dada Monika kuwa alianza kuelezwa asijihusishe na wanaume na mwisho alipata kidonda cha kichawi.

Nilimkubalia kumridhisha tu, lakini niliendelea kuwa na uhusiano na binti mmoja ambaye ndiye tuliyepanga kuoana siku za mbeleni. Siku zote mambo yangu nilikuwa nayafanya kwa siri kubwa bila baba kujua kwa kuamini sina uhusiano wa kimapenzi na mwanamke.

                                                                       ****

Siku moja nikiwa nimelala niliota kitu kama nyoka, lakini sikukielewa vizuri kikiniuma kwenye mguu wa kulia kwa ndani. Nilishtuka lakini hakukuwa na kitu chochote, niliendelea kulala. Kesho yake nilikwenda dukani kama kawaida na kuendelea na shughuli zangu.

Wiki moja baadaye nilianza kusikia muwasho sehemu niliyoota nimeumwa na kitu kama nyoka. Nilimueleza mama asubuhi baada ya kujikuna mpaka kukaleta weusi sehemu iliyokuwa ikiniwasha. Mama alishtuka, jambo lililonitisha.

”Mama mbona umeshtuka?”

“Baba yako alikueleza nini?”

“Kuhusu nini?”

“Huo muwasho wako?”

“Hata, sijazungumza lolote.”

“ Mmh!” Mama aliguna.

“Unaguna nini?” nilimuuliza.

“Hapana.”

“Mbona kama unanitisha, unakuwa hauna tofauti na wa dada Monika?”

“Ni kweli.”

“Unataka kuniambia ndiyo huu?”

“Ndiyo.”

“Mungu wangu nimekwisha.”

“Wala hujaisha, ukifuata masharti yake hauna tatizo.”

“Kwa hiyo na mimi nitakuwa na kidonda kama dada Monika?”

“Ndiyo lakini hakiumi.”

“Na nikikosea nitakufa kama dada Monika?”

“Monika kafa na yake.”

“Mamaa, juzi tulizungumza nini, leo unanibadilikia?” Nilimuona mama akitaka kuficha mambo.

“Masalu nakuomba suala hili muulize baba yako na usimueleze kuwa tumezungumza.”

“Sawa mama.”

Niliachana na mama huku mwili wote ukininyong’ea kwa kujua niliyoelezwa na dada Monika yametimia.

Siku ile hata hamu ya kwenda kwenye duka langu sikuwa nayo, kwa kuamini nilikuwa nimeishaharibika. Nilishinda ndani huku nikilia lakini mama alitumia muda wake kunibembeleza kuwa sijaharibika kama ninavyo fikiria.

“Masalu usilie mwanangu.”

“Mama kwa nini mnanitendea unyama kama huu kosa langu nini?”

“Huna kosa mwanangu, kidonda hiki humfuata yule aliyeteuliwa na mizimu.”

“Wataniteua vipi wakati mimi sitaki?”

“Huwezi kukataa.”

“Mama nina malengo yangu wewe unajua.”

“Ni kweli, lakini hakuna wa kumzuia baba yako uamuzi wake.”

USIKOSE SEHEMU IJAYO

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni