Machapisho

BALAA (25)

Zephiline F Ezekiel
Jina: BALAA
Mtunzi: Halfani Sudy

SEHEMU YA ISHIRINI NA TANO
ILIPOISHIA...
Alimshika Mbili shingoni na kumrudisha Mbili ndani kwa nguvu. Sasa mkao ulibadirika....Daniel Mwaseba akakaa ule upande ulikokuwa mlango huku Mbili akiwa kwa ndani. Wote wakiwa wamejipanga tayari kwa mapambano. Mbili alikuwa na silaha ya kisu tu ambayo ilikuwa imetulia kiunoni,

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
kisu alichotumia kukata suruali ya Daniel Mwaseba. Daniel alikiona kile kisu pale kiunoni. Lakini hakujari. Sasa Daniel alikuwa anautambua vizuri sana uwezo wa watu wale kimapambano. Sasa aliamua kupiga mapigo ya nguvu! Mapigo hatari wanayofunzwa watu maalum ili kuwapiga watu maalum. Mbili nae alisimama imara....tayari kwa lolote. Daniel nd'o alianza kushambulia, alirusha kareti ya nguvu iliyokuwa inaelekea moja kwa moja katika shingo ya Mbili, lakini mbili aliiona. Kwa kasi ya haraka aliinama kidogo huku akiachia ngumi ya kwa mkono wa kushoto, ngumi iliyokwenda katika tumbo la Daniel. Lakini Daniel nae alijiandaa kwa hilo, aliikwepa ile ngumi kiufundi mkubwa. Sasa mafahari hawa wawili wakawa wanatazama.

Kila mmoja kasimama, tayari kwa lolote, tayari kwa chochote, muda wowote. Daniel ndiye alikuwa wa kwanza tena kuamua, alirusha ngumi nane za harakaharaka, nne kwa mkono wa kulia, nne kwa mkono wa kushoto lakini Mbili alizipangua zote, kirahisi sana. Zilikuwa ni ngumi mzito sana, ngumi moja ikitosha kabisa kumpeleka kuzimu mtu dhaifu kama wewe, lakini Mbili hakuwa mtu dhaifu, alikuwa mtu imara kabisa. Cha ajabu Mbili alikisahau kile kisu kiunoni....alikiacha kimetulia tu, labda alidhani atamuweza Daniel kwa mikono mitupu. Mbili nae alirusha ngumi usawa wa mwamba wa pua wa Daniel Mwaseba, lakini Daniel aliiona ngumi ile, aliikwepa huku akiachia ngumi ya nguvu sana kuelekea katika mbavu za Mbili.

Mbili aliguna kwa maumivu, alishika mbavu zake kwa mkono wa kulia, lilikuwa kosa! Daniel Mwaseba alipeleka ngumi ya nguvu katikati ya sura ya Mbili. Mbili alipepesuka huku akiwa amechanganyikiwa, ashike mbavu ama sura. Kubabaika kwake kulitoa mwanya mwengine kwa Daniel, aliruka juu huku akipiga teke la kinyumenyume, teke lilomkumba kwa nguvu Mbili na kwenda kumgongesha ukutani vibaya sana! Mbili alikuwa amepatikana. Daniel hakutaka kumpa nafasi, alienda na kifuti pale ukutani na kulipata tumbo la Mbili barabara. Mbili alitapika damu! Daniel alimkaba kabali Mbili, akainyonga ile shingo kwa nguvu kuelekea upande wa kushoto! Roho mbaya ya Mbili ilisalimu amri, roho iliuacha ule mwili dhaifu na kuelekea kusikojulikana. Baada ya kufanikiwa kumuuwa Mbili wa Six Killers Daniel Mwaseba akauacha mwili wa Mbili pale chini na kuusogelea ule mlango wa kile chumba cha chumba cha mateso.....chumba cha kifo!

Roho mbaya ya Mbili ilisalimu amri, roho iliuacha ule mwili dhaifu na kuelekea kusikojulikana. Baada ya kufanikiwa kumuuwa Mbili wa Six Killers Daniel Mwaseba akauacha mwili wa Mbili pale chini na kuusogelea ule mlango wa kile chumba cha chumba cha mateso.....chumba cha kifo! Alifungua mlango taratibu na kuchungulia kwa nje, kulikuwa shwari. Hakukuwa na lolote la kutilia shaka. Daniel Mwaseba akaiangalia ile nyumba ya bluu kwa hasira. Akijua kuwa watu wale makatili walikuwa mle ndani. Daniel Mwaseba akapiga hatua za haraka kuelekea kule kwenye nyumba ile ndogo ya bluu. Kule nje ya nyumba ile, walikokuwa Dokta Yusha na Mwanasheria mlevi waliomaliza usiku ule wakiwa katika hali ya kusubiri.

Hadi asubuhi inafika Dokta Yusha na Mwanasheria mlevi walikuwa bado wanasubiri, walikuwa hawajapata namna ya kuingia mle ndani ya kambi ya Six killers. Walibaki wamejibanza vilevile, sehemu ile nyuma ya mti mkubwa wakisubiri kudra tu za Mwenyezi Mungu ili waweze kuingia mle ndani. Na kwa bahati mbaya sana hadi sasa hizo kudra za Mwenyezi Mungu zilikuwa hazijawafikia bado..nao waliendekea kuzisubiri. Kule nje ya kambi Dokta Yusha na Mwanasheria mlevi bado walikuwa wanasubiri, walikuwa wanasubiri nafasi yoyote ile ya kuwawezesha kuingia katika kambi hatari ya Six Killers.

Hadi muda huo hawakuiona nafasi yoyote ya kuweza kuingia mle ndani. Na kwa kujificha tu pale nyuma ya mti sidhani kama wangeiona...... Hata wangekaa mwezi.... Baada ya kusubiri sana, Dokta Yusha alipata wazo na kumshirikisha Mwanasheria mlevi. Walikubaliana. Dokta Yusha alitoka pale nyuma ya mti walipokuwa wamejificha na Mwanasheria mlevi, kwa mwendo wa taratibu na umakini mkubwa alianza kuizunguka ukuta wa kambi ile hatari. Mwanasheria mlevi alibaki pale kwenye mti kwa dhumuni maalum. Yeye alikuwa anamlinda Dokta Yusha kwa macho na kutoa ishara endapo itatokea hatari yoyote. Hivyo ndivyo walivyokubaliana mashujaa wale. Dokta Yusha bila kujijua alikuwa anafanya mchezo wa hatari sana. Kuizunguka nyumba ile ilikuwa ni zaidi ya hatari, tena asubuhi namna ile.

Mzunguko ule wa Dokta Yusha hatimaye ulimfikisha sehemu ulipokuwepo ule mti ulio karibu na ukuta wa kambi ile, mti uleule aliotumia Daniel Mwaseba kuingia mle kambini. Dokta Yusha nae alipata akili sawa na alizopata Daniel Mwaseba. Naam Dokta Yusha alipanda juu ya ule mti. Tofauti ilikuwa wakati Daniel Mwaseba alipanda mti ule na kuingia ndani ya kambi usiku wa manane... Yeye alipanda katika mti ule asubuhi na kutaka kuingia ndani ya kambi ya Six Killers asubuhi. Dokta Yusha alikuwa amefanya jambo hatari sana, kujianika mbele ya wauaji hatari wa Six Killers namna ile. Dokta Yusha alifika hadi pale kileleni, juu ya ukuta. Kutokea kule kwa juu alishuhudia vizuri mandhari ya kule ndani ya kambi, ambayo yeye alikuwa anayafahamu vizuri kabla.

Kumbuka Dokta Yusha alipanda ule ukuta wa kambi ile hatari asubuhi jua likiwa limechomoza, na pia Dokta Yusha alikuwa kashawahi kuingia katika kambi ile, na kwa bahati nzuri zaidi alibahatika kutoka salama. Akiwa pale kwa juu alipeleka macho yake katika kibanda kilichokuwa pembeni kidogo mwa ile nyumba ya bluu. Dokta Yusha alikumbuka mengi sana wakati anakiangalia kibanda kile. Alimkumbuka yule askari aliyepoteza uhai wake katika kiti cha kifo ndani ya kibanda kile. Askari aliyekufa kwa kubadirika rangi na kuwa nyekundu sambamba na kiti kile na kupotea katika ulimwengu kwa kuyeyuka palepale katika kiti cha kifo. Dokta Yusha alimkumbuka yule jamaa aliyepambana nae katika kibanda kile, na kufanikiwa kumsukuma katika kiti cha kifo! Kilichopo ndani ya kibanda alichokuwa anakitazama.

Nae aliyeyuka huku akibadirika rangi sambamba na kiti. Akiwa kule juu Dokta Yusha alijipa moyo, huku akijivika ujasiri kuwa lazima akapambane! Sasa dokta Yusha alifuta kabisa hali ya hofu katika moyo wake na kuona ni heri kufa kishujaa, kuliko kuishi ukiwa unashuhudia maovu yakiendelea kufanyika ulimwenguni. Kilikuwa ni kiapo alichoapa Dokta Yusha akiwa juu ya ukuta hatari....na alipania kukitekeleza kiapo chake. "Nitakufa nikipambana..." Dokta Yusha alihitimisha mawazo yake kwa kujisemea mwenyewe kimoyomoyo. Kwa taarifa tu, ule mti uliokaribu na ukuta wa kambi ya Six Killers uliachwa kwa makusudi na kundi la Six killers sehemu ile. Hawakutaka kuukata ingawa walikuwa na uwezo huo. Ni Moja wa six Killers ndiye aliyeshauri mti ule uachwe, kwa makusudi ili utumike kama mtego.

Ndio...... Waliuacha mti ule wakijua adui yoyote akitaka kuingia katika ile nyumba lazima atautumia ule mti. Maana ndo sehemu pekee iliyokuwepo kwa mtu mjanja kuingia mle ndani ya kambi yao. Nao kule ndani hawakuzubaa hata chembe, wakiwa kule kwa ndani walikuwa wanaulinda kwa kuuangalia ule mti kila baada ya dakika tatu. Komando Moja wa Six killers akiwa kule kwa ndani alimshuhudia vizuri sana mtu akipanda katika mti wao. Mti wa mtego ulioachwa kwa sababu maalum. Na sasa sababu za kuachwa ule mti zilileta matokeo. Tena matokeo yenyewe yalitokea na kuonwa na Moja mtu ambaye ndiye alishauri mti ule uachwe kama mtego. Yeye ndio alikuwa zamu kuulinda mti ule. Na ilikuwa kazi rahisi sana kwake kumshudia mtu yule akiwa katika kilele cha ule mti wa mtego.

Na alimshuhudia yule mtu hadi jinsi akivyoruka toka kule mtini mpaka pale katika ukuta wa kambi yao. Alivyofika juu ya ukuta alimshuhudia mtu yule akiangalia kibanda chao cha kufanyia mateso..kibanda chenye kiti cha siri, kiti cha kifo! Moja alimtambua mtu yule... "Dokta Yusuph Shaweji, daktari mfukunyuku umekifata kifo chako! Tena umekifata ukiwa unakikimbilia kwa kasi! Hahaha...umekutana na malaika mtoa roho hahaha" Moja aliongea peke yake huku akitoka nje taratibu kwa kicheko chake cha karaha. Wakati uleule ambao Moja wa Six Killers alikuwa anatoka nje ya nyumba ile ya bluu ili kwenda kumvia na kumuua kabisa Dokta Yusha kama alivyojiahidi mwenyewe akiwa ndani ndio wakati uleule ambao Daniel Mwaseba alikuwa anatoka kule kwenye kibanda cha mateso.

Alikofanikiwa kumuua Mbili. E bwana wee! Komando namba moja wa kundi hatari la Six killers na Mpelelezi mahiri nchini Tanzania Daniel Mwaseba walikutana uso kwa uso.....Kumbuka Dokta Yusha bado yuko juu ya ukuta. Kwa upande wa jeshi la Polisi nalo halikulala kabisa, tangu siku ya kwanza kutokea kwa mkasa huu wa ajabu wa kupotea watu kimaajabu bila sababu kujulikana, jeshi la Polisi waliingia kazini. Jeshi la Polisi walianza

kufanya msako wao kimyakimya. Lakini kimyakimya yao haikusaidia chochote. Walikuwa wanazunguka palepale bila kujua chanzo cha upotevu wa watu wale, wala kujua ni nani akiyewaficha watu wale. Unaweza sema bora Dokta Yusha na Mwanasheria mlevi walipiga hatua kubwa sana kuwakaribia wahalifu kuliko jeshi la Polisi. Jeshi la Polisi hawakuwa wanajua lolote kuhusu uwepo wa kundi hatari la Six Killers ndani ya Kilwa. Mbinu ya kimyakimya ilivyoleta matokeo hasi hatimaye jeshi la Polisi waliamua kufanya msako wa hadharani. Makundi ya askari yalimwaga mitaani kujaribu kutafuta fununu yoyote juu ya kupotea kwa watu au mahali walikopelekwa na kwa lengo gani. Vijana wa Fresh Nigger walipata sana misukosuko ya kukamatwa na kupelekwa kituo cha polisi kwa mahojiano. Lakini hata hivyo hawakupata fununu yoyote ile, pamoja na kutumia hadi njia ya vitisho na mateso kwa wale waliokuwa wanawatilia shaka, kwa bahati mbaya kabisa hawakuwa wamepiga hatua yoyote ile.

*****

Inspekta Jasmine Wahabu, alikuwa askari wa kike. Askari shupavu na jasiri aliyekuwa anategemewa sana na jeshi la polisi nchini Tanzania. Inspekta Jasmine alishafanikiwa mara kadhaa kuwatia wahalifu nguli mbaroni. Kufanikiwa huko kwa Inspekta Jasmine kulifanya azidi kutegemewa na nchi, kutegemewa na jeshi la Polisi. Inspekta Jasmine alitegemewa pia na raia wema. Baada ya wiki kadhaa za kuwatafuta wahalifu pamoja na watu na wanafunzi waliopotea katika mazingira ya kutatanisha kugonga mwamba.

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni