KONSTEBO NGUZU (20)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA ISHIRINI
ILIPOISHIA...
Usingizi ulimkuta Nguzu akiwa katika uchambuzi hafifu wa kitabu hiki maarufu, alianza kwa kumpa kongole mwandishi Edwin Semzaba kwa kuandika kitabu hiki, kisha akahamia kwa Ngoswe na Mazoea na hadi anasinzia alikuwa amefikia mahali ambapo Mazoea ameanza kuzoeana na Ngoswe!

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
Hii ni baada ya Ngoswe kumuhadaa kuwa atamtorosha waende wote mjini......

Alisinzia akiwa anatabasamu, bila shaka ni vile visa vya Ngoswe vilimpa tabasamu.

ASUBUHI ilimkuta konstebo Martin Nguzu katika ofisi ya gazeti mojawapo kati ya yale yaliyoandika habari ya kifo chake na kisha kusemekana aliyeandika ni 'mwandishi wetu.

Kama ilivyomkera inspekta Kobo na kujikuta akiponyokwa na matusi ya kiitaliano, kwa Nguzu ilikuwa vilevile lakini hakuwahi hata siku moja kuota ndoto za kiitaliano.

Yeye aliponyokwa na matusi mfululizo ya kisukuma.

Lakini hakuishia kutukana tu, aliamua kupiga hatua na aliamini hatua hii inaweza kuwa ya muhimu zaidi kumfikisha katika hatua nyingine.

Akalisoma gazeti lile na kuyapata mawasiliano ya muhariri mkuu wa gazeti hilo.

"Huyu jamaa lazima anawajua waandishi wake wote, wenye majina na wasiokuwa na majina wanaojiita 'mwandishi wetu'. Atawataja ama atakula maumivu yao..." Alizungumza konstebo wakati akizungusha macho yake huku na kule kabla hajazama ndani ya ile ofisi.

Awali alipanga kwanza kumjua sura huyu bwana na kisha ajiweke katika lindo zuri aweze kuijua gari yake.

Baada ya kujua hayo angeachana naye na kisha kumpangia siku ya shambulizi.

Alijua kuwa amezisahau taarifa zile tayari, na hata hao akina'mwandishi wetu' walikuwa wanaendelea na maisha yao mengine.

Mambo yakaenda tofauti, Nguzu akiwa amejivesha miwani ya jua katika uso wake huku akiziachia nywele zake wazi kwa maksudi kabisa.

Hazikufanania na nywele za askari, hasahasa wa cheo cha konstebo.

Nguzu alikuwa katika hali ya utofauti.

Alianzia mapokezi na kuulizia ni wapi atampa muhariri, katibu muhtasi akauliza ikiwa ana shida binafsi ama ya kiofisi.

Maswali yao yaleyale kila siku! Nguzu alijisemea kabla hajajibu, "Shida ya kiofisi dada."

"Ok! nyoosha moja kwa moja hadi katika ile korido kisha pinda kushoto utaiona ofisi, keti katika foleni subiri huduma."

Nguzu akainama chini kidogo huku akijishika kifua chake kama ishara ya kushukuru.

Akatoweka!

Alimkuta bwana mmoja mwenye mvi akiwa anangoja kuingia, akaketi pembeni yake.

Bwana mwenye mvi akaanzisha soga kuhusu siasa mara ahamie katika mpira wa miguu, huku ndipo alizidi kumpoteza Nguzu.

Ushirikiano wake pekee ukawa 'ndio' ama kujichekesha.

Hatimaye mzee akaingia na kutoka baada ya muda mfupi.

Bila shaka muhariri hakuwa tayari kusikiliza soga nyingi kutoka kwa yule bwana.

Ikawa zamu ya Nguzu.

Hofu ikamwingia hakutambua kama yupo sahihi katika hatua ile ama ameitupa karata yake vibaya.

Akaufungua mlango na kuingia ndani huku akitambua kuwa yeyote yule anaweza kustaajabu kuhusu ile miwani lakini alifurahi kwa sababu ni watanzania wachache sana anaweza kukuona haupo sawa katika jambo fulani naye akawa kimya asikwambie badala yake anamweleza rafiki yake kisha wanacheka!

Hee! Watanzania?! Tusaidiane kujishangaa.

Kweli! hakuna aliyemuuliza.

"Karibu!" Sauti nyembamba lakini ya kiume ilimkaribisha huku mikono ikimwonyesha mahali pa kuketi.

Martin akaketi.

"Naitwa Sebastian! natokea Temeke Dar es salaam." Alianza kujitambulisha.

Muhariri hakuonyesha kujali juu ya lile jina, Nguzu akaendelea.

Sasa akayafungua magazeti kadhaa aliyokuwa ameyashika mkononi akayatua mezani.

"Nakusikiliza bro.." Sauti ile iliyotawaliwa na kiburi cha kuwa muhariri ilizungumza.

"Nilikuwa nataka kuuliza..."

"Ulikuwa unataka ama nd'o unataka kuuliza mkuu?!" Muhariri akamuwahi Nguzu.

Nguzu akafadhaika na kuamua kutuliza akili yake, tayari alishagundua kuwa alikuwa anakosa kujiamini.

Akajipa sekunde kadhaa akaingia tena kushambulia.

"Nauliza, hizi habari ambazo anaandika mwandishi wetu, ni nani anaziandika na kwa nini asijitambulishe kwa majina yake." Akaweka kituo.

"Samahani umeuliza ama umetoa lalamiko!" Muhariri mwenye nyodo akazungumza, sasa aliachana na kazi alizokuwa anafanya akamtazama Nguzu huku akiyabetua mabega yake.

"Nimeuliza."

"Ni utaratibu wa kiofisi. Ukihitaji ubadilishwe utapaswa kuandika barua na kuiweka kuleee kwenye sanduku la maoni. Sijui kuna la ziada lililokutoa Temeke bwana.... bwana..." Akalisahau jina lake na kulipuuzia.

Konstebo Martin Nguzu akanywea na kujiona anazidiwa karata hivihivi mchana kweupe.

Akapaniki!

Akasimama wima, akawa anayetafuta neno la kuzungumza linakikataa kinywa linarudi kichwani.

Akaona haifai kuendelea kusimama hivyohivyo.

"Huyu aliyeandika hii habari ni nani?" Akafoka. Bado alikuwa wima.

Muhariri hakuligusa lile gazeti badala yake akainyoosha shingo yake na kuona nini anaonyeshwa.

Akakutanisha macho yake na habari juu ya kifo cha Nguzu na kuhusishwa sababu za kimapenzi na mengineyo.

Akajikuta anarudi nyuma kwa kasi, uso wake ukiitangaza wasiwasi yake.

Akaishika simu na kutaka kubofya nambari kadhaa, palepale Nguzu akauwahi ule mkono na kuugandamiza.

Kisha ili kuimarisha usalama akachomoa kisu kikubwa kutoka katika ficho lake.

"Huwa ninaua bila taarifa maalumu, sipendelei ufe hivyo. Jibu swali langu." Hakuonekana kuonyesha mzaha.

Muhariri akalitambua hilo.

"Sijaandika mimi."

"Mwandishi wetu ni nani?"

"Mwandishi wetu... sim... simj.."

Ngumi kali ikatua katika shingo ya muhariri.

Ilikuwa ngumi maalumu kwa ajili ya kumzuia yule mwanadamu anayependa kuongea kwa sauti ya juu, kumpunguza uwezo wa kupiga kelele na kujikuta akinong'ona.

Nguzu alimwacha akihangaika pale akauendea mlango na kuufunga!

"Simu yako ya mkononi..." Alisema kisha akautega mkono wake. Muhariri akaikabidhi huku akilia kwa sauti yake ile nyembamba ambayo ngumi kali ilizidisha ule wembamba na kujikuta akigumia kama mtoto wa kike.

Nguzu aliipekua ile simu upesi upesi katika sehemu za jumbe mbalimbali, hakupata ujumbe wa kumvutia.

"Unapendelea kufia ofisini ama nyumbani kwako?"

"Si... aahm! nisamehe si... nitasema lolote utakalo."

"Unanijua mimi?"

"Sikujui."

"Ni nani huyu mwandishi wetu na anapatikana wapi?"

"Niliandika mimi... lakini hata mimi nilipewa."

"Nisikilize we fala.... ndoto yangu moja ambayo nahitaji kuitimiza ni siku moja nimuue mtu akiwa ofisini nimkatekate nimtie kwenye mfuko wa rambo, kisha nitoke na ule mfuko niingie nao katika daladala niutelekeze huko. Vyombo vya habari vishindwe kuelewa vitaandika nini kuhusu kifo hicho...... Nina hasira ya kutimiza ndoto zangu. Nakupa nafasi ya mwisho kujieleza ukitetereka natimiza ndoto yangu. Nakuhakikishia kuwa sitaacha walau tone la damu humu ndani kwa ajili ya wapelelezi." Nguzu alizungumza huku akiwa amemkazia macho muhariri.

Kijasho kikamwagika...

Akatapika kila alichokuwa anakijua katika ile habari iliyoandikwa na 'mwandishi wetu'.

_____

JAMBO la kwanza lililokituliza kichwa cha Martin Nguzu ni juu ya inspekta Kobo.

Nguzu alistaajabu asimini hata kidogo kuwa aliachoelezwa kipo kama kilivyo. Licha ya kukiri kuwa yule muhariri alikuwa 'chamtoto' sana na asingeweza kuficha lolote kwa kitisho alichompatia lakini bado hakutaka kumpatiliza na kumwamini kwa asilimia zote.

Nguzu alitoka pale moja kwa moja akisimamia wazo lake kuwa kwa namna yoyote ile ni lazima afike nyumbani kwa Koplo Zubeda, aliamini kuwa ni huku ambapo angeweza kuupata mwanga zaidi katika hatua zake.

Alikiri kuwa kuonekana kwake mbele ya Zubeda kutazua kizaazaa cha aina yake ambacho kinaweza kusababisha majirani wakajazana kutaka kujua nini kinatokea.

Nguzu akajipa tahadhari kubwa sana kuwa ni lazima umakini utangulie mbele kuliko kiherehere cha kutaka kukutana na Zubeda ambaye kichwani anaamini Nguzu ameuwawa.

Ili kuondoa macho mengi kumfuatilia juu ya alichokuwa anahitaji kufanya Nguzu akaamua kufanya uvamizi wake mchana kweupe. Alilipenda giza lakini alijua linavutia wengi sana....

Akauchagua mchana kwenda nyumbani kwa Zubeda.

Akajiapiza kuwa Zubeda akionyesha dalili zozote za kuwa upande usiokuwa wake basi hatasita kumshukia kama mwewe anavyomshukia kifaranga na kumwacha mamaye akipiga kelele asiweze kutoa msaada.

Majira ya saa nane mchana alikuwa analitazama geti la kuingilia nyumbani kwa Zubeda.

Hali ya ukimya ilitawala sana, akategea mpaka alipowaona wanaume wawili wakipita kuelekea njia ile naye akaunga tela ili asionekane kama anajihusisha kwa lolote na nyumba ile.

Akapita na kuangaza huku akiulazimisha ule ukimya umwingie akilini na kumpatia jawabu la ni kitu gani kinaendelea.

Kimya kilimtatanisha!

Si kwamba hapajawahi kuwa kimya ama huwa ni sehemu yenye kelele za kutisha, ila ni mwili uligoma kuupokea ukimya ule katika namna ya kawaida.

Alilipita geti lile kwa mara ya kwanza huku akifanikiwa kujifunza kuhusu mazingira yale upesiupesi, mara ya pili aliporudi alilifikia geti na kubisha hodi.

Mlinzi akajitokeza na kufungua.

Hakusema kitu akabaki kumsikiliza Nguzu mwenye miwani nyeusi.

"Ni mgeni wa Zubeda! Koplo Zubeda.." Nguzu akajitambulisha huku akigundua kuwa huyu mlinzi ni mpya sio yule wa awali.

Akasaili eneo lililomzunguka yule mlinzi na kugundua kuwa hata silaha imebadilika.


Akaduwaa, kunani mpaka Zubeda aamue kuajiri mlinzi ambaye ana utaalamu wa kutumia silaha hii tena mchana kweupe.

"Sub machine gun!" akajikuta anajisemea kichwani kwake, kana kwamba ni mashairi ya wimbo anaotaka kuukariri.

"Wewe ni nani?" Mlinzi akauliza.

Polisi! Machale yakamcheza Nguzu kwa jinsi mtu yule alivyouliza lile swali, hakuwa mlinzi wa kawaida huyu alikuwa polisi.

"Naitwa Sebastian Madeko. Ni jirani..." alijitambulisha.

"Nisubiri hapa!" mlinzi alimwamrisha kisha akapiga hatua kwenda katika mlango wa nyumba ya Zubeda.

Nguzu akamwacha hadi alipoufikia mlango akawa makini kumtazama atazungumza na nani.....

Alishatambua kuwa hali haikuwa shwari, ni aidha Zubeda alikuwa matatani ama la alikuwa analeta matata.

Mlinzi akarejea baada ya dakika mbili.

"Twende!" akamwambia huku akimkazia macho.

Nguzu hakutaka kuionyesha hofu yake badala yake alijiandaa kwa mapambano.

Mlinzi akalifunga geti vyema kabisa kabla ya kumwongoza Nguzu kuelekea katika mlango wa kuingilia nyumba ya Zubeda.

Wakaufikia mlango, Nguzu hakuendelea kuwa kondoo.

Katika mlango ule wa kioo, aliweza kumsoma yule mlinzi, kuna shambulizi alijiandaa kumkumba nalo kabla hawajaingia ndani ama kuishia palepale.

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni