
Mtunzi: George Iron Mosenya
SEHEMU YA KUMI NA TISA
ILIPOISHIA...
ILIPOISHIA...
kuna kipindi alikuwa akitamani hata kumdhuru yule inspekta ambaye ndiye kikwazo pekee kilichokuwa kati yake na penzi la uhuru baina yake na Zubeda.
Nguzu alikuwa akitamani kumtambulisha Zubeda kwa marafiki zake kama shemeji yao, ukiachana na kuufurahisha moyo wake na pia kuuweka wazi udhibiti wake dhidi ya Zubeda,
JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈
ENDELEA...
Sifa pia kilikuwa ni kigezo cha kutamani uhuru ule.
Nani ambaye angeacha kumsifia kuwa anamiliki 'mtoto mkali'
Zubeda alikuwa mzuri, urembo wake haukufichika hata alipojitundika katika gwanda zake za kazini.
Askari wengi walikiri kuwa binti huyu alikuwa wa aina yake, na hii ni sifa waliyoitoa huku akiwa katika gwanda zake.
Nguzu alikuwa amepata fursa ya kuziondoa zile gwanda kisha akamvesha kanga moja nyepesi mwanadada huyu na kisha kuambatana naye maliwatoni.
Macho yake mawili yenye nguvu yakifanikiwa kutazamana ana kwa ana na mzigo wa matiti ambayo yalikuwa yamevuka kidogo ule muda maarufu wa 'saa sita' lakini hayakuwa mbali sana kufananishwa na muda huo hasahasa yakipewa msaada mdogo wa sidiria.
Macho ya Zubeda yangeuamuru mwili wa mwanaume yeyote atakayemtilia maanani kujikuta ukisisimka na donge la hamu kumshika.
Macho yake makali angali akiwa kazini yalikuwa yanatepeta wakiwa wawili na Nguzu na kumfanya Nguzu ashangazwe na hali hii.
"Huyu mtu aliupata vipi ukoplo wa polisi? Kwa macho haya tepevu?" Haya ni baadhi ya maswali aliyojiuliza kabla hajachoshwa na mikono laini ya Zubeda. Mikono ambayo hakuamini hata kama inao uwezo wa kuzishika pingu na kumlazimisha mtuhumiwa azivae.
Ajabu Zubeda alisifika kwa kuwahenyesha watuhumiwa.
Kuhenyesha watuhumiwa??
Ilishangaza!
Lakini Nguzu naye akajikuta anahenya kupambana na msisimko uliokuwa ukimkumba kila mara mikono ile ilipomgusa.
Na hapo akakiri kuwa hata yeye ni mtuhumiwa pia na alikuwa anahenyeshwa wawapo chumbani wawili.
Kweli Zubeda ni kiboko!
Kumbukumbu hizi zikajirejesha nyuma kwa kasi ya ajabu, Nguzu akakumbuka jinsi alivyokutana na Zubeda jijini Mwanza.
Akaukumbuka utambulisho wake wa kijivuni dhidi ya Zubeda ambaye hakuwa na cheo chochote wakati ule na hata jeshini alikuwa hapajui.
"Naitwa Martin, Konstebo Martin Nguzu!"
Tabasamu likamponyoka na kujikuta akipiga saluti ya kihuni.
Akakiendea kitanda na kujirusha hapo kwa fujo zote.
Kitanda kikahimili kishindo!
Na hapo kikaanza kuufyonza ule uchovu wote na kuugeuza kuwa raha ya kipekee.
Usingizi ukampitia.....
_____
MAHAKAMA kuu ya Tanzania ilikuwa imesheheni haswa, maaskari walikuwa wanafanya kazi ya ziada kuwazuia watu waliozidi kumiminika pale mahakamani.
Punde ikasikika amri ya kumaanisha kuwa jaji na baraza zima la wazee lilikuwa linaingia pale mahakamani.
Kimya kikuu kikatanda ikiwa ni ishara ya kuheshimu mahakama.
Akiwa na pingu miguuni na mikononi kisha pingu hizo za miguu na mikono zikaunganishwa na mnyororo mgumu aliongozwa hadi katika kizimba.
Alipofikishwa kizimbani akafunguliwa zile pingu, akaingia akiwa huru kizimba kikafungwa.
Macho yake yaliyozama ndani na kuzidi kuonekana kuwa ni makubwa yaligeuka huku na kule, safari hii hakuwa na uoga tena alikuwa ameikubali hali halisi.
Macho yake yakatua katika kiti alichokuwa ameketi mama yake aliyepooza upande mmoja.
Licha ya kwamba alikuwa amelia sana hadi machozi kumkauka aliweza kuhisi machozi ya moyoni yakimlowanisha.
Wakagonganisha macho yao, akamwona mama yake akizungumza maneno yasiyoweza kusikika hata kidogo huku machozi yakimtoka kwa wingi.
Aliamini kuwa mama yake alikuwa akimwombea kwa Mungu ili kesi ile ipate muujiza wa yeye kushinda.
Uchungu uliomshika alitamani angepewa walau nafasi moja tu ya upendeleo naweze kuzungumza na mama yake, amkumbatie na kumfariji.
Jicho lile likaendelea kubarizi pale ndani ili aweze kuwaona watu wengine ambao huenda anawajua.
"Marafiki hawana maana!" Alijisemea baada ya kuhakikisha kuwa hakuna rafiki yake hata mmoja aliyefika mahakamani hapo.
"Kwa hiyo wameogopa kuwa nitawachoma ama?" alijiuliza.
Hakupata muda wa kujiuliza zaidi wakati jicho lake likitua katika kiti kingine upande wa kushoto.
Macho yakagongana tena na huyu mkaaji wa kiti hicho.
Zubeda!
Walitazamana kwa sekunde kadhaa kabla Martin Nguzu hajakwepesha macho yake.
Hakutaka kumwangalia binti huyu aliyekonda sana na kuonekana wazi alikuwa akitawaliwa na uchungu mkubwa.
Alipomaliza kuzungusha macho yake akamwona jaji akitoa ruhusa ya mwendesha mashtaka kumuuliza maswali mshtakiwa.
Maswali yalikuwa magumu sana, akayajibu kadri alivyoweza. Mengi alikuwa ameyasahau kabisa.
Miaka sita mahabusu bila kesi kusikilizwa, angekumbuka nini sasa.
Wakati wote huu alikuwa akishangaa kumwona wakili kwa ajili ya kumtetea.
"Lakini nilimkataza mama kuhangaika kuweka wakili." Martin Nguzu alijiuliza huku akitikisa kichwa chake kama namna ya kusikitika.
Akakiri kuwa katika ulimwengu huu mzazi ni mzazi lakini mama ni bora zaidi kuliko baba. Mama anaumia sana akimwona mwanaye katika wakati mgumu wakati baba huhesabu ugumu ule kama changamoto na kusema 'kijana wangu amekua na atatatua changamoto hizo' mama huinama chini na kusema 'mtoto wangu anateseka'
Ni hii tofauti aliikiri katika kesi yake hii. Mama mzazi aliyepooza mwili alikuwa mahakamani kushuhudia kile kiumbe alichokileta duniani baada ya suluba ya miezi tisa, kisha kuhangaika katika malezi.
Hakujali kupooza kwake, hakujali kuwa yawezekana mwanaye akahukumiwa kifungo cha maisha gerezani ama kunyongwa kabisa kwa jinsi kesi ilivyokuwa.
Alichokifuata pale ni kumwona mwanaye kwa jicho lake mwenyewe. Kama alivyomuona wakati amemzaa, alihitaji kumwona tena katika ugumu huu, ugumu wa kukondeana kwa sababu ya mateso na lishe duni, ugumu wa kuwaza kufia jela.
Mama alibaki kuwa shuhuda wa mwisho!
Ni nani kama mama kwani?
Wakili alisimama na kutema vifungu vya sheria ili kumnusuru Martin Nguzu kutoka katika janga lile.
Alionekana kuijua vyema sheria lakini upande wa mashtaka ulionekana kuwa imara zaidi, sura nyingi zilitawaliwa na hasira kali. Hasira hii iliboreshwa zaidi na mavazi yao, walifanania na kundi la mafia ambalo limemshukia mwenzao baada ya kuwasaliti na sasa wanataka kumpa adhabu ya kumzika huku akiwa hai akaupiganie uhai wake akiwa chini ya ardhi.
Nguzu akamgeukia jaji ambaye alionekana mwingi wa chuki kuliko haki.
Jaji alipounyanyua uso wake Nguzu akajikuta anagundua kitu kipya kabisa. Ile sura ya jaji haikuwa njgeni machoni mwake hata kidogo.
Hofu ikamjaa ya kutotendewa haki juu ya kesi ile ambayo alitambua wazi kuwa ni vile tu amekosa mashahidi lakini haikuwa ikimuhusu kabisa na alitakiwa kuwa mtu huru.
Jaji yule akaanza kusoma vipengele kimoja baada ya kingine kwa utulivu sana.
Ni kama aliyeelekea kutoa hukumu, hii ilimshangaza sana Martin.
Hukumu inatoka vipi kirejereja hivi bila kesi ile kupewa muda wa baraza la wazee kuipitia na kutoa mitazamo yao.
Jaji alisoma taratibu huku kila mahali akijaribu kumbana Nguzu.
Na hatimaye kauli ikamtoka.
"UTANYONGWA MPAKA UFE"
Mungu wangu! Nguzu akamwona mama yake mzazi akitua chini kama mzigo, watu wakakimbilia alipokuwa ili kumwokoa.
Palepale akawaona askari wanne wenye ghadhabu wakisogea katika kile kizimba na pingu kwa ajiri ya kumchukua na kumpeleka katika mahabusu ya mahakama kabla hawajampeleka gereza la Ukonga.
Gereza pekee ambalo washtakiwa waliohukumiwa kunyongwa mpaka wafe huhifadhiwa huko mpaka siku ya hukumu yao.
Kuwaona watu wale kukamchanganya Nguzu, na jaji alikuwa amefunga mjadala tayari.
Nguzu akaona haiwezekani, akawahi kujirusha akaidaka silaha ya askari mmoja na mara moja akaielekeza alipokuwa yule jaji.
Jaji akakodoa macho yake alipojikuta anatazama ana kwa ana na bunduki iliyoshikwa na mtu asiyekuwa na masihara hata chembe.
Akafyatua risasi kiufundi lakini yule jaji akawahi kujificha chini ya meza.
Na hapohapo Nguzu akaisikia sauti ya kike ikimpigia kelele kumtahadhalisha.
Ilikuwa sauti ya Zubeda!
Akageuka na kukuta amechelewa tayari, bunduki nyingine ilikuwa inaelekea kufyatuliwa ili yeye adhurike.
Ilielekezwa kifuani pake.
Akajikuta anapiga mayowe ya hofu huku akikiziba kifua chake kwa mikono yake.
Bunduki ikacheua.
"Mamaaaa nakufaaa!" alipiga kelele kubwa sana na hapo akajikuta akibiringita kama chaguo lake la mwisho.
Akashangaa kujikuta anaelea hewani. Akaanza kutapatapa akirusha miguu huku na kule.
Hatimaye akasimama wima tena.
Hakuwa mahakamani! alikuwa amesimama katika kitanda huku akiwa amejifumbata mikono yake katika kifua chake.
Ndoto!
Jasho lilikuwa linamwagika vibaya mno, bado moyo ulikuwa unapiga kama unaotaka kutoka nje ya kifua chake.
Alikuja kutulia baada ya dakika kumi na hapo ndipo akakiri kuwa ile ilikuwa ni ndoto lakini ndoto ya ajabu sana.
"Yule jaji yule! Yule jaji ni nani!? Jaji, jaji...." Nguzu alibaki kusema kama ambaye anajaribu kulazimisha kung'amua vitu kutoka katika ile ndoto ya ajabu ambayo hakutaka kuamini eti ilikuwa ndoto ya kawaida.
Alihisi yule ni babu yake anasema naye. Hofu ikatanda alipokumbuka kuwa alihukumiwa kunyongwa katika ndoto yake.
Hofu ya kifo ikamjaa, akaanza kuhofia uwepo wake katika jiji la Dar es salaam.
Jiji ambalo ipo ile mahakama ya ndotoni na pia lile gereza wanalohifadhiwa wafungwa wa adhabu ya kunyongwa mpaka kufa.
Hiki nini? alijiuliza.
Bado hofu iliishi naye, akamkumbuka mama yake alivyokuwa akimlilia na hata alivyoanguka baada ya hukumu ile kutolewa.
Hofu ya kifo ikiwa haijaisha ikapanda hofu nyingine.
Hofu ya kumpoteza mama yake mzazi pindi atakaposhuhudia matatizo yakimpata.
Nguzu akakiri kuwa huu mpambano ulikuwa maji ya shingo kwake naye alikuwa hajui kuogelea vyema. Akaamini kuwa alikuwa anahitaji watu watakaosimama pamoja naye.
Kwa mara nyingine tena jina Zubeda likakiandama kichwa chake.
"Kwanini Zubeda?" alijikuta katika swali hili.
Hisia mbili zikaanza kupambana, mojawapo ilikuwa hisia za mapenzi. Nguzu akakiri kuwa alikuwa akihangaishwa na jina Zubeda kwa sababu tu aliwahi kumpa burudani ambayo ilikatishwa ghafla bila kufika ukingoni.
Pili alihisi kuwa anahitaji kupata msaidizi na msaidizi wa kweli katika vita hii ni koplo Zubeda.
Kujua hisia ipi ni ya kweli nd'o ukawa mtihani mzito.
"Ngoswe penzi kitovu cha uzembe" Usingizi ulimkuta Nguzu akiwa katika uchambuzi hafifu wa kitabu hiki maarufu, alianza kwa kumpa kongole mwandishi Edwin Semzaba kwa kuandika kitabu hiki, kisha akahamia kwa Ngoswe na Mazoea na hadi anasinzia alikuwa amefikia mahali ambapo Mazoea ameanza kuzoeana na Ngoswe!
USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA
Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi