KONSTEBO NGUZU (25)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA ISHIRINI NA TANO
ILIPOISHIA...
Juma Kihwele akajihesabia kuwa amekutana hatimaye na mtu ambaye atamuelewa na kumwokoa.

Hakujua kuwa amekutana na anayewatuma wale aliowaona kama mashetani yanayoishi.

"Haujambo?"

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
Jeremiah aliuliza kifedhuli.

"Sija... shkamoo... sijambo.." alijiumauma katika kujibu.

"Martin Nguzu alikufa ama hakufa? na kama hakufa nataka kujua ni nani aliyehusika katika kumwokoa..." Sauti kavu ya Jeremia ilihoji.

"Sijui lolote muheshimi..." kabla hajamaliza kumjaza cheo alipokea kofi kali katika shingo yake.

Yowe la hofu likamponyoka.

"Nahitaji jibu tofauti na sijui."

"Muheshimiwa mi naapa haki ya..." Hata hii kauli pia haikumalizika kabla hajapokea kofi jingine, hili la sasa liliuchana mdomo wake.

"Umeona biblia ama msaafu humu ndani? Sihitaji viapo nahitaji majibu..."

Juma Kimbelembele sasa alikuwa amepatikana.

Alijaribu kutuliza akili yake na kuchagua jibu la kutoa lakini alihofia kuwa linaweza lisiwe na ushawishi.. Lakini ni heri kuzungumza kuliko kuwa kimya dhidi ya mtu yule aliyekuwa mbele yake.

"Nyumba iliungua mkuu, sikumuona akitoka hai. Alikufa na wanahabari waliandika..."

"Wanahabari ni akina nani hadi unawataja kama utetezi wa hayo unayosema?"

"

Kimya! hakuwa na la kujibu.

"Una uhakika alikufa?"

"Nyumba iliteketea..." alijibu kinyonge lakini unyonge wake haukumzuia Jeremia kumbutua tena, safari hii kwa kutumia mguu wake.

Juma akajikaza hakupiga kelele kubwa licha ya kuumia.

Jeremia Kazeze akatoa picha kadhaa akamtupia Juma Kihwele akawa anatazama nazo.

"Unafahamu hicho ni nini?"

"Ndio mkuu, nyumba ya hayati Nguzu baada ya kuteketea"

"Ooh! Kila mtu anajua nyumba iliteketea, sijafunga safari kutoka huko mbali kuja kupata uthibitisho kuwa nyumba iliungua..... najua kusoma na ninaona pia... nahitaji kujua wewe na Nguzu ni washirika katika ngazi ipi?"

"Wallah! naapa sina ushirika wowote na marehemu..."

"Unavyosema marehemu kama vile uliuzika mwili wake... sikiliza wewe mtoto. Kama unayaficha unayojua kuhusu Nguzu, hautajificha kuizika miili ya wapendwa wako. Kwa mkeo nitajitahidi ubaki uso pekee ili usije kugoma kuuzika mwili ukisema sio mkeo, ila hutapata hamu ya kukiuona kiwiliwili chake, na ukijitia shujaa kukiona utakuwa unakiota ndotoni kila siku na itakuwa ndoto ya kutisha..."

Akaweka kituo na kutoka nje.

Juma alipojaribu kuzungumza akaishia kujikaza asijikojolee zaidi wakati tayari keshajimwagia kojo muda mrefu tu.

______

JEREMIA KAZEZE mwenye akili kiwango cha babu yake aliona njia pekee ni kuwahi kwa IGP kwa ajili ya kujisafisha na kuyaweka sawa mazingira ikiwa tu jambo lolote litaharibika zaidi.

Aliziona dalili za kuangushwa kama alivyoangushwa babu yake zikimnyemelea....

Ilikuwa yapata majira ya saa mbili usiku.

Haukuwa utaratibu wa Kazeze kumtembelea mara kwa mara IGP, ni yeye aliyependa kutembelewa kwa sababu ya kumzidi kiumri na urithi wa tabia ya kupenda sifa za kijinga alioupata kwa babu yake.

Siku hii ilikuwa tofauti zaidi, tena saa mbili usiku.

Mbaya zaidi hakupiga simu kutoa taarifa.

Alipokelewa bila mashaka, taarifa za walinzi zikapitishwa ndani na ruhusa ikatolewa.

Kazeze akaingia kuonana na IGP.

Tofauti na nyakati nyingine walizowahi kuonana, hii ilikuwa tofauti sana. Kila mmoja alikuwa katika ulimwengu wake.

Licha ya kujilazimisha kuonenekana kuwa wapo sawa ila nafsini hali ilikuwa wazi.

Mgeni alianza kuelezea juu ya ujio wake usiku ule, akaanza kuulizia hatma ya Inspekta Kobo na sakata la kujihusisha na majambazi sugu mkoani Shinyanga.

IGP akamweleza juu juu kuwa hadi wakati huo Kobo alikuwa amekataa kukiri kuwa aliikosa shabaha ile maksudi na anaapa kuwa hajihusishi na kundi lile.

"Nawe umeamini?" Aliuliza kwa mshangao..

IGP akaduwazwa na swali lile, japokuwa haikuwa mara ya kwanza kukerwa na maswali ya yule aliyemtangulia.

Kwanini ananichimba huyu?! Alijiuliza kisha akatabasamu na kujibu, "vijana wangu wanaendelea kumuhoji. Watanipatia majibu ninawaamini sana..."

"Na unafahamu lolote kuhusu mauaji ya askari wetu mtiifu, konstebo Nguzu aliyechomewa ndani ya nyumba?"

"Naam! na nilifika eneo la tukio, vipi kuna jipya?"

"Inspekta Kobo anahusika kumteketeza, inasemekana Nguzu anajua kuhusu Inspekta Kobo kujihusisha na kundi lile, na alikuwa anakaribia kuvujisha siri.."

"Unasema Nguzu anajua kama yupo hai mkuu...."

"Aam! Nguzu alikuwa anajua..." Akarekebisha huku akijaribu kujichekesha.

"Upo ushahidi wowote wa kumweka hatiani Kobo?"

"Kuna mwandishi wa habari alishuhudia kila kitu, kuanzia muda wa kuwasili hadi muda wa tukio?"

"Aisee! aliarifiwa na nani hadi kuweza kuzijua nyendo za askari makini kama Kobo!" Alijibu IGP.

Kitendo cga Kobo kuitwa askari makini kikamkwaza Jeremia Kazeze.

"Unamuita makini na kwa maksudi kabisa ameacha kumsambaratisha jambazi sugu, jana watu nane wameuwawa huko Shinyanga, wawili kati ya hao ni askari wetu na pasi na shaka muhusika ni huyohuyo aliyeachwa apumue na Kobo. Leo hii unaendelea kumvesha nishani ya umakini? Are you damn serious brother?" Alilalama.

"Nimvishe jina gani ambalo litakuridhisha na kuyanyoosha mazungumzo yetu?" IGP akahoji, Jeremia akatambua kuwa kile ni kijembe.

hakujibu.

"Anyway, nina taarifa njema sana zinaweza kusaidia katika kuboresha hizo tuhuma" IGP akazungumza kisha akaiacha kauli ile hewani ili imuingie vyema bwana Jeremia.

Jeremia akahoji kwa kimuhemuhe.

"Ni taarifa gani mkuu..."

"Nimepigiwa simu na mtu anayedai kuwa yeye ni konstebo Martin Nguzu. Na tayari nimeagiza vijana wangu wafuatilie alipo na kumtia nguvuni, bila shaka atatusaidia sana katika kukamilisha upelelezi... tukimuunganisha na huyo mwanahabari wako, sioni Kobo anachomokea wapi...." Alimalizia huku akiwa anamtazama kwa macho ya kuibia Askari mwenzake.

Moyo wa Jeremia ulipiga kwa nguvu sana, hakuamini kile alichokuwa anakisikia, alijiona kile kikombe anachomwandalia Kobo kikigeukia upande wake ndani yake kikiwa na uji wa mto ambao anapaswa kuunywa bila kupooza.

Mbaya zaidi kile kikombe kilikuwa cha bati.

Akatamani kutoa kauli yoyote lakini kauli yenyewe ikagoma kuunganika.

Koo lilikuwa limekauka.

"Nisaidie maji ya kunywa!" Jeremia akamwomba IGP.

IGP akatabasamu kisha akaitazama meza, Jeremia alikua ana kikombe cha maji mbele yake.

Ajabu alikuwa hakioni!

"Kwani Nguzu yupo hai au?" Akatokwa na swali la kizembe.

"Kitu pekee ninachofahamu ni kwamba nyumba yake iliteketezwa, kuhusu uhai nitakuongopea,Vipi kwani?" IGP akazidi kuzungumza kwa utulivu kabisa na hapohapo akiifurahia hali ya kupagawa ya Jeremia Kazeze.

"Kwani Nguzu yupo hai au?" Akatokwa na swali la kizembe.

"Kitu pekee ninachofahamu ni kwamba nyumba yake iliteketezwa, kuhusu uhai nitakuongopea,Vipi kwani?" IGP akazidi kuzungumza kwa utulivu kabisa na hapohapo akiifurahia hali ya kupagawa ya Jeremia Kazeze.

Na hapo IGP akashuhudia tembe za jasho zikiumuka katika mgongo wa pua ya Jeremia.

Uoga!

Anaogopa nini sasa? Ina maana jamaa ana 'kamisheni' katika kutekeleza mauaji ya Nguzu?

Kwanini mtu aliyewahi kuwa na cheo cha juu kama huyu ahusike katika mpango mdogo kama ule.

Haya yalipita katika kichwa cha IGP kwa kasi kubwa.

Kwa upande wa IGP mstaafu Jeremia Kazeze alikuwa anajaribu kuutuliza muhimili wake wa kufikiri, alijiona yu katika kupagawa tayari na alihisi IGP ameanza kumgundua kuwa anapagawa.

Akajivika ukakamavu huku akijizuia asitazamane ana kwa ana na IGP kwani aliogopa kupepesda macho yake.

"Nadhani sasa mimi niende" Jeremia alizungtumza kwa kuridhika.

"Mkuu, kwa hiyo huyu Nguzu tunamfanyaje ikiwa kweli anapatikana angali hai wakati sote tunajua amepoteza maisha?" IGP akamtundika swali lililojaa maswali ndani yake.

"Nani? Nguzu...aah!" Jeremia akatetereka. Kichwani mwake akajiona yu katika kumi na nane za IGP na sasa alikuwa anajaribu kucheza naye atakavyo na ikiwa ataghafirika na kumkwatua basi uamuzi ulikuwa ni 'penati.

"Akikamatwa inabidi hapo sheria tu ichukue mkondo wake... no way out! Lazima Nguzu aadabishwe. Period!" Jeremia akajikaza kishupavu akajibu kama mtu aliyeshtuliwa toka usingizini akaulizwa moja jumlisha moja akajibu nne kwa sauti ya juu, akiamini yu sahihi

IGP akaponyokwa na tabasamu jepesi kabla hajamdhihirishia Jeremia kuwa mojawapo kati ya watu wanaoitwa mabwege basi yeye kama si kiongozi wao basi ni msaidizi.

"Sheria ya kumshtaki kwa kuchomewa nyumba ama tutamuadabisha katika 'engo' ipi afande" IGP akatupa bomu jingine dogo lenye mlipuko mkali.

Jeremia akajiona jinsi anavyodhihirisha kuwa yungali fala katika ubora wake. Na kupitia maswali yale ni namna ya kuitwa fala bila tusi hilo kutajwa.

Ilimuuma!

Hakutaka kuendelea kulithibitisha hilo mbele ya bwana yule ambaye alikuwa mdogo kwake kimri.

"Kwa hiyo unataka akikamatwa aachwe tu bila hata kusaidia upelelezi?" Akauliza kwa ghadhabu.

"Hapana mkuu, yule kukamatwa muhimu tena muhimu sana...." IGP akajibu kichangamfu kisha akamalizia, "Ishu hapa ni tunamshtaki kwa lipi? Kudanganya uma kuwa amekufa kumbe hajafa? kujichomea ndani ya nyumba au tunamshtaki kwa kuwa hai?"

Jeremia akagundua anachezewa ngoma iitwayo shere.

Ngoma wanayochezewa wajinga bila kujua wanadhihakiwa.

Akaaga na kuondoka kwa mara nyingine.

______

SAFARI ya kulifikia gari lake ilikuwa ndefu sana, Jeremiah alijiona katika akili yake anatembea kama kitoto kinachojifunza kutembea, kikijiona kinao uwezo wa kumkimbia mama yake, angali mama anapunguza mwendo maksudi ili kichukue ushindi kitoto kile.

Miguu yake ilikuwa kama inayopambana kutangulia kupiga hatua, wa kulia unataka utangulie na wa kushoto unahitaji nafasi hiyo.

Ikafikia hatua akili yake ikawqa haiwazi kitu kingine zaidi ya kuwaza namna ya kuiamuru miguu yake ipeane heshima stahiki japo kwa dakika hizo chache tu za kulifikia gari lake.

Miguu ikatii!

Akalifikia gari.

Walinzi wakamkabidhi silaha yake ambayo waliichukua kabla hajaingia ndani kwenda kuonana na IGP, akaziona saluti alizopigiwa zikiwa ni kama ishara inayochukiwa na vijana wengi wafanyiwapo.

Macho yake hayakuona saluti ya heshima bali aliwaona vijana kadhaa wakiwa wanamzomea na kumwonyeshea ishara ya kidole cha katikatika katika mpangilio wa vidole kiganjani.

Hasira zikazidi kumchemka, akapanda garini.

Akatoweka huku akikiri kuwqa katika maisha yake yote, hii ilikuwa mara yake ya kwanza kujikuta amewekwa mtu kati na siweze kujing'atua.

Aliendesha kwa mwendo wa wastani,

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni