BABA KIUMBE WA AJABU (1)

Zephiline F Ezekiel
Mtunzi: Ally Mbetu

SEHEMU YA KWANZA
Katika dunia ya Mungu kuna mambo mengi ambayo ukihadithiwa unaweza kudhani ni simulizi za kutunga na za kusisimua. Lakini siku zote kila aisifiaye mvua basi ujue imemnyea. Dunia imezungukwa na siri nzito ndani ya majumba ya watu, kuna mambo mazito ambayo ni chukizo kwa Muumba.

Si kila mwenye maisha mazuri au tajiri mali alizonazo kazipata kihalali. Wengi utajiri wao unatokana na nguvu za giza, utajiri anaoambatana na kutoa kafara ya kitu. Wapo wanaotoa kafara watoto, wake au waume zao, pia wapo wanaowageuza watoto, wake au waume zao kuwa mandondocha kama ‘chuma ulete’ wa kuwaongezea kipato.

Nyumba nyingi huwa na vyumba vya siri ambavyo huwa havifunguliwi kutokana na masharti ya mganga na kufanya watu wabaki na maswali. Pia nyumba nyingine unakuta kuna mtoto ambaye akili zake si nzuri, akikaa yupoyupo tu, mate yanamtoka ovyo kumbe ni dawa ya utajiri. Ajabu huyo ndiye anakuwa kipenzi cha baba ambaye anajua siri yake.

Wapo ambao huambiwa kama mtoto huyo atakufa basi na utajiri nao utayeyuka, ni mambo mengi yaliyoizunguka jamii na uchafu wa tamaa za watu kutaka utajiri kwa njia ya mkato na kujikuta wakifanya uchafu au ukatili mkubwa bila kuwa na huruma ilimradi wapate utajiri. 

Nayasema haya nikiwa na uchungu mkubwa baada ya baba yangu kutugeuza chuma ulete sisi wanaye kwa ajili ya kumuingizia pesa bila kujua. Nayasema haya baada ya kuteseka zaidi ya miaka saba bila kujua kumbe mateso yangu ndiyo yalikuwa chachu ya utajiri wa familia yangu. 

Tangu nilipoanza kupata matatizo yaliyosababisha mateso kila kukicha, hata siku moja sikuruhusiwa kwenda hospitali zaidi ya kutumia dawa za kienyeji zilizokuwa zinapunguza maumivu na si kuniponesha.

Miaka saba nyuma, tatizo kama langu alikuwa nalo dada yangu ambaye nilimfuata mara ya nne ambaye sasa hivi ni marehemu. Mwanzo nilipomuona dada nilijua ni kidonda cha kawaida  japo kilinishangaza kuchukua muda mrefu tangu nikiwa na miaka sita mpaka nilipokuwa na utambuzi kujua kuwa dada yangu anateseka na kidonda kile ambacho kilikuwa hakiponi.

Miaka mitatu baadaye nilisikia ugomvi mkubwa kati ya baba na dada, nilijificha na kumsikia dada akisema:

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

SASA TUENDELEE...
“Nimechoka! Siwezi kuteseka wakati wenzangu wanafaidi kwa mateso yangu, siolewi sina maisha mazuri kama wenzangu niponipo tu. Haya maisha mpaka lini? Nasema sasa hivi naondoka na hili sasa mtafutie mwingine, nakwenda kuishi maisha yangu, kama pesa nimekuingizia sana naomba niondoke.”

Monika mwanangu, kuondoka kwako kutaharibu kila kitu.”

“Baba acha viharibike, nimechoka.”

“Mwanangu unajua kabisa dawa hii haitaki uchafu, ukikutana na mwanaume tu umeharibu kila kitu.”

“Ndiyo maana nimekwambia tafuta wengine, baba wewe ni kiumbe gani usiye na huruma. Miaka yote nateseka peke yangu wakati wengine wanafaidi, watu wana majumba wana magari ya kifahari lakini mimi bado naishi maisha duni, kuna faida gani kuendelea kuteseka.”

“Basi nipe muda nivifanyie kazi.”

”Sina muda huo nimechoka.”

Kwa kweli kutokana na uchanga wangu wa akili, sikujua baba na dada walikuwa wanabishana nini, pia nilijiuliza dada ana mateso gani ambayo anamlalamikia baba. Lakini baada na mimi kunikuta nilielewa dada alikuwa akimaanisha nini. Maisha tuliyokuwa tukiishi yalikuwa ya ajabu sana, kwa sisi tuliokuwa tukiishi nyumbani tuliishi maisha ya dhiki sana tofauti na utajiri mkubwa tuliokuwa nao.

Tulikuwa na majumba kila kona ya Jiji la Mwanza, pia tulikuwa na mashine za kusaga na kukoboa ambazo ziliingiza pesa nyingi sana. Kaka zangu na dada zangu wote kila mmoja alikuwa na duka kubwa, gari na majumba makubwa. Lakini sisi tuliobakia maisha yetu hayakulingana na utajiri wa baba yetu.

Kitu kingine wakati ule kilichonishangaza ni hali ya mama, pamoja na kuwa na utajiri mkubwa kama ule, kila siku mama alikuwa akiamka asubuhi na kwenda shamba ambako alilima mpaka jioni na kurudi nyumbani. Kila mama aliporudi nyumbani alikuwa akirudi na kuni ambazo alipikia katika jiko la mafiga. 

Kwa vile mwanzo zilikuwa akili za kitoto sikuelewa nini kinaendelea wala wakati huo sikujua faida ya utajiri tuliokuwa nao. Kitu kingine ambacho sikukielewa muda ule kilikuwa ni nyumba tuliyokuwa tukiishi. Ilikuwa ni ya zamani ambayo baba aliinunua wakati anaanza maisha. 

Lakini haikuwa na mabadiliko yoyote pamoja na mabadiliko ya kimaisha kwa baba kuwa na pesa kama mchanga. Dada baada ya kubishana na baba alikaa kwa wiki mbili.

 Siku moja niliporudi sikumkuta, alikuwa ameamua kuondoka, sikujua amehamia wapi. Lakini baada ya siku tatu nilipata taarifa kuwa dada amehamia Mkuyuni ambako alikuwa amepanga na kufungua duka lake. Kuondoka kwa dada kulifanya nyumba igeuke kama pametokea msiba, kitu ambacho kilinishangaza sana.

Kuondoka kwa dada hakukuwa kitu cha ajabu kwa vile dada na kaka zangu wote walipotaka kuanza maisha yao waliondoka lakini hakukuwa na mabadiliko yoyote. Baba alionekana kukosa raha, mama naye muda mwingi mkono ulikuwa shavuni. Kitu kile kwa kweli kilinishangaza sana.

                                                          ****

Nakumbuka siku moja ndugu wote walikutana nyumbani kasoro dada Monika na kuwa na kikao kizito, cha ajabu mimi nilitolewa nje hivyo kilichoendelea sikujua kwa vile nilibaguliwa kutokana na kuonekana mdogo nisiye na mchango wowote. 

Baada ya kikao kilichochukua zaidi ya saa nne, ndugu zangu waliondoka.

Kuondoka kwao kidogo kulifanya baba achangamke bila kujua walikuwa wamezungumza nini na nini chanzo cha wazazi wangu kuwa katika hali ya majonzi.

 Nilijiuliza ilikuwa ni dada kuondoka au kulikuwa na jambo kubwa zaidi, katika akili yangu nilifikiria kuna umuhimu wa kumtafuta dada Monika ili nijue kwa nini ameondoka nyumbani na vilevile ni mateso gani aliyoyapata. Kuna kitu kimoja ambacho kilikuwa kikinishangaza tangu nilipopata akili. Kilikuwa ni donda la mguu la dada ambalo lilikuwepo kila siku na wala halikupata dawa ya kuliponesha.

Nilijikuta nikipata hamu ya kutaka kujua kwa nini dada aliyasema yale maneno ambayo yalionesha machungu kwa kuonekana akizuiwa nyumbani asiondoke lakini wengine wote waliruhusiwa. Kingine kilichoacha maswali kichwani mwangu ambacho kilikuwa hakijakomaa akilini ni hali ya dada kuonekana kama hajaliwi na baba tofauti na ndugu zangu tokea kwenye elimu mpaka maisha ya kawaida.

Wote walikuwa na maisha mazuri kasoro yeye, lakini sikutaka kujua zaidi kwa vile nilikuwa mtoto mdogo nisiye na uwezo wa kuhoji jambo. Nilipeleleza anapokaa dada, mama alinieleza anakaa pembeni ya Soko la Mkuyuni, duka lake linatazamana na soko. Siku moja baada ya kutoka shule nilipitia moja kwa moja hadi kwa dada.

Kufika kwake sikupotea, nilifika bila tatizo kutokana na duka lake kuonekana, pia ndilo lililokuwa  kubwa. Nilipofika dukani, dada aliponiona alifurahi sana.

“Karibu mdogo wangu.”

“Asante.”

“Umekuja na nani?”

“Peke yangu.”

“Umepajuaje hapa?” Dada alinishangaa.

“Amenielekeza mama, sehemu yenyewe si ya kupotea.”

“Ni sehemu nyeupe, karibu mdogo wangu.”

“Asante”

“Nyumbani hawajambo?”

“Hawajambo, mama anakusalimia.”

“Baba anajua umekuja huku?”

“Walaaa”

“Karibu soda upoze koo,” alisema dada huku akinifungulia soda.

Nilipokea soda na kuanza kunywa, wakati huo dada alikuwa akihudumia wateja waliokuwa wakinunua bidhaa dukani kwake, baada ya kumaliza kuwauzia alinigeukia.

“Mmh! Habari za shule?”

“Nzuri tu dada.”

“Umetumwa au?”

“Dada siji kwako mpaka nitumwe?”

“Siwajahi kukuona ndiyo maana nashangaa, ni muda gani toka niondoke nyumbani. Najua wote mlinichukia kwa kujua nataka kuwanyang’anya utajiri wenu.”

“Dada mimi sijui chochote zaidi ya baba kukukatalia na kuondoka kwa nguvu, zaidi ya hapo sijui lolote. Na mimi nikukasirikie kwa sababu gani wakati kuondoka kwako kumekuwa mateso na simanzi kwangu kama kuna uwezekano nije nikae kwako.”

“Najua mdogo wangu unanipenda, lakini baba yako hatakubali, ataona nataka kuuhamisha ukoo mzima.”

“Kwani dada kuna nini, mbona mazungumzo yako yamejaa uchungu?”

“Si wenzako wamekuja hapa bila aibu wala huruma na kuzungumza maneno ya kipuuzi,” dada alisema kwa sauti yenye kuonesha huzuni kidogo.

“Tena kweli dada kuna siku kulikuwa na kikao wote walikuwepo kasoro wewe, kwa nini hukuja?”

“Kikao hicho kilikuwa cha kunijadili mimi.”

“Wewe! Umefanya nini?”

“Unajua mdogo wangu wewe bado unakua, lakini kuna mambo ambayo sitaki yakutokee kama yaliyonitokea mimi.”

“Mambo gani?”

“Sasa hivi Masalu unazidi kukua na kupata ufahamu, kidato cha tatu ni upevuko wa akili.”

“Ni kweli dada.”

“Unajua kwa nini nimehama nyumbani?”

“Mmh, sijui.”

“Masalu sasa hivi una akili unajua zuri na baya.”

“Ni kweli dada.”

“Hivi maisha yangu ni sawa na ndugu wengine?”

“Kivipi?”

“Nina nyumba?”

“Hapana”

“Nina gari?”

“Hapana”

“Nina mtoto?”

“Unajua ni kwa nini?”

“Sijui.”

 “Hivi maisha tunayoishi ni sawasawa na utajiri wetu?”

“Hapana

“Hujiulizi kwa nini wengine wanafurahia maisha, wanakula chakula kizuri wanalala pazuri wanatembelea magari ya kifahari wewe na mimi tunateseka wakati baba na mama yetu ni mmoja.”

”Huwa najiuliza, nikienda kwa kina kaka au dada nakula chakula kizuri hata kulala sehemu nzuri tofauti na kwetu.”

“Hivi uwezo wa baba bado mama anaweza kulima tena kwa mkono na kuokota kuni kuja kupikia?”

“Dada hata mimi nachanganyikiwa.”

“Na wewe bila mimi kukuongeza pesa ungenunua hata chungwa ukienda shule?”

“Yaani dada toka uondoke napewa nauli ya daladala tu, tena pesa ya mwanafunzi shilingi mia.”

“Unaona sasa, hebu subiri,” dada alisema huku akimsogelea mteja kumuuzia kitu.

“Na donda lililokuwa mguuni kwangu uliliona kwa muda gani?”

“Mmh, muda mrefu sana.”

“Unaliona tena?” Dada alinionesha sehemu iliyokuwa na donda ambayo ilikuwa imepona na kuweka alama nyeusi.

“Ha! Dada umepona?”

“Nimepona mdogo wangu, lakini utajiri umeingia ufa”

“Ufa! Una maana gani?”

“Donda langu ndilo chanzo cha utajiri.”

“Unasema!” Kauli ya dada ilinishtua.

“Masalu utajiri wetu una siri nzito.”

“Siri! Siri gani hiyo?”

“Masalu utajiri wetu una siri nzito ambayo mimi ndiye niliyeibeba na sasa hivi nimeitua.”

“Una maana gani kusema hivyo?”

“Masalu kuna mambo huwezi kuyajua kutokana na umri wako,

USIKOSE SEHEMU IJAYO

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni