KONSTEBO NGUZU (26)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA ISHIRINI NA SITA
ILIPOISHIA...
Akatoweka huku akikiri kuwqa katika maisha yake yote, hii ilikuwa mara yake ya kwanza kujikuta amewekwa mtu kati na siweze kujing'atua.

Aliendesha kwa mwendo wa wastani,

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
hakuelekea nyumbani kwake na hakujali kuhusu hilo na hakufikiria walau kumpa taarifa mkewe.

Alizoea kumwendesha kama alivyokuwa na tabia ya kuendesha askari waliokuwa chini yake wakati wa cheo chake.

Kitu kama mwiba mdogo kikaichoma akili yake wakati akiendelea kuendesha gari, akawakumbuka haohao askari wenye vyeo vya chini walivyo na hatari wakipewa amri.

Akajiona jinsi watakavyomfunga pingu huku mara kwa mara wakimfokea badala ya kumwelekeza nini cha kufanya.

Wakati huo akiitwa mtuhumiwa.

Na baadaye akaziona kero za kulishwa chakula kibovu, kuhesabiwa kwa kupigwa bila sababu pamoja na kulala sehemu moja na chawa kunguni na kadhalika pindi atakapokuwa mahabusu rasmi.

Mapigo yake ya moyo yakapiga kwa nguvu zaidi, hakutaka haya yamtokee.

Lakini katika yote haya hakusita kutabasamu na kisha kutoa sauti ya chini.

"Ukoo wa Nguzu ni kiboko!"

Pongezi hizi zikamkera na kujikuta akipiga honi bila sababu zozote za msingi.

Safari yake ikaishia nyumbani kwa Veto!

Kiongozi wa kikundi cha vijana waliokuwa wakimtii, wakati na baada ya utawala wake.

Muunganiko huu ni pamoja na wale waliopewa vyema hovyohovyo bila kuwa na sifa, ama ambao watoto wao waliingizwa jeshini kwa kauli moja tu ya aliyekuwa IGP.


Wangemlipa nini zaidi ya kuwa vibaraka, wenzetu waliwaita 'puppets'.

Hakumpigia simu Veto hapo kabla, tabia ya ujivuni ilimtawala na kujiona kuwa anaweza kwenda kwa IGP bila kupiga simu, ya nini kumpigia simu Veto ambaye nd'o kwanza anapambana aweze kuupata u'inspekta?

Hakupiga!

Alifika bila kujali kuwa ule ni usiku sana, akagonga hodi mara kadhaa, hatimaye akaufungua mlango mkewe ambaye bila shaka alikuwa amelala sebuleni kwa kupitiwa na usingizi ama akimngoja mwenzi wake.

"Shkamoo shem!" Mwanadada yule alitoa salamu.

"Vipi yupo huyu?" Jeremia akaipuuza ile salamu akahoji yaliyomleta.

"Hajarudi hadi muda huu lakini niliwasiliana naye akanieleza kuwa iwe isiwe atakuja nyumbani shem" alijibu kwa nidhamu, bila shaka alikuwa akijua nguvu ya mtu aliyekuwa mbele yake.

"Alisema atakuja saa ngapi na wakati anakupigia alikuwa ameanza kuja ama?"

"Hakusema lolote shemeji... ila alini..."

"Sawa.. nitampigia simu." Akamkatisha.

"Labda ujaribu wewe, maana nimejaribu sana hapatikani, hadi nimeanza kupata mawazo. vipi kwani mbona sielewi."

"Ambacho huelewi ni kipi na ni wewe umeongea naye kwenye simu?" Akang'aka.

Mke wa Veto akawa mpole!

Wakabaki kutazamana kama kuku, kuku mmoja akiwa amechoka mwingine akiwa muoga sana.

Ukimya uliotanda kati yao ukasababisha chochote chenye kutoa sauti kiweze kusikika.

Jeremia akasikia mchakacho ndani ya nyumba.

"Upo na nani ndani?" Alihoji kama anayesuta

"Niko.. mwe.. aah! nipo na binamu yangu.."

"Binamu yako yupi?" Akahoji tena sasa akiwa amemkazia macho makali.

tayari alihisi kudanganywa.

Na hapo ikasikika sauti ya kike yenye kila dalili za kuongea kwa shida ya kukabiliwa na usingizi mkali sana.

"Nani kwani... eeh!"

Kabla sauti ile haijamalizika, Jeremia Kazeze ambaye alikuwa amerithi tabia ya kukurupuka kutoka kwa babu yake alimsukuma mke wa Veto na kuingia naye ndani kwa fujo.

Bila kutarajia akaitoa bastola yake asijue ni kwa nini alikuwa ameamua kufanya vile.

Wazo la kuwa yule mwanamke anamwongopea na Veto alikuwa yu ndani lilimfikisha hapo, akaamini kuwa Veto amenunuliwa tayari na upande mwingine.

Hivyo ilikuwa ni vita tayari.

Vita dhidi ya kijana wake mtiifu.

Giza lilikuwa limekikabili chumba, alivyoingia Jeremia mara ghafla taa ikawashwa, akababaika na kutamani angekuwa na macho memngi aweze kuona kila upande.

Mbele yake alikuwa Veto aliye hoi kabisa, kushoto alikuwa anatazamana na Inspekta Kobo ambaye alikuwa anaonyesha hali ya uchovu sana lakini anayetabasamu.

Wakati anajifikiria ni kipi anapaswa kusema akayaona macho makali ya Veto yakimulika kumaanisha kuna kitu nyuma yake, upesi akageuka na silaha yake.

Na pale akakutana na teke kali lililopiga silaha yake ikatua chini, kisha mpiga teke yule akafanya ujuzi wa ziada akazunguka na mguu uleule kisha akambamiza Jeremia katika kichwa chake.

Jeremia kazeze aliyesahau masuala ya mazoezi na kuruhusu mwili wake kuwa legevu wenye manyama uzembe alikuwa amepatikana. Lakini alijaribu naye kurusha ngumi ya hovyo, ikamkosa aliyekusudia, akayumba na kuliacha tumbo lake lililochomoza kitambi kama walivyo askari wengi wa Tanzania.

Tumbo lile likapokea tiba mbadala ya kuzuia kitambi.

Mateke mawili ya upesiupesi yakadunda katika tumbo lile.

Jeremia akatapika maji aliyokunywa nyumbani kwa IGP.

Kinywa kile kikawa kimefanya kosa la jinai kutema maji katika zulia lililokuwa na thamani ya juu, mpigaji akatokwa na ngumi nyoofu lakini ya kushtukiza ikakibamiza kile kinywa, kikaacha kutema maji kikatapika damu nzito.

Jeremia Kazeze akaanguka chini na kutulia magoti.

"Naitwa Martin, konstebo Martin Nguzu! Sikijui cheo kingine zaidi ya ukonstebo nilionao" Utambulisho ukatoka hatimaye. Huku anayejitambulisha akiwa amekunja ngumi za mikono yote miwili na mwili wake ukitetemeka sana.

Jeremia akaamini hiyo ilikuwa siku yake ya kushuhudia muujiza, anazungumza na maiti.

"Sikurithi cheo chochote kutoka kwa babu yangu nisiyermjua kwa sura wala sauti, nilirithi hiki unachokiona mbele yako mheshimiwa, sikurithi kupigiwa saluti wala kupiga saluti kinyonge.

Sikurithi roho ya kuua bila sababu na sikurithi udhaifu wa kufa kizembe.

Ninaishi katika misingi ya Florian Ngengekuzenza Nguzu, unaishi katika misingi ya Joseph Kazeze.

Babu yangu alishinda, aliniachia huu ushindi na katu hautakuja kupotea kirahisi, mliweza kuuteketeza mwili wangu lakini sio rahisi kuupoteza mzimu wa babu yangu.

Unapambana na mzimu, kama upo tayari unaweza kusimama tena ujaribu kuurushia ngumi mzimu!"

Alifoka kwa ghadhabu zote Martin Nguzu.

Jeremia Kazeze akabeua damu.

Angesema nini zaidi ya kuendelea kutema tu damu.

Baada ya Nguzu kumaliza aliyotaka kusema, akasimama Inspekta Kobo.

Pamoja na udhaifu wake uleule, hakuna aliyetarajia kuwa angeweza kuwa imara tena mpaka ambapo angepata tiba ya kutosha.

Naye akambana Jeremia Kazeze kadri alivyoweza, na hapo akataja alipo muandishi Juma Kihwele na familia yake, akalazimishwa kupiga simu na watu wale waachiwe huru mara moja.

Jeremia hakuamini hata kidogo kuwa alikuwa anachezeshwa ngoma ya namna ile na vijana wale.

Hakuwa na la kufanya akatii.

Maelezo ya ziada yakatolewa, simu ikapigwa kwa IGP kuhusu ujio wa Juma Kihwele katika himaya yake.

IGP wakati anapigiwa simu ile alikuwa tayari katika sare zake na alijisikia faraja kwenda kuimaliza vita ile angali ana nyota tele katika bega lake.

Vita ilikuwa inaelekea ukingoni kabisa, Konstebo Martin Nguzu akaingia katika chumba kimojawapo na kumkuta Koplo Zubeda akiwa katika usingizi mzito.

Akamwinamia na kuzungumza naye maneno kadhaa ambayo aliamini fika kuwa hataweza kuyasikia.

Kisha akambusu katika paji lake la uso.

Akaliendea dirisha kubwa la kioo, akaruka na kutoweka akipishana na gari kadhaa za polisi zikiwa zinalikaribia eneo lile.

Wazo la kwanza lililomuondoa ni Zubeda. Asingeweza kuendelkea kuwa naye katika mahusiano mwanamke ambaye ni usingizi wa inspekta Kobo, pia asingekuwa na amani kumwona binti yule katika mahusiano mengine hata kama ataachana na Inspektra.

Pili ni upindishaji wa sheria katika ardhi aliyokuwa ameikanyaga, masuala ya kubebana kwa sababu ya kujulikana aliyafahamu wazi kabisa.

Akakihesabu cheo nchake cha ukonstebo, cheo cha Zubeda ukoplo na Inspekta Kobo. Akajaribu kufananisha na kile cha Jeremiah aliyewahi kuwa mkuu wa majershi ya polisi IGP.

Akaamini fika kuwa lolote linaweza kutokea, aidha kuzimishwa hapohapo na kisha taarifa kubadilishwa kuwa waliuwawa wakikabiliana na polisi, ama la kubadilishiwa kesi kabisa na kuonekana walimteka Jeremia na kumtesa kesi ambayo katu isingeweza kuwaacha bila hatia.

Miaka thelathini ingewahusu pamoja na mateso makali.

Konstebo Martin Nguzu, akayaweka mapenzi kando, akautazama usalama wake.

Kubwa zaidi alikiri kuwa hakuwa yeye yule konstebo mnyonge, huyu alikuwa imara na alikuwa na kazi kubwa zaidi za kufanya kuliko kuendelea kuwapigia saluti watu kama Jeremia Kazeze.

Konstebo Martin Nguzu akazidi kukata mitaa jijini Dar es salaam, hatimaye akaipata nyumba ya kulala wageni.

Akamtazama muhudumu aliyekuwa ana mawenge ya usingizi.

Akaulizia bei ya chumba akatajiwa, akalipia na kushangaa anapewa funguo bila kusajili jina lake.

"Hee! unaniruhusu tu naingia kama unanijua vile."

"Ah! bro we kalale bwana..."

"Hapana lazima niandikishe la si hivyo nilale bure." akatilia mkazo.

Huku akiwa amekereka yule binti wa mapokezi akampatia daftari huku akihangaika kuipata kalamu.

Hatimaye Nguzu akaishika vyema kalamu, akautazama mstari wa kuandika jina, akatokwa na tabasamu la ushindi kisha akaandika kwa herufi kubwa kiasi cha kuingilia hadi mstari wa chini.

"KONSTEBO MARTIN NGUZU"

Hakujaza sehemu nyingine zilizosalia.

Akamkabidhi daftari akiwa amelifunika na kuamini fika kuwa kwa jinsi alivyoelemewa na usingizi hataweza kusoma, na hata akisoma ataambulia patupu.

Alivyokifikia chumba, akaitoa bunduki yake. Akatoa risasi na kisha akauvamia ukuta na kuandika kwa kukwangua rangi. Huku akiifurahia hali hii, alijiona hana namna nyingine ya kufanya sherehe zaidi ya hii.

Akauchubua vyema hadi ukasomea alivyotaka.

"NAITWA MARTIN, KONSTEBO MARTIN NGUZU"

Akapiga saluti na kisha akalala vyema.

Alfajiri akatoweka.

Akaelekea popote watu wanapoelekea lakini mwisho wake akiutambua yeye mwenyewe.

MWISHO

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni