MKONO WA JASUSI (18)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA KUMI NA NANE
ILIPOISHIA...
“Huu ndio mtaa wa Shilowane?” akawauliza.

“Nilijua tu we mgeni. Unatoka wapi?” kijana muuza viatu aliuliza.

Kamanda hakujificha akamweleza kuwa yeye ni Mtanzania.

“Aaaa wa nyumbaniiiiii!!!!”

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI

ENDELEA...
Yule kijana akashangilia kumbe na yeye alikuwa ni Mtanzania.

“Hongera kwa bishara, naona mbao imejaa,” kamanda akamweleza.

“Asante tunaganga njaa kwa watu huku, cha muhimu na kizuri ni kuwa watukubali sana hawa jamaa, tunaishi kwa amani,” Yule kijana akaongea kwa furaha sana.

“Ok, ni vizuri lakini usisahau nyumbani,” akamwambia huku akimpa mkono kumuaga.

Wakapiga picha ya pamoja kwa simu ya Yule kijana, wakaagana. Kamanda Amata akapita katika mtaa huo na kuitafuta nyumba anayoitaka. Alipoteremka mteremko mkali kidogo akakutana na barabara ya lami, akakunja kulia na kuielekea nyumba kubwa ya kisasa iliyozungukwa na miti mingi sana na bustani ya kupendeza, akavuta hatua mpaka getini, hakuona mtu yeyo tee neo hilo, akashika vyuma vya geti hilo na kuruka mpaka ndani, akatua taratibu bila kufanya ukulele wowote. Alipotua ndipo alipomwona mlinzi mmoja akiwa upande wa pili, moja kwa moja akamzunguka na kutumia dirisha la upande mwingine kujipenyeza ndani ya jumba hilo. Akapita taratibu na kuingia kwenye kijiofisi kidogo kilicho ndani ya jumba hilo. Ukutani alikaribishwa na picha kubwa ya Lereti Khumalo, akaibusu.

Akaanza kupekua hapa na pale mpaka alipokuta lile faili lenye mkataba wa kibiashara wa Mgodi wa Mzee Khumalo na Robinson, lakini pale alikuta mikataba miwili. Kamanda akapigwa na butwaa upi ni sahihi kati ya huu na huu mwingine, akavuta kiti akaketi, akaiperuzi harakaharaka yote miwili, ule wa pili nyuma yake uliandikwa kwa mkono maandishi yanayoonesha kuwa mkataba huo haukuwa sahihi, umerdurufishwa na kubadilishwa.

“Hii ni sababu?” akaongea kwa sauti ndogo, akaiweka pembeni ile mikataba, akavuta na faili linguine akakutana na ripoti ya vifo vya wale wachimbaji kule mgodini, nayo nakaipitia vyema ilieleza mambo mengi sana ikiwemo tatizo la mashine za hewa lililosababisha watu hao kukosa hewa safi na kufa. Akausoma kwa makini sana alipouelewa akaufunga na kuuweka pamoja na ile mikataba. Kamanda Amata alijua moja kwa moja kuwa ni mambo yale yanayohatarisha maisha ya mrembo huyu.

“Kwa nini watake kumuua?” akajiuliza.

“Lazima kuna linguine ambalo nitalijua tu,” akajijibu.

Akatazama huku na kule akaona kuna mkoba, akaunyayua na kutoa vilivyomo akaiweka ile mikataba na ile ripoti ya vifo, akauvaa mgongoni mwake, koti lake la suti akalipachika kwenye kiti cha ndani ya ofisi hiyo, akauvua mkanda wa kushikia bastola na kuutia ndani ya begi, bastola yake alkadhalika.

Akaandika memo ndogo na kuiacha mezani kisha akaondoka zake kwa njia ileile aliyoingilia na kumwona Yule mlinzi akiwa palepale, akatoka na kupotea.

Moja kwa moja alifika uwanja wa ndege na kuondoka kwa ndege ya kukodi kurudi Johanesburg.


DON ANGELO alikuwa akizunguka zunguka ndani ya sebule yake akiwa hajui nini la kufanya, alipata pigo ambalo hakuwahi kulipata. Vijana wake waliokuwa hapo na viongozi wengine wa taasisi yake walikuwa kimya kabisa, wote wakiwa katika sare yao ya suti nyeusi na kofia za pama. Ni mchana huo tu walikuwa wamepoteza vijana watano kwa mpigo akiwemo muaaji mwenye taaluma hiyo aliyekuja kutoka Cape Town, aliaminiwa kwa kazi kama hizo lakini safari hii aligonga ukuta.

“Nani anayeitikisa ngome yangu, ngome ya chuma?” alipiga kelele, na wengine walibaki kimya.

“Nauliza serikalini, eti hawajui! Wanatufanya sisi vikaragosi? Katoka wapi huyu shetani mweusi anayetafuna nafsi yangu huku namwona?” aliendelea kupiga kelele na hakuna aliyejibu, kila mmoja alikuwa kwenye mawazo mazito.

“Na sasa ametoweka Durban, ni mjanja kiasi gani cha kutushinda sisi, sisi, sisi?” aliongea kwa msisitizo huku bado akitembea tembea, akainua mvinyo wake na kupiga funda moja kubwa la nguvu, akabeua.

“Kaenda wapi? Cape Town? Au kakimbilia Mozambique? Au wapi, eti ni Mtanzania, Tanzania ina ina mtu hatari nana hii? Lazima serikali iniambie ukweli imemkodi wapi mtu huyu anayetaka kuharibu mipango ya wanadamu,” akajitupa kochini.

Zebel,” akaita, “Sikiliza, nina uchungu sana mpaka sasa vijana wangu kumi wamekufa kwa mkono wake, nahisi huu si mkono wa kawaida, ni mkono wa jasusi, jasusi linalojua kazi yake, na jasusi lazima apambane na jasusi. Zebel, namtaka huyo mtu hapa awe amekufa au maiti, nenda, tumi kila unachokitaka, na Yule mwanamke kama hajafa nataka amaliziwe,” akamaliza na Zebel akaondoka akiwaacha wale madigala wakibaki na boss wao mkuu Don Angelo kulijadili hilo.

§§§§§

KAMANDA AMATA alipofika Johanesburg, moja kwa moja aliiendea gari yake na kuingia ndani. Mara hii gari yake ilikuwa ya kijani. Kwa jinsi ilivyotengenezwa iliweza kujibadili rangi kila inapopigwa na jua kali. Akatoa yale makabrasha na kuyahifadhi kwenye box maalumu lenye madini yanayozuyia kilicho ndani kutoathirika kwa moto. Akakipachika chini ya siti ya dereva ambako ndiko kinakoishi daima. Akawasha simu yake ya ndani ya gari na kukuta missed call toka TSA makao makuu. Akaipiga tena kuiweka sikioni.

“Madam S” akaita.

“Yeah my son, nipe habari maana upo kimya sana,” akamwambia.

“Kazi inaendelea, na inakaribia ukingoni niko njiani kumbaini masterplan wa kila kitu, mpaka sasa nina majina mawili mkononi sasa nataka kuhakikisha nani ndiye hasa mkuu wa kitengo,” akajibu.

“All the best,” simu ikakasika. ‘Madam S, daima hupenda kujua kila kinachoendelea, mwanamke shupavu anayejali watu wa idara yake,’ akawaza na kutabasamu. Alipoitazama saa yake ilikuwa tayari saa kumi na mbili jioni. Akaiondoa gari yake taratibu na kuliacha eneo hilo.

Saa tatu usiku ilimkuta katika mgahawa wa kienyeji huko Soweto akipata chakula cha kawaida tu, aliepuka kubaki mjini kwa kuhofia kugundulika kurudi kwake kwa maana alikuwa na uhakika kuwa hakuna anayejua kama amerudi nayupo hapo Joh’burg.

Usiku ulipomtosha alijipanga kuingia kazini, sasa ni kuikabili nyumba ya Zebel na Zebel mwenyewe, alijua wazi kuwa kutoka kwake ataweza kujua A na B kwani ndilo aliloachiwa na marehemu Jesca katika kile kijikaratasi. Akawasha gari na kuondoka zake.

MTAA WA SPRINGBOCK

KAMANDA AMATA aliendesha gari yake taratibu akitafuta nyumba namba 320U kama alivyoelekezwa, haikuchukua muda kuiona, akaegesha gari mbali kidogo na kuteremka. Akatumia miguu kuja katika nyumba hiyo huku akihakikisha bastola yake ipo sawa, alipolifikia geti akakuta limefungwa, akatumia funguo zake za siri na kulifungua, akaingia ndani, moja kwa moja aliingia katika jumba hilo, hakukuta mtu, alipita hapa na pale akapekua huku na kule. Katika chumba cha kulala ndipo alipokuta kile anachokitaka, taarifa halisi ya vifo vile vya watu kumi na tano kule mgodini, iliyoandikwa na Dokta Nkosizulu, akaichukua na kutoka nayo mpaka mahali Fulani mlemle ndani ya lile jumba, akajua wazi kuwa kama mtu huyo atarudi, basi lazima apite hapo.

Akaketi kitini pembezoni tu mwa mlango, huku akitumia tochi yake ndogo kumulika alikuwa akiendelea kuisoma ile taarifa. Taarifa ile ya Dokta Nkosizulu ilieleza bila kificho kuwa watu wale wamekufa kwa kuvuta hewa ya sumu ya Carbon Monoxide, kisha ilieleza uchunguzi wote jinsi ulivyofanyika ikiwa ni pamoja na ubongo wa wahanga ambao ulionekana sehemu Fulani Fulani kuwa na rangi nyekundu, hili nalo ni tokeo mojawapo la mtu anayevuta hewa hiyo kwa wingi. Amata akatikisa kichwa na kujihisi chozi likitaka kumdondoka, alijawa na huruma sana kwa vifo vya hawa jamaa na vile alivyovichunguza vya watatu wengine, na lililomshangaza ni kuwa kwa nini wafe Waafrika.

‘Ushahidi wa mwisho nitaupata kwa Lereti, sasa bado hatua moja kisha utekelezaji wa kazi,’ akawaza na kucheka mwenyewe. ‘Yaani hapa kazi bado haijaanza, bado kabisaaaaaa,’ akiwa kazama kwenye mawazo hayo, akasikia mngurumo wa gari nje ikisimama, akainua bastola yake na kuiweka tayari mkononi mwake, lakini aliendelea kuketi palepale.

“Yaani huyu jamaa anatufanya sisi mabwege,” alisikika mwanaume akiongea kwa lugha ya kiingereza.

“Tutampata tu, atakufa kifo kibaya sana, naapa,” mwingine akadakia. Kwa kusikiliza michakacho ya viatu alijua watu hao wako watatu, ulikuwa mtihani kwani hakujua nani atakuwa ndiyo Zebel, lakini alitumia mbinu ya kiintelijensia kuwa watu wakiwa wengi atayefungua mlango na kuingi kwanza ndiye mwenye nyumba au mwenyeji kwa asilimia tisini. Hivyo akapanga na kupangua kichwani mwake akajua la kufanya, ‘Sina mda wa kupoteza’ akawaza.

“Lazima afe usiku huu!” sauti nzito ya mtu mwingine ilisikika, ‘Utakufa wewe kwanza, sekunde kumi zijazo,’ akajibu kwa kuwaza.

Mlango ukafunguliwa, na mtu wa kwanza akaingia akielekea kwenye ile sebule kubwa akifuatiwa na wawili nyuma yake….

KAMANDA AMATA kutoka pale alipoketi alimwangalia Zebel akiingia na kufuatiwa na wale vijana wawili, hakuwasemesha lolote. Aliwaona wale jamaa walivyojazia miili yao kimazoezi ijapokuwa hawakumfikia bado Zebel Pinch aliyeonekana kwenda heani na kujaa vizuri sana, kwa mtazamo wa kijasusi alioutumia Amata aligundua kuwa Zebel ni mtu hatari ndio maana hata Don Angelo aliamua kumuweka juu ya wengine. Alipoiendea swichi ya taa na kutaka kuiwasha; Kamanda Amata akawasha kupitia swichi iliyo nyuma ya mlango huo. Zebel alipoona taa inawaka ilhali yeye mwenyewe hajawasha, kabla hajaangalia upande ule wa mlango alijirusha kwa ustadi na kutua nyuma ya ukuta mfupi uliuotenganisha sebule na ile sehemu ya kulia chakula.

Wale vijana wawili walishindwa kumpotea Kamanda kwani walipotaka kuleta makeke tu, bastola ya Amata ilifanya kazi madhubuti kabisa na ikawatoa uhai kila mmoja wa sekunde yake, wakajibwaga chini na kuiacha meza nzuri ya kioo ikipasuka vipande vipande.

“Zebel Pinch! Inuka utazamane uso kwa uso na mkono uliomuua Tracy Tasha na wewe utaingia kwenye orodha ya mkono huo,” Kamanda alimwambia Zebel huku akiunguka kwa ufunsi kabisa ile sebule.

Amata Ric, umejiingiza kwenye mchezo mzito usiouweza, kama uliingia kwenye nyumba hii kwa miguu yako utatoka kwa miguu yaw engine,” Zebel akajibu.

“Hujiulizi nimefikaje nyumbani kwako? Je unafikiri ningeshindwa kukuaa kwa bunduki yangu pindi tu ulipoingia? Sikutaka kufanya hivyo kwani nina mazungumzo na wewe kwanza kabla ya kifo chako,” Kamanda akatamba.

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni