KONSTEBO NGUZU (17)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA KUMI NA SABA
ILIPOISHIA...
Majira ya saa sita usiku aligutuka kutoka usingizi huku jasho likimtoka sana.

Majenga! jina hili likakivamia kichwa chake, akaketi kitako na kuanza kukumbuka juu ya maneno yale aliyokuwa akiyasoma yule mzee.

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
Akatamani asubuhi ifike upesi aweze kuendelea kusikiliza ni kipi ambacho kitakuwa na faida kubwa sana kwake.

Akamaizi kuwa licha ya kushtuka vile na kuandamwa na jina hilo lakini pia alikuwa pia amebanwa na haja ndogo.

Na choo kilikuwa mita nyingi kutoka chumba alichokuwa amelala.

Akapatwa na uvivu sana huku akijilaumu kwa kukataa kunywa maji mengi baada ya chakula cha ili asije kupata shida kama hizi usiku na sasa amezipata shida zilezile.

Akajivuta taratibu kuelekea choo kilipokuwa. Nje palikuwa kimya sana, walisikika wale viumbe wanaopenda kulala mchana kisha usiku wanazurura kusumbua viumbe wengine.

Popo!

Umbali wa choo ulimtatiza sana, akajiona mpuuzi sana giza lote lile kuna vichaka vya hapa na pale ni kwanini ahangaike na choo.

Akakiendea kichaka kidogo alichokiona karibu yake.

Akakidhi haja yake lakini hakuweza kugeuka kabla ya kusikia sauti ikimuamuru asimame.

Akasimama tuli!

"Kwanini unakojoa vichakani we tahira?" sauti ikakaripia.

Martin Nguzu akastaajabu, tangu afike pale Shinyanga sauti karibia zote zilikuwa zinaambatana vyema kabisa na lafudhi ya kisukuma, iweje hii sauti inakuwa na miporomoko ya pwani ama Zanzibar?

Hakujibu kitu!

"Nakuuliza weye mwanaharamu..."

"Nisamehe tafadhali..." Hatimaye akazungumza.

"Mzee Majenga analala chumba kipi hapa? na ni nani ako...." Swali likatupwa.

"Analala nyumba kubwa!"

"Geuka utupeleke upesi.."

Nguzu akageuka na kukutana na mambo aliyoyazoea.

Mitutu ya bunduki.

Walioibebwa waliishika kizembe sana. Ni vile hawakujua kuwa ile hatari inayodhaniwa kuzikwa katika tanuru la moto, iliishia kung'arishwa na kuwa dhahabu yenye thamani kali huku ikiwa na makali ya kisu kipya.

Walisimama wanaume wawili, mmoja akiwa na bastola mkononi mwake. Huyu aliielekeza kwa Nguzu.

Nguzu akajitia kutetemeka huku akiwasihi wasimuue. Kutetemeka kule kukawazidishia uzembe.

Mmoja aliyebaki akasikika akizungumza kwenye simu kuwataarifu wenzake kuwa wamefika eneo la tukio na muda si mrefu watauchukua mzigo wao.

Walitembea hatua kumi kuelekea ilipokuwa nyumba ya mzee Majenga na familia yake.

Nguzu alizihesabu zile hatua vyema huku macho yake yakiwa makini sana kutazama kitu.

Hatimaye akakifikia, kilikuwa ni kigogo kilichokuwa njiani. Akakikanyaga na kujikwaa maksudi.

Akaanguka chini huku akitokwa na yowe la hofu.

"Inuka hanithi wewe..."

Kauli hii aliisubiri Nguzu kwa hamu, mkono wake ulikuwa tayari na jiwe, akatumia sekunde chache kubaini kuwa mshika bastola yule hakuwa anakaribia kufyatua, kidole chake kilikuwa mbali kabisa na kifyatulio.

Safi sana! akajisemea na hapo akajitutumua ainuke.

Alipoinuka akaliachia lile jiwe likampata bwana mwenye lafudhi ya kipemba usoni, kapiga yowe huku bunduki ikimtoka.

Yule mwenzake akajiweka sawa kufanya shambulizi kwa kutumia bunduki.

Nguzu akajirusha huku goti lake likitangulia mbele hadi katika kifuani kwa adui.

Akambwaga chini.

Nguzu akaitwaa ile bunduki.

"Acha ujinga dogo, vita sio kama kunywa urojo unakunywa hata kama ni kibogoyo. Vita inahitaji watu majasiri." Alimwonya alipomuona akitafuta bastola.

Yule bwana akatulia asiamini kuwa kibao kimewageukia wao.

Mwenzake alikuwa amekodoa macho.

"Mwambie jamaa aje moja kwa moja eneo la tukio, ukiongeza neno nakuua muda huu, na usipoongeza nitakuua baadaye." Nguzu akaamrisha.

Simu ikapigwa jamaa akazungumza aliyopaswa kuzungumza. Kisha simu ikakatwa.

"Nilikueleza ukiongeza neno nakufanyaje?"

"Unaniua!"

"Na usipoongeza?"

"Utaniua baadaye. Nisamehe tafadhali sisi tunatumwa tu" alijibu huku akitetemeka.

Nguzu akamgeukia yule mpemba.

"Shehe! mwenzako kaongeza neno tayari, anasema nimsamehe na sikusema hivyo." Hakusubiri jibu, akaigeuza bunduki, hakutaka kupoteza risasi akaizamisha bunduki katika kifua cha yule bwana singe ikaingia nzima nzima.

Akagalagala kuusaka uhai wake.

Mpemba akakurupuka akairukia bastola. Lakini hakuweza kufyatua kabla Nguzu naye hajamrukia na kumkanyaga mkono.

"Swahiba, nakukumbusha tena huu sio urojo kila mtu anakunywa." akamtia ngumi kali katika paji la uso wake.

Ilikuwa ni vita ya kistarabu sana, mtu akianguka chini waliolala wanajua ni maembe yanaanguka, wanajigeuza upande wa pili na kuendelea kuota ndoto zao.

Hawakujua kuwa roho zilikuwa zinatoka na uwanja ule ulikuwa umegeuka kuwa wa kivita.

Nguzu akambana maswali yule mpemba, akajibu kuwa huyo anayekuja ndiye kiongozi wao, wenyewe hawajui kiundani juu ya tukio lile.

"Kwa maana hiyo unamaanisha wewe hauna umuhimu wowote kwangu sivyo."

"Walah! naapa mie wanionea bure tu sina nijualo." Jibu lile likawa la mwisho.

Kama hauna maana unabaki na Nguzu kufanya nini.

Akaunganishwa katika safari ya mwenzake aliyekuwa ametulia tayari.

Nguzu akaweka windo lake kumngojea huyo aliyeitwa mjua mengi.

Windo hili likazua safari mpya ya Konstebo Martin Nguzu kurejea jijini Dar es salaam.

Jiji ambalo linaamini kuwa yu kwa muumba akijibu tuhuma zinazomkabili. Huku wengine wakiamini bado anahangaika na adhabu ya kaburi.

ILIKUWA safari iliyojaa katika kichwa chake ghafla baada ya vita ile ya usiku iliyoondoka na uhai wa watu watatu ambapo mmoja kati yao alikuwa ni kiongozi wao kwa mujibu wa maelezo yao.

Martin Nguzu ambaye sasa hakuwa akiushangaa uwezo wake wa kukabiliana na maadui alikuwa amewaangusha wengine watatu huku akifanikiwa kuwapokonya bunduki tatu pamoja na risasi za kutosha kabisa.

Hakutaka kulala baada ya kuhakikisha ameitelekeza ile miili mbali na ngome ya mzee Majenga. Alimwamsha mzee Majenga na kumweleza kwa ufupi juu ya kilichotokea.

Tofauti na matarajio yake kuwa taarifa ile itamtisha sana Majenga, hii ilikuwa kinyume. Mzee Majenga akatokwa na kicheko kidogo kisha akampigapiga kifuani Martin Nguzu na kumwita kwa jina la babu yake.

"Ngengekuzenza Nguzu umezaliwa upya..." Kauli ile ilimtoka na kumwacha Martin Nguzu katika pumbazo asielewe ni kitu gani bwana yule alimaanisha.

"Mimi nimezeeka kijana wangu, niliisubiri sana hii vita kwa muda mrefu lakini imekuja nikiwa mzee tayari. Nenda ukapambane hii ni vita yako na inakuhusu. Nakuachia haya maandishi niliyoyaandika bila kuongeza wala kupunguza neno kutoka katika kinywa cha hayati babu yako anayeishi sasa katika nafsi yako. Hakikisha unayamaliza yote kabla haujaivaa hiyo vita...... mimi nitakuwa salama kabisa na tutakutana nikiwa hai, na hata nikifariki ni kwa sababu ya uzee tu..." Aliongea kwa ujasiri mkuu. Kisha akachechemea hadi ndani na kuchukua makaratasi yaliyoandikwa kwa kalamu akamkabidhi Martin.

"Nilikuwa napenda sana kuandika na babu yako alikuwa anapenda sana kunisimulia, nadhani ni maneno hayo kwa ufupi yatakupa jawabu nilikutana vipi na babu yako." Majenga alitoa kauli ile na Martin akaipokea lakini alikuwa na swali la ziada.

"Niliokoka vipi katika ule moto jijini Dar es salaam?"

"Mzee wako asingeweza kukuacha uangamie. Wazee wa zamani hawakuwa wa kawaida, akinuia jambo linakuwa kama lilivyo, nadhani ni kutokana na kutenda dhambi chache nd'o maana Mungu alikuwa akiwasikiliza." Alifafanua na kuzidi kumvuruga Martin.

Akagundua mvurugano ule, akaongezea "Kasome haya yote kabla hujaamua wapi pa kuanzia"

Maongezi yakaishia hapo.

MAANDISHI YA NGENGEKUZENZA.

Ubaya ni kwamba wakati wa ukoloni, sisi watu wa rangi nyeusi hatukuishia tu kunyanyaswa na ngozi nyeupe katika uhai wetu, hata ulipokuja ustaarabu wa kuhifadhi maiti zetu sisi tuliwekwa katika kundi la mbwa koko aliyefia jaani baada ya kukabwa na mfupa aliodhani ni mnofu.

Ukipata bahati sana unafukiwa, ila ni waafrika wachache waliokuwa na bahati, wengi tulitunukiwa nuksi.

Ukiwa na nuksi unaachwa hapohapo ulipofia ama unasogezwa kidogo porini, ukawe chakula kwa wanyama wenye tabia ya uvivu katika suala la kuwinda na ndege wanaoona sifa kudonoa donoa.

Hata babu yangu alikuwa na nuksi vilevile baada ya kufariki alitupwa, akaipata bahati akiwa maiti tayari waafrika kadhaa wakamfukia.

Baada ya kuupata uhuru wetu nikawa naitembelea ile sehemu niliyoaminishwa kuwa babu yangu alifukiwa pale, pakawekwa alama nami nikawa naenda kumsalimia na kuzungumza naye bila kujali ananisikia ama la!

Sasa yule mwanahizaya baada ya kuona haitoshi kumchukua kiharamia mke wangu na kuniacha katika jitimai, akaona hata! hii haitoshi huyu bwege bado anapata raha. Akaanza kuniandama kivingine, najua aliwatuma mashushu wake waliokiamini na kukiabudu chama chao kuliko Mungu wa mbinguni na miungu ya porini.

Hawa wakamfikishia habari kuwa ninayo furaha nyingine, furaha ya kuzungumza na babu yangu makaburini.

Ikapita ajenda katika siku nisiyoijua na baadaye ikawa ni amri bila kutahadhalishwa.

Eneo lile lilipaswa kupandwa miti, mara lilitakiwa kupita barabara.

Sikuelewa hata kidogo, na hakuna aliyesubiri nielewe.

Kwani Ngengekuzenza nani mpaka aelewe?

Lile nililoamini kuwa ni kaburi likavunjwa na huyu mkoloni mshenzi mwenye rangi kama yangu huku akiiga miondoko ya wazungu na afro yake kichwani akiipaka kalikiti na kuwa laini kama nywele za mkoloni.

Lugha yake pia ilifanana na yao.


Kama ni kunipiga, hapa alinipiga na mjeledi wa chuma nikaangukia pua huku mikono yangu ikishika makaa ya moto.

Huyu mjinga aliniweza hakika!

Uchungu wangu ule nikamshirikisha mwanangu Salama nikamweleza kuwa Jose anataka kuvuka mipaka ambayo ameivuka tayari, yaani sielewi anachotaka.

Salama alinisihi niachane naye, nikaona hajui uchungu ninaoupitia kwa kupokonywa mke na kisha hapohapo nikapokonywa furaha yangu.

Babu yangu!

"Salama, nikiachana naye akagundua nina furaha kuwa na wewe atakuchukua na wewe pia...." nilimwambia Salama. Wazo hili likamkuna na kuiona hatari ya waziwazi.

"Sasa utamfanya nini?"

"Yule ni mjinga tu kwangu, nataka nimfanyie yale mambo ambayo wajanja huwafanyia wajinga wanaodhani pesa nd'o ujanja." nilimweleza huku nikiona wazi kuwa hanielewi.

"Unataka upigane naye?" aliniuliza.

"Nikipigana naye wote tutakuwa levo ileile ya ujinga, nataka nimpige ili tuunde daraja kati ya nani mjinga na nani mjanja."

"Lakini baba, huyu ana pesa na cheo atakusumbua sana. Yaani nina uhakika hautafikia hata nusu ya azma yako."

"Kwanini unasema una uhakika." nilimuuliza salama.

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni