Machapisho

KONSTEBO NGUZU (18)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA KUMI NA NANE
ILIPOISHIA...
"Lakini baba, huyu ana pesa na cheo atakusumbua sana. Yaani nina uhakika hautafikia hata nusu ya azma yako."

"Kwanini unasema una uhakika." nilimuuliza salama.

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
"Si kila kitu kipo wazi, ana pesa na vyeo na zaidi ana kundi kubwa la watu linalomzunguka."

“Nd’o maana unasema ni hakika?”

“Ndio baba”

"Sikiliza mwanangu Salama na uliweke hili milele katika maisha yako, hapa duniani kuna kitu kimoja tu nd'o cha uhakika vingine vyote si vya uhakika. KIFO pekee ndo jambo la uhakika, kila mtu atakufa hii haina mjadala. Ujiue, unyweshwe sumu, ugongwe na gari ama hata ukilala usiamke. Vyote vina maana moja tu ya uhakika.... asije akakudanganya mtu kuwa jambo hili ni uhakika... anakulaghai na wewe unayemsikiliza na kumkubalia unakuwa upande wa mjinga. Sipendi uwe mjinga siku moja...." Nilimsomea mambo yale. Yakamuingia na kumpa ujasiri naye akanibariki katika uamuzi wangu na hiyo ilikuwa ni mnamo mwaka elfu tisa mia themanini na tatu ama nne kama sijasahau.

Sijui itakuwaje miaka ya huko mbele lakini enzi zetu hizi hapakuwa na ulinzi wa kutosha kwa viongozi, ulinzi huo tuliusikia tu na kuuona walipokuja viongozi kutoa nje, Mwalimu Julius Nyerere alihamasisha sera za kuishi kijamaa, nasi tukaamua kuishi kama ndugu.

Hapakuwa na wa kumpinga kirahisi mwalimu. Ukitaka kumpinga sisi tunakwambia nenda ukapambane kuileta Tanganyika huru ndipo ujilinganishe na mtaalamu huyu.

Hivyo tuliishi kijamaa sana, halikuwa jambo la ajabu kukutana na mwalimu Nyerere barabarani na kusalimiana naye kwa kushikana mikono. Sasa vipi kuhusu mjinga huyu anayeitwa Joseph Kazeze?

Sidhani kama kwa miaka yenu huko mbeleni itakuwa hivi. Nahisi hata balozi naye atatafuta ulinzi...

Nilikueleza awali kuwa tangu nilipokuwa mtoto nilikuwa nina uwezo mkubwa sana darasani, hata akili yangu haikuwa ndogo katika kufikiri.

Nikaamua kuitumia akili yangu kumwonyesha yule bwana nini maana ya mwanaume kutoa machozi.

Kwakweli nilimkosesha amani!

Kwanza nilifurahia kile kitendo cha mwalimu Nyerere kutowafukuza wazungu baada ya kutupatia uhuru, hivyo upatikanaji wa silaha hadi miaka ya themanini bado ulikuwa ni mwepesi sana, unaweza kuipata bunduki hata kwa kubadilishana na gunia la mahindi pekee.

Zilikuwa zimezagaa.

Nami nikajipatia bunduki yangu, uzuri nilipitia jeshini hivyo sikuhitaji kufundishwa lolote.

Nikamuaga mwanangu kuwa naanzisha mapambano rasmi.

Sikuwahi kuua ila nilijeruhi sana.

Nilianza na baba yake mzazi, akiwa katika mizunguko yake. Nikamteka na kumpiga kipigo cha mbwa mwizi, akavunjika mkono.

Sikumtumia salamu Jose Kazeze kama ni mimi ili aendelee kuhadaika.

Akafuata mdogo wake, huyu nilimfungia safari hadi Morogoro, nikamkamata na kumfunza adabu asiweze hata kuiona sura yangu.

Jose Kazeze kitu alichosahau ni kwamba sisi tulikuwa marafiki na nilimfahamu vyema yeye na familia yake.

Niliendelea kumpa presha bwana yule kwa kufikia hatua ya kuvamia kwake nikarusha risasi zikavunja vioo vya nyumba aliyokuwa akiishi lakini sikumdhuru mtu na sikutaka kumdhuru.

Uwezo wangu katika kupanga matukio ulianza kunishangaza hata mimi, kila nikilala na kuamka nawaza pigo jingine.

Jose akaanza kukonda!

Mara akaachana na yule mwanamke aliyenipokonya.

Nami sikurudiana naye mjinga yule aliyekosa hata nukta ya akili.

Nilikuwa nina hasira kali.

Baadaye baba yake alifariki, kwa magonjwa mengine sijui kama na kile kipigo kilichangia.

Sikujali!

Siku mbili baada ya kuzikwa nikaenda makaburini, huku nikaweka bomu nililolipata kwa bei nzuri tu.

Likafanya mlipuko uliotikisa nchi.

Hakuna kilichobaki zaidi ya jeneza kusambaratika huku na kule.

Hili lilikuwa pigo kubwa zaidi, wanandugu wakalundikana nyumbani kwa Jose Kazeze kujadiliana nini kinaendelea.

Nikavamia na huko na kurusha bomu jingine katika choo kilichokuwa mbali kidogo na nyumba na hii ni baada ya kuhakikisha hapakuwa na mtu ndani yake.

Mparangano uliojitokeza nilijikuta nacheka mwenyewe.

Amakweli mtenda akitendwa....

Jose akazidi kuzorota kiafya.

Ni hapa ndipo nikaamua kumweleza bayana ili kama ni kufa kwa mshtuko afe tu, who cares?

Hakufa!

Ila alipagawa vibaya mno, na hapo ndipo ikaanzishwa oparesheni ya Ngengekuzenza Nguzu anasakwa auwawe.

Kisa ni jambazi, yakaundwa matukio ya kushangaza kunihusu mimi na hapo nikaanza kusakwa rasmi.

Nilijua kuwa hali ni mbaya, nikaraejea kwa mwanangu... usiku wa mwisho kumwona mwanangu.

Akanieleza kuwa yu mjamzito, nikamweleza kuhusu kinachoandikwa na magazeti ya serikali huku nikimweleza kuwa moyo wangu u radhi kuwa nimemuweza yule bwana.

Zaidi ya hayo nikamsihi kuwa iwapo atazaa mtoto wa kiume basi amwite Nguzu!

Tulikumbatiana huku sote tukishindwa kuyazuia machozi.

Nikaondoka na kuja kwako Majenga unihifadhi nikusimulie ya kuandika kama ulivyohitaji wewe kijana wangu.

Na nimejitahidi sana kukusimulia.

Maandishi yale yaliacha nafasi kubwa kisha ikafuata aya ambayo mwandishi wake alikuwa ni Majenga.

Mnamo mwaka 1988 mwezi wa kumi na moja mzee Ngengekuzenza mwenye msongo wa mawazo kwa kuishi maisha ya mashaka kila kukicha aliniaga kuwa anakwenda msalani, ilikuwa majira ya usiku. Hakurejea mapema nikalazimika kutoka pamoja na mbwa kwenda kumtafuta.

Nilimtafuta sana hadi pambazuko likanikuta nikiwa namtafuta, mbwa asiyechoka ndiye alinihimiza kumsaka mzee wangu nimpendaye.

Hatimaye nikaufikia mti ambao alikuwa amejitia kitanzi.

Nasikitika kuwa sikuwahi kukiri kuwa ninamfahamu mzee yule kwa sababu za kiusalama, alikuwa anasakwa sana na jeshi la polisi kama jambazi sugu.

Niliporejea ndani nikakutana na karatasi katika kitanda alichokuwa akilalia. Haikuwa na maneno mengi sana aliniandikia kama nilivyokuwa nimefanya tayari.

"Umenihifadhi kwa moyo wote wa upendo, wewe ni kijana wangu nikupendaye. Ninaomba uendelee kunitunzia maneno yangu..... utawapatia wajukuu zangu ili wajifunze kuwa babu yao hakuwahi kuwa mtu dhaifu hata kama nilionewa, babu yao sikuwahi kuwa jambazi hata kama watayaona maandishi hayo, pia kwa imani yangu kuu naamini kuwa sijafa kirahisi rahisi. Mizimu ya mababu zangu waliouwawa kifedhuli utumwani imeniambia kuwa najipumzisha ila ipo siku nitazaliwa na nitazaliwa katika damu yangu mwenyewe. Ninapumzika Majenga ila nikizaliwa tena usishangae. Naamini mizimu hii kulikoni dini walizotuletea wakoloni, dini zilizotuongopea kuwa Mungu ni mzungu, zikaenda mbali na kusema kuwa Mungu anaishi katika majengo yao waliyoyajenga.

Dini za kishenzi zilizonipatia jina la kishenzi, Frolian na kunipokonya jina la kishujaa kutoka kwa babu yangu.

Dini zilizotulaghai kuwa kila asemacho yule mzee mweupe anayesimama mbele yetu basi ni sawa, anatuona tunateseka na anasema tumwachie Mungu, nasi tukijaribu kupambana anasema tena sisi ni watu wabaya sana na hatufai kuwekwa kundi la wanadamu.

Dini zao hazijaniambia kuwa siku moja nitarejea, lakini wazee wangu ambao tuliwalilia njaa wakatusikia katika miti, tuliwaomba kila kitu na walikuwa wakweli.

Wazee hawahawa wamesema nami, acha nipumzike ila ipo siku nitarejea na sitakuwa wa kujificha tena.

Kwaheri mjukuu wangu!"

Kisha akwakeka hitimisho Majenga kwa wino mzito.

"MNAMO MWAKA 1988 BABU YETU Ngengekuzenza aliaga dunia na ni mwaka huohuo mwanaye Salama alipata kujifungua... yule mtoto akaitwa NGUZU"

_________________

NGUZU alibaini kuwa alikuwa anatetemeka baada ya kuimaliza sentensi ile ya mwisho.

Akaituliza akili yake na kutaka kumaizi ni kitu gani kimempa majibu katika maandishi yake.

Kwanza, aliamini katika mizimu na kimyakimya akakiri kuwa mzimu wa babu yake ungali ndani yake.

Pili, Jose kazeze yawezekana aliweka kisasi cha kudumu, baada ya familia yake kunyanyaswa akaisambaza ile chuki kwa wajukuu na vitukuu kama wapo.

Hivyo yawezekana mmoja kati ya kitukuu ama mjukuu alikuwa akilishambulia jina la Nguzu popote atakapokutana nalo hivyo naye alikuwa ameshambuliwa.

Mambo haya mawili yakamwacha katika sintyofahamu nyingine mpya.

Akajaribu kulitaja jina la Inspekta Kobo...... akatazama kisa chake hadi kuja kumchomea ndani ya nyumba yake.

Hili akaliweka katika mabano, yawezekana kuna watu wengine walihusika katika hili jambo.

Akayakumbuka maneno ya yule kiongozi wa waliotumwa kumkamata Majenga.

Akakumbuka kuwa yule bwana ndiye aliyemueleza juu ya Inspekta Kobo kuwa yungali rumande akituhumiwa kwa kesi mbaya kabisa inayoweza kumtokomeza uraiani, lakini alimtajia jina la kiongozi wao mkuu ambaye hata wao hawakuwahi kumwona hapo kabla.


Nguzu akafuatilia katika mitandao mbalimbali kutazama huyu mtu ni nani katika serikali ili ajue je? ana uhusiano na ukoo wa Kazeze? na kama hana uhusiano ni kitu gani anataka?

Kichwa kikamuuma alipojikuta anayo orodha kubwa sana katika kichwa chake.

Na kadri basi lilivyoikaribia ardhi ya jijini Dar es salaam,mara moyo wa Nguzu ukapiga kwa nguvu sana.

Kuna kitu alikuwa amekisahau kwa muda mrefu.


Mungu wangu! Akahamanika kutokana na hali ile ambayo ilimtokea naye asijue ni kwanini imekuwa hivyo ghafla wakati analikaribia jiji na si wakati yupo mbali?

MAJIRA YA saa saba usiku Martin Nguzu alikuwa akirandaranda katika kona mbalimbali za jiji la Dar es salaam kusaka hoteli ambayo angeweza kulala kama si kupumzika mpaka patakapokucha na kuutaza uelekeo ambao anapaswa kuanza nao.

Hakuwa na mashaka yoyote ya kuufichaficha uso wake, habari zake zilikuwa zimesambaa lakini si picha yake.

Wasambaze picha yake kwa cheo chake cha u-konstebo kwani hawana mambo mengine ya kuandika.

Alifanikiwa kupata hoteli ya bei ya wastani, akafanya malipo na kujiandikisha kwa jina batili.

Akakabidhiwa chumba.

Alipoingia na kuufunga mlango akaiwasha taa, akakiona kioo kikubwa jirani na mlango.

Akajitazama jinsi alivyokuwa, kimaumbile alijiona yungali vilevile lakini ndani ya mwili wake alijihisi yupo ngangali sana tofauti na awali.

Bila kutarajia akajikuta akimuwaza tena Zubeda.

Akiwa palepale mkabala na kioo alifikiria ule ukaribu wao jinsi ulivyokuwa ukimpa raha ya kipekee, raha iliyomfanya ajikute akimwonea wivu inspekta ambaye alisemekana kummiliki Zubeda, kuna kipindi alikuwa akitamani hata kumdhuru yule inspekta ambaye ndiye kikwazo pekee kilichokuwa kati yake na penzi la uhuru baina yake na Zubeda.

Nguzu alikuwa akitamani kumtambulisha Zubeda kwa marafiki zake kama shemeji yao, ukiachana na kuufurahisha moyo wake na pia kuuweka wazi udhibiti wake dhidi ya Zubeda,

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni