KONSTEBO NGUZU (22)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI
ILIPOISHIA...
Balaa!

Akajaribu kumshirikisha Nguzu aliyekuwa bado hoi. Nguzu hakuwa na la kuchangia.

Askari yule imara ndani kwa ndani na legelege kwa umbo la nje alitoweka mpaka chooni.

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
Huku aliweza kuona kila kitu kilivyokuwa kinaendelea nje.

Alimtua Nguzu na kumsihi anywe maji yanayotoka katika bomba ili aweze walau kupata nguvu kiasi. Wakati huo akiendelea kuilazimisha akili yake ifanye kazi kwa kasi zaidi kuhusu tukio linalokuja mbele yao, alifahamu fika kuwa hakuna namna ya kuwa salama angali mle ndani kuna maiti mbili.

Kwa namna yoyote yeye na Nguzu watayamalizia maisha yao gerezani.

Maji yalikuwa msaada mkubwa sana kwa Martin Nguzu. Hayakumfanya kuwa imara sana lakini walau macho yake yaliweza kuona na aliweza kupumua vyema kwa sababu aliweza kuyaondoa mabonge ya damu yaliyounda uzio mbele ya pua zake na kumsababisha apumue kwa mdomo badala ya kutumia pua.

"Martin, Martin!" Zubeda aliita kwa kunong'ona.

Konstebo Martin akaupokea wito ule kwa kutulia akimsikiliza.

"Askari wote wanatuzingira." alimweleza kana kwamba Nguzu alikuwa anafahamu tayari juu ya uwepo wa ugeni ule..

"Akina nani? wako wapi?"

Zubeda hakumjibu badala yake alimsaidia kunyanyuka na kisha akamwelekeza kila alichokuwa akikiona kwa nje.

Walichoka!

__________________

BAADA ya kukataa kata kata kubadili maelezo yake, amri ilitolewa ya kwenda kupekua nyumba ya inspekta Kobo ili iweze kubainika kama anayo mawasiliano yoyote aliyowahi kufanya na kikosi cha majambazi kilichoinyanyasa Shinyanga kwa wakati ule huku askari kadhaa wakiangushwa na kupoteza maisha.

Msako wa kwanza haukuzaa matunda yoyote waliyoyatarajia.

Walikata tamaa huku wakianza kuamini yawezekana kuwa inspekta Kobo aidha hajuani na lile kundi ama la ni mafia aliyefuzu mafunzo yote stahiki.

Yaani hata umkate mguu akisema sijui ni sijui. Anameza maneno yake na kuingia nayo kaburini...

Wakiwa wanakaribia kuondoka, askari mmoja akafika na kitu kipya.

Akamtupia swali Kobo.

"Hii nyumba unayoishi ni mali ya nani?"

"Binafsi." Alijibu kwa sauti iliyokata tamaa.

"Umeijenga mwaka gani na umeanza kuishi humu lini?"

"Huu ni mwaka wa kumi sasa naishi humu."

Jibu lile likamfanya askari yule afanye tabasamu hafifu kabla hajamtundika pagumu bila yeye kujua.

"Umejenga nyumba nyingine tofauti na hii?"

"Hapana!"

"Mtu akifika hapa kukutafuta na asikupate je? ni wapi zaidi anaweza kukupata?"

"Kazini kwangu."

Jibu la sasa likayafanya meno ya yule askari yaonekane kwa sababu ya kicheko kidogo.

Na hapo akayabwaga makaratasi kadhaa mbele ya maaskari wenzake na Kobo akayashuhudia.

Alikuwa ni mnyonge lakini haya yalimtia unyonge zaidi.

Mikataba!

Mikataba baina yake na mmiliki wa nyumba aliyokuwa akiishi hawara yake.


Alitamani ardhi ifunguke atumbukie humo, alijiona waziwazi kuwa alikuwa anaelekea pabaya.

Kwanza alidanganya kuwa hana makazi mengine zaidi ya hayo, pili mikataba yote aliiandikisha kwa majina yake na si ya Zubeda.

Mkataba wa mwisho aliuandikisha miezi miwili tu iliyopita.

Anakwepa vipi rungu la sheria?

Watamuhesabu kama mnyang'anyi ambaye analo eneo la siri kwa ajiri ya kufanyia shughuli zake haramu.

Inspekta Kobo akaumia zaidi kwa sababu alikuwa anakwenda kumweka Koplo Zubeda na maaskari aliowaweka kumlinda matatani.

Wote hawa watahesabika kuwa ni chama kimoja cha kimafia na wataminywa kama alivyominywa yeye hadi kufikia hapo alipo.

Akaunganisha meno yake kwa uchungu mkubwa.

"Tunaenda moja kwa moja hadi katika nyumba hii. Ukithubutu kutudanganya utajutia uongo wako" Akachimbwa mkwara, akamtazama yule bwana kwa jicho kali, akajilaumu sana kwa sababu alikuwa na pingu, vinginevyo angefanya shambulizi kwake.

Hakupendelea masuala ya kuchimbwa mkwara!

Inspekta Kobo akawaelekeza nyumba ile inapopatikana, na hata asingewaelekeza bado kuna namba ya nyumba iliorodheshwa katika ile mikataba.

Bila kusahau kiherehere cha mmiliki wa nyumba ile kuweka nambari yake sahihi kabisa ya simu ya mkononi na ile ya ofisi.

Wakatoweka kuelekea nyumbani kwa Zubeda!

ZUBEDA hakuamini macho yake pindi alipomshuhudia inspekta Kobo akishushwa garini huku akiwa hajiwezi walau kutembea, nguo yake kwa mbali kabisa ilionekana kumpwaya, na ilikuwa imefubaa huku mabakamabaka yaliyoashiria kugandiana kwa damu yalionekana.

Donge la uchungu likamkaba kooni, akajikuta yungali katika mfadhaiko mkubwa sana.

Hakujua ni kwanini Kobo yu katika hali ile lakini kichwani aliitabiri kuwa haikuwa ya heri hata kidogo.

"Martin...... Inspekta Kobo..." Alimwita kutoka pale alipokuwa ameinama bafuni.

Martin akajikuta akisimama wima na hapo akawa amejitonesha mbavu zilizokuwa katika maumivu makali.

Hakujikunja tena, akanyoosha shingo akakiona kile ambacho Zubeda alikuwa anakiona.

Mpango huu ulikuwa maridhawa kabisa.

"Hatuchomoki!" Zubeda alijikuta akitokwa na kauli ile ya kukata tamaa.

Kauli ile haikuelea sana hewani kabla mlipuko mkubwa haujasikika na palepale askari wawili walio katika sare wakaanguka chini.

Mmoja aliyekuwa amemshika Kobo ili aweze kutembea alimwachia na Kobo akatua chini mzimamzima.

Akatulia!

Hapoikazuka vita mpya, Nguzu na Zubeda wakashindwa kuelewa hii vita inahusisha pande ngapi.

Wakati wanaamini kuwa ni pande mbili pekee sasa wanashangaa kuwa wao hawahusishwi na wakati huohuo vita inaendelea.

Milio ya risasi za kuviziana ikaendelea huku askari wakipokea amri kalikali kutoka kwa kiongozi wao.

Mambo yalikuwa magumu haswa!

Asakari walikuwa wamepagawa, ni kama walikuwa hawajatarajia upinzani wa aina ile kutoka katika nyumba ile aliyokuwa akiishi Zubeda.

_______

HAKUWA katika mavazi yake yaliyowatisha wengi pindi walipomuona, hakuwa katika kiti chake cha kuzunguka huku akipokea taarifa zilizopaswa kumfikia yeye na kisha kutoa maamuzi.

Hakuwa katika nafasi yake ya kuwasiliana na raisi wa jamuhuri wa muungano.

Alikuwa katika fulana yake pamoja na bukta laini, na alikuwa chumbani kwake.

Vyeo vyote aliamua kuviweka kando.

Alichoingia nacho pale chumbani ni thamani ya urafiki.

Hakuwa na roho mbaya, na hilo alilitambua vyema bali alikuwa ni mtu anayesimamia haki na usawa.

Ukimwona ana roho mbaya kwa sababu tu amekushinda kwa kuusema ukweli basi alikuwa tayari kuonekana hivyo.

Aliijua mipaka yake vyema, hakuwa shabiki wa mateso wala vifo vya hovyohovyo.

Alikuwa na weledi wa kutosha na hii haikuwashangaza wenzake baada ya kusikia jina lake likitajwa kuwa atakuwa mkuu wa majeshi ya polisi.

Hata yeye hakushangaa, maana hakupewa cheo kile kwa bahati mbaya.

Alistahili!

Sasa alikuwa hayafikirii yote haya, alikuwa akimfikiria Kobo, ambaye alitokea kuwa rafiki yake sana mpaka mtafaruku ulivyokuja kuwaweka mbali kidogo kisha madaraka yakahakikisha wapo mbali kabisa.

Kwa kufumba ama kufumbua macho IGP hakuacha kuiona sura ya Kobo ikiitaka huruma yake, akayakumbuka maneno ya Kobo juu ya mkewe ambaye yu katika kuzimia.

"Nampenda sana mke wangu, ninapaswa kumuomba msamaha. Kama haitafaa mimi kubaki huru nakusihi rafiki yangu na mkuu wangu nifanyie upendeleo nisining'inie katika kitanzi kabla mke wangu hajazinduka."

Maneno haya yalimuumiza mno, akajaribu kuelekeza macho huku na kule ili asahau kuhusu Kobo lakini akajikuta akilitazama tukio la Kobo kujitoa muhanga na kumsukuma kando ili asipatwe na risasi iliyomkusudia.

Akajikaza hisia zisimwendeshe lakini chozi likamsaliti.

Akajikuta analia!

Akayakumbuka maneno makali ya Kobo juu yake alipomwambia kuhusu pambazuko baya kupindukia.

"Jitazame yawezekana pambazuko hili likakuandama wewe pindi utakapogundua kuwa sikuwa nyuma ya maovu haya."

IGP akasimama na kujifuta machozi pamoja na jasho lililoanza kumtoka.

Akachukua simu yake na kumpigia msaidizi wake, ambaye pia alikuwa ni rafikii yake nje ya madaraka hayo.

Akajaribu kumweleza kwa kifupi, akaeleweka na hatimaye wakachukua maamuzi ya kutuma watu watatu wa ziada katika tukio hili kutazama jinsi linavyokwenda.

Walikuwa ni vijana wanaoaminika sana kiuwezo katika mapambano na pia katika umakini.

Walau IGP aliweza kulala vyema baada ya kufanya hatua za mwisho kabisa za kutambua ikiwa Kobo anastahili jela ama la?

Majira ya saa kumi jioni alishtuliwa na simu yake ya mkononi.

Ni nambari aliyompatia msaidizi wake ili lolote litakalotokea waweze kupeana taarifa.

Akaipokea upesi ile simu.

"KIjana mmoja ameuwawa na mwingine amejeruhiwa begani." Taarifa ile ilimtisha mno IGP.

Alitambua kuwa jambo hili lina uzito lakini hakukadiria uzito ule kufikia huku kwa vijana ngangari kama wale kutetemeshwa.

Akamsihi aongeze vijana na amri iwe moja tu, warejee na majibu.

"Kiongozi kuna kitu kingine cha ziada." Alisema kisha akamwacha IGP apumue kidogo.

"Ile sauti uliyoniambia imesikika tena. 'SHUSHA MBUYU KUNA NYOKA..."

"Ni sauti ya nani?" Aliuliza kwa utulivu wa hali ya juu.

"Aliyeisikia ni marehemu tayari. Lakini ni mmoja kati ya timu uliyoipa dhamana ya kwenda kuikagua nyumba ya Kobo."

"Na ni nani anayeshambulia ikiwa sio hao wapekuzi?"

"Kuna safu nyingine kutoka katika kona za nyumba waliyoenda kuipekua. Kuna vita ya pande zaidi ya mbili mkuu."

"Ongeza vijana, fanya wanane. Wahakikishe wanaleta majibu."

"Sawa. Afande..." Alijibu na kukata simu.

Hali ilikuwa mbaya tayari.

_____

INSPEKTA KOBO alianguka mwili wote lakini hakuzimika macho yake. Alitulia kama aliyekwishapoteza uhai tayari.

Aliendelea kutazama mashambulizi yalivyokuwa ya kutisha, kuna jambo alikuwa akilisoma.

Wapinzani waliokuwa wamejificha katika kuta na dari walikuwa wakifanya mashambulizi ya akili sana huku hawa waliomsindikiza kukagua nyumba walikuwa wengi lakini bure kabisa.

Walikuwa ni watu wanaotii sheria tu, wakiambiwa waachie risasi wanamimimina hovyo bila kumaanisha kudhuru!

Akiwa palepale alizungusha macho yake huku na kule, na mara akatua katika madirisha ya nyumba ile.

Akaona kama kivuli kikivuka upesi kwa kuinama chini.

Kivuli kile alikuwa amekizoea sana, kama kisingekuwa chenyewe basi kingekuwa ni pacha ya kile alichokizoea.

Zubeda! Inspekta akatokwa na jina lile huku akiwa bado amenasa pale chini, kulia kwake pakiwa na mwili wa askari aliyetokwa na uhai tayari.

Kwa umakini wa hali ya juu akajisogeza mita kadhaa taratibu hadi akawa jirani kabisa na yule askari. Muda wote macho yake yaliwatazama wale washambuliaji waliojificha.

Alishagundua tayari kuwa washambuliaji walikuwa wanaye mdunguaji wao na alijua vyema kazi ya kudungua maana alikuwa hakosi kila akishambulia.

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni