KONSTEBO NGUZU (23)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU
ILIPOISHIA...
Kwa umakini wa hali ya juu akajisogeza mita kadhaa taratibu hadi akawa jirani kabisa na yule askari. Muda wote macho yake yaliwatazama wale washambuliaji waliojificha.

Alishagundua tayari kuwa washambuliaji walikuwa wanaye mdunguaji wao na alijua vyema kazi ya kudungua maana alikuwa hakosi kila akishambulia.

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
Faida kuu kwa Kobo ni kwamba huo ulikuwa moja kati ya mchezo wake uliompandisha cheo upesi na mchezo huohuo ulikuwa umemuingiza matatani.

Shabaha!

Kobo akainyakua silaha ya askari mfu pale chini.

Akatabasamu baada ya kuitambua kuwa ni silaha aipendayo.

Akatulia tena kama mfu huku akiangalia ni wapi anapoweza kuanza kushambulia. Alitambuwa wazi kuwa hawezi kushambulia kwa muda mrefu kabla nguvu hazijamwisha na pia kuchabangwa risasi na kupoteza maisha hivyo alihitaji akifanya shambulizi liwe kubwa na lenye maana kubwa.

Akiwa bado katika kuliandaa shambulizi aliisikia simu ya upepo jirani na lile gari waliloingia nalo pale ikiunguruma maneno kadhaa ya kusihi.

Hakuwa na uhakika kama msikilizaji wa ile simu aliamua tu asiijibu ama simu ilikuwa haina msikilizaji.

"Shusha mbuyu kuna nyoka. Shusha sasa hivi ova!"

Sauti ile ilitokea nyuma ya gari ambalo lilikuwa limeharibika vibaya kutokana na milipuko ya risasi.

Mapigo ya moyo yakaongeza kasi, umakini ukatoweka akataka kukurupuka lakini alipokumbuka kuhusu 'sniper' aliyejificha mahali fulani aliendelea kutulia.

Punde baada ya amri ile kutoka mita kadhaa hadi kuufikia ukuta mrefu kiasi ulioizunguka nyumba ile akasikia kishindo kikali, na kisha kikasikika kilio.

Kuna mwanaume alikuwa amemezeshwa risasi tayari. Alikisia

Huyu ni nani? alijiuliza kisha akajigeuza na kuilalia ile bunduki na kuendelea kubaki kana kwamba hana uhai.

Alikuwa na uhakika wote kuwa alichokisikia katika simu ni sauti ileile iliyomkosesha shabaha na utulivu mjini Shinyanga na kisha kumletea majanga.

Lakini safari hii ilisikika katika simu ya upepo. Hakufahamu fika ni nani mzungumzaji na alikuwa upande upi.

Na punde baada ya kauli ile shambulizi likafanyika.

Ni nani huyu? likabaki kuwa swali zito kwa Kobo.

Tukio la Kobo kuichukua bunduki hadi kuilalia lilikuwa likifuatiliwa vyema na mdomo wa bunduki iliyokuwa tayari kukohoa risasi.

Kobo hakujua, aliamini kuwa umakini wake ulikuwa wa kiwango cha juu zaidi.

Baada ya shambulizi lile akazisikia hatua zikisogea kwa kujiamini kuja mahali alipokuwa.

Akazivuta pumzi zake kisha akaanza kuzitoa nje taratibu kabisa.

Akakisikia kiatu kigumu kikimkanyaga mguuni.

"Huyu tayari... hamna kitu humu." bwana aliyekuwa anamkanyaga akatoa jibu lile.

"Chapa risasi kabisa kujihakikishia, hakawii kuwa hai akatuharibia." Iliamrisha sauti nyingine kwa ukali iliyotawaliwa na madaraka.

Kobo akaanza kuweweseka pale chini, alijilazimisha kuendelea kutulia kana kwamba ni mfu lakini kitendo cha kusikia kuwa anapaswa kuchapawa risasi ili kuhakikisha juu ya uzima ama kifo chake, hii ilikuwa ni sahihihi mbaya kabisa.

Kobo hakumsikia yule aliyeamriwa akijibu kitu chochote, alishindwa kuelewa nini maana ya kimya kile.

Hakutaka kucheza bahati nasibu ya 'nitakufa ama wataniacha'

Akaamua kutumia nguvu zake za mwisho na njia pekee iliyosalia katika kujitetea.

Akageuka upesi mtutu wa bunduki katika mikono yake tayari kwa kufyatua.

Lakini hakuwa na mwendokasi wake wa zamani, Kobo huyu alikuwa mgonjwa, mzito, asiyeweza kuona vyema.

Hakuwa Kobo anayetisha tena.

Inspekta Kobo alikuwa amechelewa tayari......

"Nayaweza yote kwa Imani na jitihada"

Kama alivyoona ndivyo ilivyotokea, yule bwana akafyatua risasi.

Kobo hakutarajia kama angepata nafasi ya kusikia risasi ile ikivuma pembezoni mwa sikio lake.

Lakini hivyo ndivyo ilivyokuwa.

Shabaha iliyumba malikiti.

Kobo akapata muda wa kufumbua ili atazame kama ataweza kubiringita tena ili akwepe kwa mara nyingine tena.

Akayahimiza macho yake kutazama....

Macho yakakutana na kitu cha kutisha, haikuwa risasi ya kawaida... hii ya sasa asingeweza kuikwepa asilani.

Ilikuwa pana sana, hata kama angebiringita kwa kasi kuu bado asingeweza kujinasua.

Inspekta Kobo akasalimu amri kwa kuitanguliza mikono yake kukabiliana na kitu kile kikubwa.

Kilipomkaribia zaidi akayafumba macho yake.

Kikatua juu yake, upepo ukakata!

Kobo akarejea katika ulimwengu wa waliopoteza fahamu wasijue namna ya kuzitafuta.

__________

MIILI miwili ilikuwa imebebana bila kukusudia, yote isiyojiweza na bila budi kujibweteka mwili mmoja juu ya mwingine.

Miili hii ilitazamwa kutokea mbali na vikundi viwili visivyokuwa na majina rasmi ya kuvitambulisha.

Kukosa majina hakukumaanisha ule uwepo ni batili.

"Unahisi bado anapumua yule?" Sauti dadisi ya Zubeda ilimuuliza Nguzu.

"Uhakika pekee ninaoweza kuuthibitisha ni kwamba yule bazazi nimemfyatua barabara katika chembe ya moyo wake..." Alijibu huku akiwa bado na umakini wa hali ya juu.

Kundi la pili lilikuwa katika mfadhaiko, wakati likiamini kuwa limeunyakua ushindi na kilichosalia ni kuvikwa taji mara shambulizi linatoka wasipopajua na kumsambaratisha mwenzao aliyekuwa anangojewa waweze kuondoka eneo lile.

Makundi yote mawili yalibaki katika tahadhari hakuna aliyekuwa tayari kwenda kuwatenganisha wawili wale waliolaliana.

Mmoja akiwa ni mwili na mwenza wake akiwa ni mwili na roho pamoja na fahamu zilizokwenda likizo isiyokuwa na muda maalumu.

"Martin.... bila kujalisha kama mzee Kobo atainuka ama la, bila kujali kama tutabaki hai ama la. Naomba unisamehe mimi kwa yote yaliyotokea" Sauti tulivu ya Zubeda ilipenya katika masikio ya Martin Nguzu.

Hakuitoa silaha yake katika lindo lake katika watu wale wawili waliolaliana mmoja akiwa ni Inspekta Kobo.

"Unavyozungumzia kuwa hai ama la kana kwamba ni pipi ambayo unaweza ukaamua kuimung'unga ama la na isikupunguzie lolote. Uhai unayo thamani kubwa sana usiuongelee kijuu juu hivyo" Akamjibu kwa kumnanga.

Koplo Zubeda akabaki kimya huku hatia ikimsulubu na kujiona yu mkosaji mkubwa sana.

Hakukumbuka kujiuliza ni lipi basi kosa lake?

KUTOKEA upande wa pili, tumaini la ghafla katika pori la mfadhaiko liliibuka, aliyeshuhudia akawasihi na wenzake nao waone.

"Oya...yupo hai aisee... namuona anatikisika" Alisema na kuwavuta wenzake kutazama kwa makini, kweli mwenzao alikuwa anajitikisa.

Ile hulka ya wanadamu waonapo jambo wasilolitarajia hujikuta wakiisahau misingi yao yote na kujikuta katika mkumbo wa liwalo na liwe, haikuwa upande huu badala yake ilikuwa upande wa pili.

Zubeda anayesukumwa na hatia ya kupendwa kwa dhati kisha kuja kumsaliti Inspekta Kobo na hatimaye kumweka katika kitanzi kile ilikuwa inamponza.

Konstebo Nguzu naye alihitaji sana kujua ni nini hatma ya Kobo pamoja na makundi yanayoshambulia yana nia gani.

Hakuamini hata kidogo kuwa yawezekana kabisa kuwa eti chanzo ni yeye tu hadi haya yote yanatokea.

Kama ni yeye kwanini wahukumiwe hata wasiokuwa watu wa ukoo wake?

Wakati akiwaza na kuwazua akaikumbuka sura tulivu ya Kobo iliyojaa hekima na busara siku aliyomuita na kumsihi aachane na Zubeda wake!

Huruma kuu ikamvamia.

Hali hizi ziliwafanya wasisimke walipoona ile miili pale chini ikijitikisa.

Nguzu akamuhakikishia Zubeda kuwa aliyejitikisa ni Kobo si yule hayawani aliyejaribu kumfyatua.

Zubeda hakuamini upesi, Nguzu akajitoa muhanga kwenda kumwokoa Kobo, huku nyuma shughuli ya kulinda usalama wake akaiacha mikononi mwa Zubeda.

"Kiumbe yeyote atakayejaribu kunidhuru, fyatua usifikirie mara mbilimbili. Ule muda utakaotumia kufikiri nd'o muda ambao macho yako yatakishuhudia kifo changu. Hiki cha sasa kitakuwa kifo taslimu." Nguzu alimweleza Zubeda.

Kisha akamkumbatia kwa nguvu sana, akamtazama machoni na kuzungumza kwa sauti tulivu.

"Naitwa Martin Ngengekuzenza Nguzu. Jina langu lina maana kubwa kulikoni uhai wangu... kwa lolote lile nikianguka naomba nifukiwe kwa jina hilo." Akamaliza na kumbusu Zubeda katika papi za midomo yake.

Akaondoka akimwacha Zubeda akipambana machozi yasiyazibe macho yake.

Alihisi lile ni busu na kumbatizi la mwisho kutoka kwa kijana yule machachari.

Umakini ukarejea baada ya Konstebo Nguzu kuingia ukumbi wa vita, Zubeda askari mkakamavu akaishikilia vyema silaha yake, akavuta pumzi na kushusha akajiandaa kukabili kwa lolote kama alivyoelekezwa.

Umbali wa kutoka mlangoni hadi ulipokuwa mwili wa Kobo haukuwa mita nyingi sana, lakini ilikuwa ni zaidi ya kilometa kadhaa kwa Nguzu kutokana na kutokuwa na uhakika ni wapi anaweza kuwepo adui awezaye kuitoa roho yake mara moja.

Akapiga hatua huku uoga ukishamiri katika moyo wake, alijitia ujasiri kwa maneno aliyoelezwa na mzee Majenga kuwa hatakufa kwa sababu mzimu wa babu yake unaishi naye mpaka atakapoitimiza azma yake.

Hatua takribani kama tano kabla hajaufikia ule mzoga juu ya mwili. Kilio kikubwa kikasikika kutokea katika dirisha ambalo alibaki Zubeda kama mlinzi wake wakati akielekea kumkomboa Kobo.

Upesi Nguzu akaiweka vyema silaha yake lakini hakujua ni wapi afyatue kabla hajaisikia sauti kali nyuma yake ikimwamuru kutulia kama alivyo.

Nguzu alikuwa mikononi mwa watu wabaya!

Nini kimejiri kwa Zubeda?? alibaki akijiuliza wakati huu ambapo alimuhitaji sana mwanamama yule ili kuweza kumkomboa.

Kimya! hapakuwa na shambulizi lolote la kumkomboa.

"Taratibu kabisa angusha silaha yako chini, bila kuinama walau sentimita moja" Sauti ikachimba mkwara zaidi.

Nguzu hakusubiri onyo la pili akaiachia bastola yake itue chini naye abaki na Mungu pekee kama mlinzi wake wa haja.

"Wananiua wapuuzi!" alijisemea

"Sogea mbele kwa hatua za taratibu kabisa. Bila shaka sina haja ya kukumbusha kuwa ukifanya upuuzi wowote ule hautakumbuka chanzo cha kifo chako...." sauti ile tulivu inayojiamini iloiendelea kumwongoza Nguzu.

Nguzu akatii!

Alikuwa kama hayawani ama zuzu asiyejua 'a' wala 'ba'. Kifo pekee nd'o kitu ambacho aliwaza kwa wakati huo.

"Shusha mbuyu mwamba...." Sauti tofauti na ile iliyokuwa inamwongoza ilizungumza kwa kukaripia na kuonyesha uharaka.

Mbuyu? Nguzu akajiuliza asijue ni kitu gani kimemaanishwa katika kauli ile tata.

Hakuwa tayari kuuwawa namna ile bila kuimaliza kazi yake, lakini pia hakuwa walau na akili ya ziada ya kujiokoa.

Utajiokoa vipi ungali jirani na mdomo wa bunduki usiokuwa na huruma ukifunguliwa?

"Mpigie tajiri..." Sauti iliyokuwa ya kwanza kumtetemesha Nguzu ilizungumza.

Baada ya sekunde chache, mazungumzo yalisikika upande uliosikika zaidi ulikuwa upande wa kwanza huku aliyepigiwa simu akisikika kwa mbali sana.

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni