KONSTEBO NGUZU (24)

Zephiline F Ezekiel

SEHEMU YA ISHIRINI NA NNE
ILIPOISHIA...
"Mpigie tajiri..." Sauti iliyokuwa ya kwanza kumtetemesha Nguzu ilizungumza.

Baada ya sekunde chache, mazungumzo yalisikika upande uliosikika zaidi ulikuwa upande wa kwanza huku aliyepigiwa simu akisikika kwa mbali sana.

JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈

ENDELEA...
Simu haikukatwa iliachwa hewani na hapo Nguzu akarushiwa swali.

"Unaitwa nani? na upo hapa kwa shughuli gani?"

Nguzu akafikiria kuhusu kuongopa kuhusu jina lake, lakini akachagua kucheza karata nyingine.

"Naitwa Martin, nipo hapa kwa ...."

"Martin nani?" Swali lilitupwa, hadi sasa alikuwa hajaziona nyuso za maadui zake.

"Martin Nguzu!" Akamalizia.

"Acha upuuzi, hatuna muda wa kupoteza," alijibu kwa hasira kisha akarejea katika simu yake, "Tajiri... huyu mjinga anasema anaitwa Martin Nguzu. Hana faida kwetu..."

"Naitwa Martin, Konstebo Martin Nguzu. Sijawahi kufa lakini nakijua kifo. Jaribuni kuniua mara ya pili huenda nikakijua kifo" Nguzu akapigilia hofu na utata mwingine. Alikuwa ameupata ujasiri wa hali ya juu sana.

Wale mabwana wawili hawakuelewa ni kipi anachojiamini angali hana silaha na wakiamua ni sekunde moja tu wanammaliza.

Mazungumzo katika simu yakaendelea huku akibaini sasa kuwa mpiga simu alimuhitaji akiwa hai. Lakini hilo si pekee lililomjengea ujasiri.

Kuna jambo la ziada ambalo lilihesabika kwa sekunde kadhaa kabla halijabadilika na kuwa kindumbwendumbwe!

Ilikuwa ghafla sana, Nguzu akaruka upande wa kushoto bila wale watu kumtarajia kama atafanya hivyo.

Palepale milipuko miwili ya risasi ikasikika.

Mayowe ya hofu na maumivu yakasikika.

"Usithubutu walau kujitikisa, maana nitafyatua jicho lako badala ya bega!" Sauti iliyoongea kwa tabu kabisa ilitoa maelekezo.

Bwana aliyekuwa anazungumza na simu akabaki kutulia tuli asiamini kilichokuwa kinatokea.

Inspekta Kobo kutoka katika usingizi wa kifo alikuwa amechota medali zake za ushujaa palepale chini.

Nguzu pekee ndiye aliyeutambua uhai wake, na aliamua kumuamini walipozungumza kwa ishara za macho.

Ishara ambazo ni wao pekee wangeweza kuelewana kwa sababu wamepitia mafunzo ya kijeshi.

Nguzu akajitokeza na kuiwahi ile silaha ambayo ilimponyoka yule aliyesambaratishwa na Kobo kwa shabaha moja iliyojikita katika kifua chake moja kwa moja.

"Nahitaji ujibu swali uliloniuliza hapo kabla. Ni nini unafanya hapa na unafanya kwa manufaa ya nani? Niko tofauti kidogo na wewe... sichimbi mkwara huwa natenda. Ukichelewa kunijibu nakuvunja miguu....." Nguzu akiwa anatazama na bwana yule aliyepagawa alizungumza.

Yule bwana akapagawa asiamini anaonana ana kwa ana na Kontebo Martin Nguzu ambaye wanaamini kuwa walimteketeza ndani ya nyumba.

Hakuwa na budi kujieleza vyema kabisa.

Nguzu akashtuka jina la muhusika wa haya lilipotajwa.

Lilikuwa jina refu lakini ubini wa 'KAZEZE' ukamwacha katika namna ya kupigwa butwaa.

Jina ambalo lipo katika kitabu cha babu yake, mzee Florian Ngengekuzenza Nguzu, jina lililosheheni chuki, visasi na unyanyasaji.

Jina hili linasikika tena katika maisha yake.

"Ina maana Joseph Kazeze alikiacha kisasi chake kirithiwe na watoto wake ama?" Nguzu alijikuta akiuliza kwa sauti, lakini asipate mtu sahihi wa kumjibu.

"Zu...Zubeda yupo wapi" Inspekta Kobo akiwa ameketi chini aliuliza kwa sauti ya chini sana, bila shaka alikuwa katika maumivu bado.

Swali lile likamshtua sana Nguzu, alikuwa amesahau kabisa kuwa kuna mlipuko ulikuwa umesikika kabla hajadhibitiwa na mabwana wale waliodai kuwa walikuwa wameagizwa na mkuu wa majeshi mstaafu, Jeremiah Stamford Kazeze.

Kukosa kule utulivu kukaondoka na umakini wake.

Yule mtumwa akamvamia Nguzu upesi na teke kali ambalo liliiondoa silaha yake mkononi.

Akarusha teke la pili ambalo lilielekea kupasua fuvu la kichwa cha Nguzu. Nguzu akawahi kuinama.

Wakati anajiandaa kumkabili akajikuta akikabiliana na madonge ya damu.

Kobo alikuwa amejipima tena umakini wake kama upo sawa.

"Usingemuua Inspekta..."

"Angekuua wewe.... amepitia mafunzo ambayo wewe hujawahi hata kuyaona kwenye luninga.... hata hivyo sijamuua labda aamue kufa mwenyewe tu..."

Hatimaye Inspekta alisimama kwa tabu, wakati huo Nguzu alikuwa ametangulia kwenda kuitambua hali ya afya ya Zubeda ambaye bila shaka alishambuliwa.

Hakika alikuwa amepoteza fahamu, risasi ilikuwa imemkwangua begani na kumtupa ukutani.

Halikuwa jeraha kubwa sana, hata alivyoshtuliwa kwa kumwagiwa maji ilikuwa rahisi kwake kusimama na kutambua kila kilichokuwa kinaendelea.

Kigiza kilikuwa kinaanza kuingia wakati watatu hawa wakiwa wamepata fursa ya kuwa mbali na ile nyumba na walikuwa wameweza kujadili kwa ufupi sana juu ya kisa hiki.

Hakuna aliyegusia suala la mapenzi ya kuchangia, walitazama zaidi uhai na amani yao.

Inspekta akashauri wafanye mchakato wa kuwasiliana na IGP waweze kuupata msaada wa upesi sana dhidi ya Kazeze IGP mstaafu waliyeamini fika kuwa yupo nyuma ya yote haya.

Wakati wao wanafikiria namna ya kuwasiliana na IGP.... ni wakati huohuo IGP mstaafu Kazeze alikuwa yu njiani kuelekea nyumbani kwa IGP.

JOTORIDI lilikuwa la wastani lakini hiyo ilikuwa kwa wale wenye amani pekee.

Mashaka ya mwandishi wa habari, Juma Kihwele 'kimbelembele' yalisababisha mwili wake utokwe jasho mara zote zlizokuwa akifikiria ni mbinu gani za ziada atazitumia kuweza kuipata tena amani yake na uhuru.

Hapo kabla shuleni alikuwa nguli wa kusaliti wenzake linapokuja suala la mgomo. Hakuwa mtu anayeweza kupigana, kila penye shari yeye alijiweka kando na alikuwa shahidi wa kwanza ulipohitajika ushahidi wa nani ameanzisha ugomvi.

Hali hii ilifanya walimu wampende lakini alichukiwa na wanafunzi.

Mbaya zaidi darasani alikuwa anaongoza, chukia usichukie nd'o ilibaki hivyo.

Baadhi ya wanafunzi ambao walijikuta matatani kutokana na ushahidi wa Juma Kihwele waliishia kumwekea viapo ambavyo kwa macho ya kibinadamu ilionekana wazi kuwa ni maneno ya mkosaji.

Walimweleza kuwa ipo siku atajutia uoga wake, kiherehere chake na hapohapo akili zake za darasani hazitamwokoa.

Aliishia kucheka na kuendelea kuhsika namba za juu darasani.

Baada ya miaka mingi kupita Juma amejichanganya na kujiingiza katika 'dili' alilolichukulia kuwa ni pesa nyepesi, sasa yu mikononi mwa watu ambao ili uone jino lake moja ni pale tu atakapokuwaanapiga mwayo. Kinyume na hapo zilikuwa ni ndita na lugha za ukali kila mara.

Juma Kihwele analazimishwa aelezee ana ubini gani na Martin Nguzu ambaye aliendelea kutambulika kama hayati Konstebo Martin Nguzu.

Juma alikuwa ametema kila alichokuwa anakitambua lakini bado hakuonekana kama amesema lolote, hakuwa amepigwa sana, vibao kadhaa na mateke yasiyodhamiria kuvunja lakini kipigo hicho kwa Juma alijihisi anapaswa kuorodheshwa katika kitabu cha rekodi za dunia kama mwanadamu aliyewahi kupigwa kupita wote duniani na bado anapumua.

Juma hakujua maana halisi ya kipigo.

Maelezo ya Juma Kihwele yakalileta mezani jina la Inspekta Kobo na Koplo Zubeda.

Juma akamtaja Zubeda kuwa anajihusisha kimapenzi na Inspekta Kobo na hapohapo alikuwa anajihusisha na Konstebo Nguzu.

Jibu hili likaongeza umakini kwa waliotumwa kumuhoji, majibu yakatumwa na kufika sehemu husika.

IGP Mstaafu Jeremia Kazeze akayatazama majina yale kama maadui zake, yeyote aliye karibu na Nguzu kwake alikuwa ni adui asiyefaa kuishi.

Sumu aliyomezeshwa na babu yake na kisha baba yake ilikuwa imekolea na ilikuwa muda wa kuitema.

lakini urithi si kwa magonjwa tu, hata nidhamu ya akili unaweza ukarithi.

Hayati Florian Ngengekuzenza Nguzu wakati anamsimulia Majenga kwa ajili ya kuandika kumbukumbu ya kizazi chake alimuhesabu Joseph kazeze (babu wa Jeremiah) kama mshamba anayetumia cheo chake kijinga. Ngengekuzenza alijihesabu kama mshindi kwa vita vyote dhidi ya Joseph Kazeze, na kweli alimtandika ipasavyo kwa mbinu chache tu ambazo kwa Joseph Kazeze zilikuwa ngeni na zilizosheheni suluba kubwa.

Sasa wawili hawa walikuwa wamepumzika tayari katika nyumba zao za milele.

Ngengekuzenza Nguzu akijitoa uhai kwa kujinyonga huku Joseph Kazeze akikamilisha safari yake kwa shinikizo la damu. Shinikizo lililosababishwa na mapigo kutoka kwa Ngengekuzenza Nguzu.

Chuki haikuishi katika moyo wa Konstebo Martin Nguzu na hakujua hapo kabla kuwa kuna vita mbayo haikuwahi kukamilika, lakini Jeremiah Kazeze yeye alibaki na chuki kuu.

Akafuata misingi aliyorithishwa ikiwa pamoja na mbinu za 'kikuda'za kukabiliana na adui zake.

Akavishwa cheo cha IGP na kukitumia kusulubu wowote aliodhani ni maadui.

Akamaliza muda wake huku akiwa hajakutana na jina Nguzu.

Akiwa hana cheo jina lile linamjia ghafla mezani kwake.

Vita mpya inaanza, vita mbayo haikuonekana kama inatisha.

Jeremia Kazeze anatuliza akili yake na kufikiria ni kifo gani kitamfaa zaidi Konstebo Martin Nguzu, kifo ambacho kitakuwa ni kisasi sahihi kwa yale yaliyomtokea babu yake miaka ya nyuma.

Hatimaye anamchagulia adhabu ya kuchomwa moto dunia kisha akakutane na mwingine katika safari yake nje ya dunia.

Mpango mdogo unasukwa kwa akili ileile ndogo, Nguzu anachomewa ndani ya nyumba yake.

Wakati wa utafiti wa kuzifuatilia nyendo za konstebo Nguzu. Wanapata jambo jipya, mahusiano kati ya Nguzu, Zubeda na Inspekta Kobo.

Jeremiah anachekelea na kuamua kumuuzia kesi ile Inspekta Kobo.

Oparesheni inafanyika na jalada linakaribia kufungwa.

Mwishoni mwa mchezo anatokea Juma Kimbelembele akijaribu kuandika makala juu ya yaliyotokea.

Anakuwa amenunua kesi pasi na kujua kuwa ni kesi kubwa.

Upande wa Jeremia Kazeze ukaamini fika kuwa yule bwana kuna uwezekano anafahamu ni wao wanahusika katika kuiteketeza nyumba ya Nguzu.

Upesi akaamuru kundi jingine linalomtii limfuatilie kwa ukaribu kila hatua ambayo atakuwa anapita.

Ni katika kufuatilia huku yanazuka mengine makubwa.

Sasa Juma Kimbelembele yu katika mikono yao.

Anatamani walau kupambana lakini uwezo huo hana. Amelia kama mtoto lakini haijatosha kulainisha sauti za watu wale wanaozungumza kama wauguzi wa wodi ya vichaa walioshindikana.

Kila mara wanafoka!

Ilikuwa siku nyingine tena katika mazingira yaleyale, lakini sura ngeni ilimjia.

Ilikuwa ni ngeni kwa pale ndani na sura hii ilimpa tumaini jipya kwa sababu alikuwa akiifahamu vyema.

Alikuwa ni mkuu wa jeshi la polisi mstaafu.

Jeremia Kazeze.

Juma Kihwele akajihesabia kuwa amekutana hatimaye na mtu ambaye atamuelewa na kumwokoa.

Hakujua kuwa amekutana na anayewatuma wale aliowaona kama mashetani yanayoishi.

"Haujambo?"

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi

Chapisha Maoni