NISAMEHE LATIFAH (17)

0
Mwandishi: Nyemo Chilongani

SEHEMU YA KUMI NA SABA
ILIPOISHIA...
Walipofika nje kabisa, tayari mlango wa gari moja likafika uwanjani hapo, lilikuwa lina bendera ya nchi hiyo, lilikuwa la kifahari sana. Mwanaume mmoja aliyevalia suti akawafuata na kuwaambia kwamba walitakiwa kwenda kuingia ndani ya gari lile.

“Ni gari la serikali?” aliuliza Latifa.

KUNA MATANGAZO YANATOKEA YAGUSE KILA UNAPOFUNGUA SIMULIZI ILI KUNIPA NGUVU YA KUENDELEA
INSTALL CnZ Media ILI USIPITWE NA MIENDELEZO KILA INAPOKUWA TAYARI

SASA ENDELEA...
“Ndiyo!”

“La nani?”

“Waziri Mkuu!”

“Mmmh! Mwenyewe yupo wapi?”

“Wewe twende, tutaongea mbele ya safari,” alisema mwanaume huyo, walipolifikia gari lile wakaingia ndani na kuanza kuondoka, furaha ambayo watu walikuwa nayo kipindi hicho wakaanza kulikimbiza huku wakishangalia.

“Karibu sana Latifa,” alimkaribisha mwanaume huyo aliyezungumza Kiswahili vizuri kabisa.

“Ahsante sana. Aya, nijibu sasa,” alisema Latifa.

“Nchi hii ipo kwenye matatizo sana,” alisema mwanaume yule.

“Matatizo gani?”

“Watu wanataka waziri mkuu ajiuzulu.”

“Kisa?”

“Machafuko yaliyotokea, yaani watu wana hasira naye, anaishi kwa kujifichaficha tu, kama angeonekana hata pale uwanjani, wangeweza kumuua,” alisema mwanaume yule.

“Nimekuelewa.”

Safari iliendelea mbele, walizungumza mambo mengi huku kila mmoja akimuuliza mwenzake maswali. Kila swali ambalo Latifa aliliuliza lililonekana kuwa muhimu, Dominick aliliandika kwenye notebook yake.

Hawakuchukua muda mrefu wakaingia katika jumba moja kubwa la kifahari, kwa kuliangalia kwa nje tu isingekupa wakati mgumu wa kugundua kwamba mmiliki wa jumba hilo alikuwa mmoja wa watu wenye fedha nyingi.

Gari liliposimamishwa ndani ya eneo la jumba hilo, wote watatu wakateremka. Latifa akabaki akiliangalia jumba lile la kifahari, lilikuwa moja ya majumba makubwa aliyowahi kuingia, kulikuwa na bustani nzuri ya maua, masanamu yaliyonakshiwa kwa unga wa dhahabu, kulikuwa na mbuga ndogo ya wanyama iliyokuwa imezungushiwa fensi huku ndani yake kukiwa na wanyama wachache, kulikuwa na bwawa kubwa la kuogelea, kwa kuliangalia tu, ungegundua kwamba mtu aliyekuwa akiishi ndani ya jumba hilo alikuwa mtu mwenye pesa nyingi.

Wakaingizwa ndani, kulikuwa na makochi makubwa yaliyozungushiwa vyumba vilivyokuwa na rangi ya dhahabu, kadiri Latifa na Dominick walivyokuwa wakiliangalia, bado akili yao iliwaambia kwamba mtu aliyekuwa akilimiliki jumba hilo hakuwa mtu wa mchezo kwenye mambo ya fedha.

Mara mwanaume mmoja akatokea mahali hapo, alikuwa mfupi, mwenye kitambi kikubwa, sura mbaya huku kichwani akiwa amenyoa mtindo wa kijana ujulikanao kama kiduku.

Alikuwa na umri mkubwa, kama miaka sitini lakini kwa kumwangalia, muonekano wake ulikuwa wa ujana zaidi. Alivalia fulana iliyokuwa na picha ya muimbaji wa Marekani, Jay Z, mikononi alivalia saa ya dhahabu. Miguuni, alivalia raba zilizokuwa na chata kubwa ya Nike, kwa muonekano wa harakaharaka usingeweza kugundua kama mwanaume huyo alikuwa mtu mzima.

“Karibuni sana,” aliwakaribisha huku naye akijiweka kochini.

Huyo alikuwa waziri mkuu nchini Kongo, alikuwa miongoni mwa viongozi waliochukiwa mno, machafuko yaliyokuwa yakitokea nchini humo mara kwa mara, yeye ndiye aliyekuwa akisuka mipango huku lengo lake kubwa likiwa ni kuchukua dhahabu na kuwauzia Wazungu.

Wakongo hawakumpenda, waliandamana hadharani kupinga uwepo wake nchini humo, walimchukia sana lakini hawakujua walitakiwa kufanya nini kwani kila uchaguzi mkuu ulipofika, alishinda kwa kishindo kikubwa, ila kwa kuiba kura nyingi.

“U msichana mzuri sana Latifa,” alisema bwana Nelson Savimbi huku uso wake akiupendezesha na tabasamu pana lakini uso haukubadilika, bado ulikuwa mbaya.

“Nashukuru sana.”

Walizungumza mambo mengi, Latifa aliyeonekana kuwa mchangamfu zaidi alimwambia kile kilichokuwa kimemleta nchini Kongo hivyo kuhitaji muda wa siku mbili kwa ajili ya ziara ya kutembelea hospitali za nchini humo na baadhi ya kambi za wakimbizi.

Hilo halikuwa tatizo haa kidogo, alichokifanya bwana Savimbi ni kumruhusu na hivyo kuwasiliana na wahusika na kuwaambia juu ya uwepo wa Latifa nchini humo. Baada ya kuzungumza kwa kipindi kirefu hapo ndipo walipoondoka na kuelekea katika hoteli kubwa ya nyota tano, The Bufalloes iliyokuwa katikati ya Jiji la Kinshasa.

“Nakutakia usiku mwema Latifa,” alisema Dominick.

“Ahsante! Nawe pia,” alisema Latifa na kuingia chumbani kwake.

Usiku hakulala vizuri, kichwa chke kilikuwa kikifikiria juu ya safari yake kubwa ya mafanikio aliyokuwa nayo, ilikuwa safari ndefu ambayo kwa kipindi hicho alijivunia mno kuwa hapo alipokuwa.

Hakuacha kuwakumbuka wanaume waliouumiza moyo wake, wanaume aliotokea kuwachukia kuliko wote katika dunia hii. Hakumpenda Ibrahim hata mara moja, alimchukia Liban, mwanaume wa Kihindi ambaye aliamua kumuacha kwa kuwa tu aliwasikiliza ndugu zake.

Hakutaka kujificha, alikiri kwamba kati ya watu aliokuwa akiwachukia mno basi watu hao walikuwa mstari wa juu kabisa. Usiku huo hakuacha kukumbuka kuhusu mama yake, aliambiwa kwamba mama yake aliitwa Nahra, mwanamke mrembo aliyekuwa mlevi ambaye alifukuzwa na wazazi wake mara baada ya kupewa mimba na mtu mweusi kisha kumfukuza.

Chuki yake ikaongezeka, watu aliokuwa akiwachukia wakaongezeka, pia alimchukia baba yake ambaye hakuwa akimfahamu, sababu kubwa ya kumchukia ni jinsi alivyomfukuza mama yake kisha kuingia kwenye ulevi mkubwa uliompa Ugonjwa wa UKIMWI na mwisho wa siku kufariki.

Mbali na baba yake, aliwachukia babu na bibi yake kwa upande wa mama kwa kitendo chao cha kumfukuza mama yake kisa tu alizaa na baba yake. Moyo wake ulimuuma mno ila wakati mwingine alibaki akimshukuru Mungu kwa kuamini kwamba isingekuwa hivyo, inawezekana leo hii asingekuwa hapo alipokuwa.

Siku iliyofuata, akajiandaa tayari kwa kuanza safari ya kuelekea katika hospitali mbalimbali, alipomaliza kujiandaa, akatoka nje ambapo akakutana na Dominick akiwa tayari nje, alipomuona, tabasamu pana likajengeka usoni mwake.

Hotelini hapo kulikuwa na ulinzi mkubwa, polisi walikuwa wakizunguka huku na kule kuhakikisha kwamba ulinzi unakuwa mkubwa na wa kutosha. Japokuwa Latifa hakupendwa kulindwa na silaha lakini hakuwa na jinsi, alikubaliana na kila kitu.

Wakaondoka na kuelekea katika Hospitali ya Mobutu. Idadi kubwa ya watu ilikuwa hospitalini hapo, waandishi wa habari kutoka katika vyombo mbalimbali vya habari walikuwa mahali hapo kwa ajili ya Latifa tu.

Gari lile lililombeba yeye na Dominick liliposimama, wakatoka nje, waandishi wakawasogelea na kuanza kuwapiga picha. Latifa aliachia tabasamu pana, akashindwa kuvumilia, akajikuta akibubujikwa na machozi ya furaha, akaanza kuwapungia mikono watu hao.

Alichokikuta ndani ya hospitali hiyo kilimliza, hospitali ilikuwa chafu, huduma mbovu, wagonjwa walirundikana kila chumba, hakukuwa na mpangilio wowote ule. Kila aliyezungumza naye, walimwambia wazi kwamba huduma ilikuwa mbovu hivyo waliiomba serikali iweze kuwasaidia kudumia huduma na si kula hela na kuuza madini kiholela.

“Nitawasaidia kufikisha kilio chenu,” alisema Latifa.

Ziara ya siku mbili ikafanyika kwa mafaniko makubwa, walipomaliza wakaanza safari ya kuelekea nchini Tanzania katika Mkoa wa Kigoma. Walipofika huko, wakachukuliwa na kupelekwa katika Hoteli ya Hiltop na kuchukua vyumba humo. Kama ilivyokuwa sehemu nyingine, hata huko pia watu wengi walitamani kumuona msichana huyo mdogo mwenye mafanikio na hatimaye kuwa bilionea mkubwa akiwa na umri mdogo tu.

Waandishi wa habari na watu wengine walikusanyika katika Hoteli ya Hiltop kwa ajili ya kumuona Latifa ambaye wala hakuwa na hiyana, akaonana na watu hao kwa kukaa nao sehemu fulani kisha kuanza kuzungumza nao, walikuwa kama hamsini hivi.

“Unajisikiaje kuwa Latifa?” aliuliza mwanamke mmoja.

“Najisikia kawaida, ila najiona kuwa na thamani, hiki ndicho nilichokitaka, nitambulike mimi ni nani na nina mchango gani katika jamii,” alijibu Latifa huku akiachia tabasamu.

“Na huyo ni nani? Shemeji yetu?” aliuliza mwandishi mmoja.

“Nani? Huyu? Huyu ni rafiki yangu, anaitwa Dominick, nilikuwa naye tangu Senegal,” alijibu Latifa huku akichia tabasamu pana.

“Mnapendeza kuwa pamoja, kama wapendanao,” alisema mwandishi mwingine, akawasogelea na kuwapiga picha.

Maneno yale kama yakawa yameibua kitu fulani moyoni mwa Latifa, akauhisi moyo wake ukiingiwa na kitu cha tofauti kabisa, kitu alichokuwa nacho kipindi cha nyuma mara baada ya kuisoma barua aliyoandikiwa na Ibrahim.

Alipomwangalia Dominick, mvulana huyu aliachia tabasamu pana, kitu ambacho hata yeye mwenye hakujua kilikuwa nini, akaona kuwa mwanaume mzuri mno, akahisi kuanza kumpenda.

Maswali yaliendelea zaidi, Latifa aliwajibu wote lakini kichwa chake kiliingia katika fikra nyingine kabisa, alikuwa akimfikiria huyo Dominick aliyekuwa bize akiandika. Mara baada ya kumaliza mahojiano, wakaimama na kuelekea ndani.

“Dominick…” aliita Latifa, mwanaume huyo akamsogelea na kusimama karibu yake, walikuwa koridoni katika ghorofa ya tano hotelini.

“Naaam..” aliitikia Dominick huku akimwangalia Latifa, walikuwa karibukaribu mno.

“Au basi…” alisema Latifa, akageuka na kuingia chumbani.

Kichwa chake kikaanza kusumbuka, yule Dominick ambaye alimwambia wazi kwamba hakutaka siku amwambie kwamba alikuwa akimpenda, leo hii alijikuta akianza kumfikiria, mapenzi yakaanza kuchomoza moyoni mwake.

Usiku hakulala, alibaki akimfikiria mwanaume huyo tu. Kitandani, ni mawazojuu ya Dominick ndiyo yalikuwa yakimsumbua kila wakati. Hakujua afanye nini, hakujua kama lingekuwa jambo la kawaida kumwambia mwanaume huyo kwamba alimpenda.

“Dominick…These feelings have to stop right now, I can’t bear them,” (Dominick…hisia hizi zinatakiwa kutoka sasa, siwezi kuzibeba) alisema Latifa huku akibimbirikabimbirika kitandani pale.

Alibaki na mawazo mpaka ilipofika saa nane usiku ndipo alipopatwa na usingizi. Alipoamka asubuhi, akajiandaa na kutoka nje ambapo baada ya kumuona Dominick, akajikuta akishtuka na moyo wake ukidunda kwa nguvu.

“Umeamka salama?” aliuliza Dominick huku akitoa tabasamu lilimvuruga kabisa Latifa.

“Nimeamka salama, wewe?”

“Hata mimi nipo poa.”

Siku hiyo safari ilikuwa ni kwenda katika Hospitali ya Mkoa ya Maweni na hospitali nyingine hapo Kigoma, kote huko, watu walikuwa wakijazana na kumwangalia Latifa, kila aliyemuona hakutaka kuamini kama msichana yule alikuwa Mtanzania kama walivyokuwa.

Wagonjwa wakafarijika, maneno aliyokuwa akiyazungumza msichana huyo yakawatia nguvu na kujiona wakiingiwa na nguvu za kusonga mbele. Baada ya siku nzima ya kuwatembelea wagonjwa, siku iliyofuata ilikuwa ni zamu ya kwenda katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu.

Huko, Latifa alijikuta akibubujikwa na machozi, hakuamini kama kulikuwa na watu waliokuwa wakipitia mateso makubwa kama alivyokuwa watu hao. Wengi walikuwa wagonjwa, madaktari walikuwepo kwa ajili ya kuwahudumia lakini kutokana na idadi ya wakimbizi kuwa wengi, hata wale madaktari walionekana kuwa wachache.

USIKOSE SEHEMU IYOFUATA

Bonyeza Matangazo Kila Unapoyaona ili Kunipa Nguvu ya Kuendeleza Simulizi

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)