
Mtunzi: George Iron Mosenya
SEHEMU YA KUMI NA SITA
ILIPOISHIA...
ILIPOISHIA...
Maelezo aliyokuwa ameyatoa waliosikiliza hayakuwakuna kabisa na hivyo wakaona suluhu ni kumbana vyema kwa kumuumiza ili aweze kutapika siri zote alizomeza.
"Inspekta Kobo, hili ni agizo la mwisho kabisa la kukubembeleza wewe kusema ukweli wote ili ubaki kuwa salama ama la tutatumia nguvu.
JE UNAISOMA SIMULIZI HII NJE YA APP YA CnZ Media?
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
IPAKUE ILI KUPATA MWENDELEZO KWA WAKATI
👉GUSA HAPA KU-INSTALL👈
ENDELEA...
Na hatushindwi!" Sauti ya kusihi iliyojaa madaraka iliunguruma.
Inspekta akastaajabu, hawa mabwana tayari walikuwa wameitengua taya yake, wakaupoteza njia mguu wake na sasa yungali mahututi katika bahari ya maumivu, sasa anaelezwa kuwa asiposema ukweli watatumia nguvu.
Nguvu! alistaajabu...
Nguvu gani zaidi ama watamkaliza katika kiti chenye shoti ya umeme, au watampiga risasi?
Hizi nd'o nguvu ambazo walikuwa hawajatumia.
"Mkuu nilichokiandika katika maelezo yangu ni hicho hicho sijaongopa hata nikishtuliwa usiku wa manane siwezi kupindisha ukweli huo." Alijibu kwa shida sana.
"Kama uliweza kupindisha shabaha yako maksudi na kumwacha hai jambazi mkorofi ambaye tumehangaika miaka nenda miaka rudi kumsaka unashindwa vipi kuupindisha ukweli?" Alihoji kisha akasimama wima na kuendelea kuzungumza.
"Kobo, katika maisha yako ya kulenga shabaha umeangusha mibuyu mingapi iliyoleta ukorofi?"
"Mingi sana afande." alijibu kwa sauti ya chini.
"Umetunukiwa shani ngapi kutokana na kulenga kwako shabaha?"
"Tano afande."
"Unaikumbuka shabaha yako ngumu kupita zote?"
"Ahh! mmh! ndio afande, ni ile ya kutoka ghorofa moja kwenda nyingine." aliendelea kujibu upesiupesi. Bila kujua nini hatma ya maswali yale.
"Unaukumbuka umbali kimakadirio?"
"Mita mia tano...." alijibu kwa utulivu. Na safari hii sauti ilikuwa chini zaidi kwa sababu aliijua nia ya maswali yale.
"Yaani nusu kilometa sivyo? Na haukuwa katika utulivu wowote, na uliweza kuipata ile shabaha bila kukosa. Na ilikuwa ni usiku..... halafu leo hii unapiga risasi tatu maksudi unamkosa adui anayetikisa taifa. Kobo! Kwa kitendo chako hicho cha kumuacha adui wa taifa unadhani watanzania wapo radhi kukusamehe? Mimi kama mtanzania siwezi kukusamehe... nastaajabu wanakuchelewesha nini kukutia kitanzi bazazi wewe.... uliyechagua kumlinda mwanaharamu mwenzako!" Sasa alikuwa amewaka yule bwana aliyekuwa anamuhoji Inspekta Kobo. Na alikuwa anatetemeka mno.
Inspekta alikuwa amekamatwa pabaya.
"Ok! unalipwa shilingi ngapi kila anapofanya uhalifu wake.... tuzungumze kama wanaume na haya mambo yaishe. Maana Tanzania mambo ya kitanzi tulishayafuta, na hata ukifungwa maisha huyo mwanaharamu atakuja kukutoa tu utakuwa huru. Haya nieleze tu, unapewa kiasi gani kulisaliti jeshi la polisi katika oparesheni kabambe namna ile." Swali likatupwa.
Inspekta Kobo akafadhaika mno, kwa sababu hakuwa kama walivyodhania.
Alipojaribu kupinga, hasira za yule bwana zikamuangukia.
Akapokea teke kali katika shingo yake, akarushwa na kutua pembeni akabaki kukoroma huku damu ikimtoka puani.
Akatamani kuelezea ukweli wa kila jambo lakini hakuona kama ataeleweka maana katika maandishi yake hakuandika kuhusu mashaka yake juu ya ile sauti inayotamka 'ANGUSHA MBUYU'. Hakuandika kuhusiana na kifo cha utata cha Martin Nguzu na hakugusia hata kidogo juu ya mahusiano baina yake na koplo Zubeda.
Angeanza kuelezea hayo angeonekana ni muongo mara mia zaidi ya alivyochukuliwa awali.
Inspekta akaamua kubaki kimya.
"Inspekta Kobo hivi unajua kuwa hii kesi yako inaweza kuhesabiwa kama kesi ya uhaini na itakuweka pabaya wewe na familia yako, ama unajitazama wewe na masilahi yako pekee hauitazamani familia yako. Haumtazami mkeo ambaye hadi sasa hajui kinachoendelea ulimwenguni, hujali kuhusu watoto wako unajitazama wewe pekee. Sasa mimi nimekusihi sana imetosha naandika ripoti tusilaumiane katika hili." Alizungumza kwa sauti tulivu kabisa huku akiwa anamtazama Inspekta Kobo.
Maneno yale juu ya familia yake yalimvuruga Kobo aliyejitambua wazi kuwa hana kosa lolote lile, lakini la kufanya nd'o hakuwa nalo.
Akarejeshwa katika chumba alichokuwa anafungiwa mle akiwa peke yake.
Tofauti na siku nyingine ambapo chumba hiki kilikuwa kinazimwa mwanga wa taa na kubaki katika giza siku hii kilikuwa kina mwanga na zaidi kiliongezeka kiti.
Nanyongwa!!
Hisia zikakipiga kichwa cha inspekta Kobo, tumbo likaanza kuunguruma kwa hofu ya kuupoteza uhai wake.
Akaingizwa pale chumbani.
Kimya kikatanda kwa dakika zisizopungua tatu. Kisha zikasikika hatua zikijongea katika kile chumba.
Mlango ukafunguliwa na askari wawili, kisha kwa mwendo wa taratibu akaingia Inspekta jenerali wa polisi (IGP).
Mwili wa inspekta Kobo ukaingiwa na ubaridi mkali sana, akaunyanyua uso wake na kumtazama bwana yule nadhifu kabisa aliyekuwa katika mavazi yake ya kazi.
"Funga mlango!" akawaamuru wale askari.
Wakatii! kisha wakaondoka na kuliacha eneo lile likiwa na watu wawili pekee.
Mwili wa Kobo ulikuwa umesulubika sana, lakini kwa kumtazama bwana huyu mwili ukajiona kuwa inayokuja nd'o suluba taslimu.
Kobo alitambua kuwa IGP aliisubiri hii nafasi kwa hamu sana ili aweze kumnyoosha na sasa alikuwa ameipata. Iwe isiwe atamwadabisha.
"K" IGP akaita kwa upole.
Inspekta akamtazama kisha akaitika kwa shida sana.
"Pole sana rafiki yangu. Pole!" IGP aliketi vyema.
Unafiki! Kobo akajisemea.
"Kabla sijazungumza mengi na wewe ninapenda kukueleza kuwa ninakupenda sana rafiki yangu, huwezi kuamini haya lakini elewa kuwa nimejaribu zaidi ya mara tano kuonana na wewe lakini nimeshindwa kwa sababu sikuwa tayari kukuona katika hali hii. Umeteseka sana K" alizungumza kwa hisia IGP.
Hali hii ilimtisha Kobo, akajiuliza anachokisikia ni sahihi ama kuna namna ya ulaghai.
Yaani huyu bwana ajisikie vibaya kwa yeye kuwa katika wakati ule mgumu.
Haiwezekani.
Inspekta Kobo akakumbuka vitisho vyote alivyowahi kupewa na IGP wakati huo akiwa hajapewa dhamana hii ya juu katika jeshi la polisi.
"K, yale yote yalikwisha kwa upande wangu. Nimetafiti sana na nikagundua kuwa wewe haukuwa chanzo cha mke wangu kuwa mlemavu. Niliumia sana awali na kujikuta nikikuchukia lakini nimeikubali hiyo hali na nipo hapa kwa ajili ya kukusaidia tu! Tafadhali sema nami"
"Niliyoyasema ni hayohayo." Akajibu kwa ukaidi Kobo, bado alikuwa na hisia za chuki dhidi ya IGP bado hakuamini kuwa wao ni marafiki tena.
"K, sikiliza ndugu yangu. Ukaidi hautasaidia kitu chochote kwa wakati huu. Laiti kama ningekuwa juu ya sheria ningeamuru uachiwe huru na ubaki kujuta na nafsi yako ikiwa ni kweli umefanya yote hayo ama la. Lakini kwa hili mimi sina ninalazimika kuiheshimu sheria ya nchi, sio kuivunja kisa ninakuonea huruma. K, tafadhali nieleze ni nini kilitokea...." IGP alizungumza kiukarimu kabisa.
Inspekta Kobo akaamua kurusha karata yake ya kwanza. Akaelezea kwa ufupi sakata la Nguzu, hakulitaja jina la mwanamke ambaye alikuwa anahusika.
Akaitaja ile sauti ambayo aliisikia usiku wa tukio la Nguzu kuchomewa ndani na kisha akaitaja tena sauti ileile ilisikika siku ambayo alikuwa ameishika bunduki yake tayari kwa kufanya shambulizi.
"Nikapagawa sana kugundua kuwa licha ya kwamba nimelenga shabaha kwa ajili ya kummaliza adui ila ndani yetu pia kuna adui. Tena adui asiyekuwa na huruma aliyeiteketeza kwa moto nyumba ya askari mwenzetu pasi na huruma kabisa. Nilitetemeka sana, hata lile agizo alilonipa la kuushusha mbuyu lilinikwaza badala ya kunihamasisha. Hakika nilikuwa natetemeka..."Alimalizia.
Palepale IGP akamsogelea na kumnong'oneza jambo kwa kusihi.
"Usiyaseme maneno haya popote pale. Umeniamini mimi imetosha sana na ninakuahidi italeta manufaa. Nimeupata mwanga."
IGP akatulia kidogo kisha akarusha suala jipya kabisa ambalo lilikuwa jipya kwa inspekta Kobo.
"Umesema juu ya Nguzu kuchomewa ndani ya nyumba yake, unadai ulienda kuzungumza naye usiku ule. Sawa kabisa.... na je Majenga unamfahamu vipi?"
"Ma nani?"
"Majenga" Aklajibu IGP huku akimtazama kwa ukaribu kabisa inspekta Kobo.
"Sijawahi kulisikia jina hili katika maisha yangu."
"K, mbona hutaki kuamini kuwa ningali upande wako? nieleze nijue ni wapi nakusaidia rafiki yangu. Ujue kuna watu watatu wameuwawa huko Shinyanga na huu mlolongo wote unakuangukia wewe. Ndugu zao wamechachamaa si kidogo, huyo Majenga ni nani Kobo! Tell me..." alianza kupandwa na ghadhabu IGP.
"Simjui na sijawahi kulisikia jina hilo Gervas, mbona unanilazimisha kutema maneno ambayo akili yangu haijawahi kuyameza. Simjui huyo Majenga for God's sake!!" Aling'aka inspekta Kobo huku akimtaja IGP kwa jina lake.
IGP akaanza kufura kwa hasira, akajitahidi kujiweka katika hali ya kawaida. Akauliza tena na tena bila majibu kubadilika.
Inspekta Kobo akasimamia analoliamini!
IGP akamtazama kwa sekunde kadhaa, akatoa kitambaa chake mfukoni na kujipangusa matone ya jasho na mwisho akamtupia Kobo neno la mwisho.
"Pambazuko hili litakuwa baya sana kwako na sitakuwa na namna ya kukusaidia. Nimejaribu sana Kobo nawe umeona. Umekataa kumtaja Majenga na unamjua waziwazi...."
Akasubiri kidogo, Kobo akamtazama kisha akalazimisha tabasamu na kisha akazungumza.
"Nimekuwa na mapambazuko mabaya sana tangu mke wangu apate janga lile, nimekuwa na mapambazuko mengine mabaya tangu vijana wako, vijana niliowafundisha ukakamavu jeshini walipougawana mwili wangu na kufanya kwa vitendo yale niliyowafundisha, mapambazuko mabaya hayataanza leo ama kesho yalianza tangu uliponituhumu kuwa nimeshiriki kumfanya mkeo awe mlemavu wa miguu angali nilijaribu kadri ya uwezo kuokoa maisha yake, niliokoa maisha yako pia Gervas kwa kukusukuma ili usipigwe risasi, nikawa na mapambazuko mabaya ulipozisahau fadhila zangu, ni pambazuko gani baya zaidi unaloniahidi sasa... eeh! pambazuko gani unalolisema, pambazuko la kupoteza uhai? Kuteswa? Kufungwa gerezani maisha yangu yote? Hakuna pambazuko la ajabu hata moja kati ya hayo, ni wewe utayaishi mapambazuko ya ajabu siku utakapoujua ukweli angali nimenyamaza katika kile kimya cha milele, Attaccati a sto cazzo."
akaweka kituo huku akimalizia kwa kutokwa na lile tusi lake murua katika lugha ya kiitaliano.
IGP akabaki kuganda, midomo ikimchezacheza asijue ni maamuzi gani ayachukue.
Akatoweka pale na kwenda nyuma ya mlango. Akajibanza pale na machozi yakaijua njia yake, yakayalowanisha mashavu, kamasi nyepesi zikatoka kuchungulia nini kinaendelea katika uso wa IGP.
IGP alikuwa analia kiume!
_____
Majira ya saa sita usiku aligutuka kutoka usingizi huku jasho likimtoka sana.
Majenga! jina hili likakivamia kichwa chake, akaketi kitako na kuanza kukumbuka juu ya maneno yale aliyokuwa akiyasoma yule mzee.
USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA
Share CnZ Media App kwa Wapenzi wa Kusoma Simulizi Ili Tuwe Wasomaji Wengi