
Mtunzi: Ibrahim Gama
SEHEMU YA KWANZA
ILIPOISHIA...
ILIPOISHIA...
Ilikuwa ni Jumapili moja tulivu, majira ya asubuhi. Gereza la keko lilikuwa katika pilikapilika, kama ilivyo kawaida yake katika siku za mwisho wa wiki! Watu walikuwa wengi sana wanaandikisha majina yao, na majina ya ndugu na jamaa zao waliokwenda kuwatembelea katika Gereza lile. Karatasi zilizojaa majina zinapelekwa ndani Gerezani, ili kuitwa majina ya watu walioandikishwa na jamaa zao pale nje, iwe ni Mahabusu au Wafungwa. Nani lazima uandikishwe jina lako, jina la Mahabusu au Mfungwa uliemtembelea, sehemu unayotoka, na uhusiano uliopo baina yako na mtu uliemtembelea.
“Oyaa hapa watakaoingia ni wale watu waliokuja, na vitu vya kuwaletea ndugu na jamaa zenu, kama hujaja na chakula, au chochote, duka letu lile palee mkanunue”.
“pia sehemu yakuongelea na jamaa zenu ni ndogo, haitoshi kuingia watu wengi kwa wakati mmoja. Hivyo mtaingia watu kumikumi, kufuatana na namba za majina ya karatasi mlioandikishwa!”
Ilikuwa ni sauti ya askari magereza iliyokuwa inawafahamisha wale wageni waliokwenda katika Gereza la Keko Jijini Dar es salaam.
Upande mmoja wa eneo lile, alikuwa amesimama Dada mmoja mwembamba, mrefu wa wastani akiwa amembeba mtoto mdogo mgongoni wa takribani miaka mitatu au minne hivi. Mkononi mwake dada yule alikuwa amebeba kikapu,chenye vyombo ndani yake vilivyowekwa chakula, alikuwa muda mrefu amekosa furaha, sura yake ilitawaliwa na simanzi kubwa. Alikuwa amezama katika lindi la mawazo!
IKIWA UNASOMA SIMULIZI NJE YA APP YA CnZ Media IPAKUE ILI USIPITWE NA SIMULIZI
ENDELEA...
“Wee sikiliza hiyoo, haina kurudia hii, naita majina ya ndugu zenu walioitika majina yao huko ndani,kama hukusikia jina la ndugu au jamaa yako katika karatasi hii namba moja, na wewe umeandikisha katika karatasi hii na zingine zitakazofata. Basi ujue ndugu yako hayupo katika Gereza letu.” Ilikuwa sauti ya askari Magereza iliyokuwa katika lafudhi ya luhga ya watu wa Jela, ikiwataka wageni kuwa makini katika kusikiliza. Kisha akaanza kuita majina yale aliyokuwa nayo mkononi mwake, moja baada ya jingine, hadi jina la kumi akamaliza kwa kulitaja jina la MWADUGA DINGO.
“Haya aliesikia jina la ndugu yake anifate, ili akaongee na ndugu yake, na kama hukusikia jina la ndugu yako, basi huenda akawa katika Gereza la Segerea au Ukonga, nendeni huko mtawapata.”
Alimaliza kusoma majina na kutoa ufafanuzi askari yule, kisha akaongoza mbele huku akifatwa na kundi la watu kumi nyuma yake, kwenda kuwaona ndugu na jamaa zao, waliopo Mahabusu, na waliofungwa katika Gereza lile la Keko.
“Wee Dada unaitwa nani na kwa nini umekuja na mtoto mdogo huku? haturuhusu watoto wadogo kuletwa magerezani, kwani mtakuja kutuletea vilio tu huku!” Ilikuwa ni sauti ya askari magereza aliekuwa akimuhoji yule Dada aliekuwa amembeba mtoto mgongoni, ambae muda mwingi alikuwa katika simanzi.
“Mimi naitwa Eshe Muhidini, Mume wangu Mwaduga Dingo yupo humu Gerezani, nami sina mtu wa kumuachia mwanangu, ingawa pia nilikuwa sitambui kama watoto hawaruhusiwi kuja nao huku!”
“Haya leo nakuruhusu uongee na mumeo, ila siku nyingine usije na mtoto Gerezani, sawa?”
Eshe aliitikia kwa kuinua kichwa lakini hakufungua mdomo wake kumjibu yule askari, akapiga hatua moja kubwa kuingia ndani ya mlango mkubwa wa magereza, na akaonana uso kwa uso na mumewe Mwaduga Dingo, aliekuwa upande wa ndani, na yeye Eshe akiwa upande mwingine, wakitenganishwa na bomba za chuma, zilizojengwa maalum, bila shaka kwa ndugu jamaa kuonana na ndugu zao waliokuwa ndani katika gereza lile, kama Mahabusu au Wafungwa.
“Tunatoa dakika mbilimbili kuongea na kumkabidhi kitu au chakula ndugu yako uliekuja kumuona, kwani nje huko kuna kundi la watu wengi nao pia wanataka kuja kuwaona ndugu zao.”
“Pia kitu chochote unachotaka kumpa mahabusu au mfungwa, lazima umpe askari, akikague kwanza,kisha askari atamkabidhi muhusika.”
“Na ikiwa umeleta chakula, lazima uonje kwanza ndiyo tumpe mlengwa. Ila mliokuja kuwaona wafungwa, hao hawaruhusiwi kupewa chakula cha nyumbani, wala nguo za kiraia, hawa ni watu wetu washakubali, hivyo wanakula chakula cha jela hadi kifungo chao kitakapomalizika, sambamba na kuvaa sare za kifungwa. Isipokuwa maji, sabuni, mafuta, mswaki, dawa ya meno, na nyembe ruksa kuwapa.”
Ilikuwa sauti ya askari wa zamu, alikuwa akitoa taratibu za lazima katika sheria za Magereza.
Eshe alisogea karibu, na zile bomba, huku akibubujikwa na machozi, na kumwambia mumewe,
“Pole mume wangu, kuwa na subira mungu atakujaalia, utatoka tu ili tuje tumlee mtoto sote.”
“Asante mke wangu, nawe pia kuwa na subira, kwani mimi najua siku ya kuingia humu gerezani, sijui lini nitatoka.”
Mwaduga Dingo aliposema maneno hayo, akashindwa kujizuia akaanza kulia, kwani mwanae alikuwa anataka kutoka katika mgongo wa mama yake alipobebwa, akitaka kwenda kwa baba yake.
“Haya ndiyo maana sisi haturuhusu watoto kuingia nao humu ndani kwani yanamuumiza huyu aliyoko ndani, umeona sasa mama mtoto ee?!”
Yule askari magereza, alimkaripia Eshe Muhidini kwani sasa kulikuwa ni kilio kutoka kwake, kwa mwanae, na kwa baba mtoto.
Mwaduga alifuta machozi, akaingiza mkono mfukoni mwake mwa suruali, akatoa barua na kumkabidhi askari wa zamu aliekuwa makini katika kuangalia kila kinachotoka, na kuingia katika vile vitu walivyokuja navyo wageni, kuwaletea ndugu zao.
“Afande naomba hii barua umpe mke wangu, anipelekee maskani, akawape madereva wa taxi wenzangu.”
Mwaduga alinyoosha mkono wake wenye barua, akamkabidhi Yule afisa wa zamu, nae Yule askari aliipokea, akaifungua na kuisoma. Baada ya kujilidhisha kuwa ile barua haina madhara kwa usalama wa Gereza, Yule askari afisa wa zamu, alimuangalia Mwaduga usoni, na Mwaduga nae akamkazia macho Yule askari, kwa sekunde kadhaa. Kisha Yule askari, akamkabidhi ile barua mke wa Mwaduga.
Eshe aliipokea ile barua huku bado machozi yakimbubujika machoni mwake, midomo yake ikitetemeka na kugongana mithili ya mgonjwa mwenye homa kali.
“Haya muda wenu umekwisha, na wenzenu nao, wanataka kuingia.”
Yule askari wa zamu alitoa amri, ya watu kutoka nje, na Mwaguga aligeuka huku akibeba chakula, na vitu alivyoletewa na mkewe,akirudi ndani ya gereza, huku nyuma mkewe Eshe binti Muhidini, sasa akaangua kilio kwa sauti ya juu, na mwanae pia akimlilia baba yake, akawa analombokeza, katika huzuni iliyotawala katika familia yao, kwa ghafla!
Mwaduga akasimama huku nae akilia,akamwambia mkewe kwa sauti ya huzuni na unyonge.
“Nyamaza kulia, muangalie mtoto, pia hakikisha hiyo barua unawapelekea jamaa kijiweni, niombee dua mke wangu nita…………!”
Mwaduga alishindwa kumalizia kalima aliyoikusudia, kwani mkewe, Eshe alitolewa nje na mlango ukafungwa!
Eshe aliondoshwa pale baada ya muda uliowekwa wa watu wa awamu ya kwanza kumalizika, huku akiwa mnyonge na mwanae akiwa anamlilia baba yake, huku akiwa anataka kuchomoka mgongoni ili aende kwa baba yake, Eshe alimdhibiti mwanae huku na yeye machozi yakimtoka. Mwaduga alikuwa katika wakati mgumu sana, kumuona mtoto wake wa pekee anataabika namna ile.
Eshe alitoka nje ya eneo la magereza, huku akiwa analia kwa kwikwi. Akaivuta kanga yake akawa anaifutia machozi, akawa analia huku anatembea hadi nje ya eneo la Magereza. Mara akatokea Dada mmoja, akamfuata Eshe pale alipokuwa. Kwani sasa alikuwa ameegemea kiambaza cha nyumba moja, iliyozungushiwa mabati inayoendelea na ujenzi, na kumuuliza “kulikoni?!”
Eshe akamfahamisha kuhusu barua aliyopewa na mumewe ambaye ni mahabusu, akimtaka awapelekee madereva Taxi ili wamfatilie, kitu ambacho kinamliza Eshe na kuona kuwa hakitamsaidia mumewe kutoka. Kwani tokea mumewe apatwe na matatizo, hajamuona Dereva wa Taxi yoyote kuwa Karibu nae, isipokuwa wakitokea kukutana njiani kila mmoja hujitia anaguswa sana!
“Pia hatuna pesa yakuweka Wakili, hivyo mimi na mtoto wangu tunaishi katika mazingira magumu. Kwani hata wazazi wetu wapo mbali,wanaishi Tanga mpakani na Mombasa”.
Eshe alimwambia yule Dada msamalia.
Yule dada akamuhurumia sana Eshe na mwanae, na kumpa pole huku akifikiri, aliingiza mkono mfukoni na kutoa simu. Alibonyeza namba kadhaa na kuiweka sikioni.
“Wee usiniambie! yaani jumaapili yote hii upo kazini!?” Yule dada alizungumza na mtu aliekuwa anawasiliana nae.
“Sawa sasa naomba nisaidie jambo moja, kuna dada mmoja hapa ninae, ninamuelekeza aje kwako, tafadhali naomba umsaidie kadiri ya uwezo wako”.
Baada ya kusema hayo, yule dada akakata simu, Kisha akamuelekeza Eshe aende kwa mtu alietoka kuongea nae muda si mrefu, akampa na pesa kiasi cha shilingi elfu mbili, ili afanye nauli.
Eshe akamshukuru yule dada mwenye machozi mateke, na kuelekea sehemu aliyoelekezwa aende akiwa na barua yake mkononi.
Eshe akiwa na mwanae mgongoni, ambae sasa alikuwa amelala baada ya kilio cha kufa mtu! Alitembea hadi katika kituo kiitwacho TAMECO, akasubiri daladala zinazokwenda posta, na haikuchukua muda mrefu, ikaja gari inayofanya safari zake TANDIKA, POSTA akapanda.
*******
Eshe alikuwa yupo wizara ya mambo ya ndani ya nchi, pale maeneo ya Posta mpya. Akitazamana na Dada mmoja mwenye sifa zote za kuitwa mrembo. Kule uani mwa jengo lile, kwenye ofisi za mbao. usingeweza kabisa kuamini kuwa yule dada angeweza kuwa askari, kwa jinsi alivyopendeza. Namna alivyopangilia nguo zake, na zilivyo mkaa. Kifupi yule dada alikuwa ana damu ya nguo!
“Karibu dada Naitwa Inspekta Jamila, sijui nikusaidie nini?”
Eshe aliulizwa na yule mwenyeji wake aliemkusudia.
“Mimi Naitwa Eshe Bint Muhidini, amenielekeza dada mmoja aliekupigia simu muda si mrefu.” Eshe alijibu na kujitambulisha kwa mwenyeji wake.
“Ahaa, wewe ndiye aliekuelekeza Dokta Zahala? Upoje nae yule, kwani ni shoga yangu mkubwa yule, toka tukiwa Shuleni. Na ndiyo Daktari wangu.”
Eshe akamueleza mazingira aliyokutana nae yule dada, ambae sasa amemtambua kuwa ni Dokta Zahala.
Mwisho akamueleza kilichompeleka pale, na kumkabidhi ile barua.
Inspekta Jamila aliipokea na kuisoma. Ilikuwa ni barua ndefu, iliyoandikwa katika mtindo wa Shairi, ikiwa na kichwa kilichosomeka BARUA KUTOKA JELA. Ilikuwa ikisomeka hivi.
Naiandika barua, hapa nipo gerezani Natuhumiwa kuua, eneo la mikocheni Hakika ninaijua, sihusiki asilani. Tuhuma ya jambo zito, kama hili maishani Bora nipakate moto, niungue miguuni Kuliko kuwa na joto, lisilokwisha moyoni Mimi ni Taxi dereva, nikipaki magomeni Akaja bwana Mzava, enda Sinza kijiweni Kumbe baa linawiva, mimi kuwa hatiani.
USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA
Ili Kunipa Nguvu ya Kuendelea Kuwaletea Simulizi Shawishi Wapenzi wa Simulizi Wapakue(Install) App ya CnZ Media