BARUA KUTOKA JELA (2)

Zephiline F Ezekiel
0
Mtunzi: Ibrahim Gama

SEHEMU YA PILI
ILIPOISHIA...
Tuhuma ya jambo zito, kama hili maishani Bora nipakate moto, niungue miguuni Kuliko kuwa na joto, lisilokwisha moyoni Mimi ni Taxi dereva, nikipaki magomeni Akaja bwana Mzava, enda Sinza kijiweni Kumbe baa linawiva, mimi kuwa hatiani.

IKIWA UNASOMA SIMULIZI NJE YA APP YA CnZ Media IPAKUE ILI USIPITWE NA SIMULIZI

ENDELEA...
Nilipokuwa narudi, barabara ya namnani

Nilimuona Masudi, tunaishi majirani

Nami sikuwa na budi, bali kupaki pembeni.

Wakaja watu watatu, wakaingia garini

Tunazo elfu tatu, tupeleke kwa Macheni

Wana begi na viatu, wameshika mikononi

.

Masudi nikamwambia, tutaongea nyumbani

Huku nikitia gia, kurudi barabarani

Pia nikifurahia, kurudishwa maskani.

Baa likaja timia, tulipofika mwishoni

Askari wa doria, walikuwa kwa Macheni

Jamaa walikimbia, wakawacha begi ndani.

Askari walinivamia, na bunduki mikononi

Nikiwa nimetulia, sijui nifanye nini

Nikapigwa pasi hatia, kila sehemu mwilini.

Kivumbi sasa sikia, ndani ya begi kuna nini

Namba za gari bandia, na “Sub mashine gani”

Bastola naishuhudia, na Risasi ishirini.

Kisha nikafungwa pingu, nikapelekwa kituoni

Akaja tajiri yangu, nikapata ahueni

Akapakiwa majungu, akaniona shetani.

Akataka gari yake, aitoe kituoni

Sikuwa na mana kwake, kanitelekeza ndani

Huyoo akaenda zake, namchungulia dirishani.

Habari zilienea, zikasambaa mjini

Jambazi lilozowea, limenaswa mtegoni

Walionitembelea, wengi hawakuamini.

Walikuja ndugu zangu, jamaa na majirani

Mke na mtoto wangu, machozi tele machoni

Baba angu baba angu, analia Marijani.

Uchungu nilionao, hausemeki mdomoni

Unamuwacha mwanao, kwa kuwa kizuizini

Kula na kuvaa yao, ishakuwa mtihani.

Polisi wakachunguza, kiasi siku sitini

Huku wakiniongoza, kuenda mahakamani

Kesi wakaigeuza, nikaletwa gerezani.

Robali ikawa Mada, mazito haya jamani

Bastola ile ya kimada, wa bosi Serikalini

Anaeitwa Hamida, kauwawa mikocheni.

Mimi naweza kunyongwa, hadi kufa kitanzini

Nataka wakili bingwa, pesa sina mifukoni

Nilipo nina magonjwa, kwa kupewa milo duni

Taxi dereva wenzangu, popote pale nchini

Nauaga ulimwengu, bado ninautamani

Someni Barua yangu, kisha nisaidieni.

Karatasi inajaa, ndugu zangu Buriani

Imenijaa fadhaa, na donge tele moyoni

Kuonyesha mashujaa, walau andamaneni.

Naomba wasamalia, mwanangu nileleeni

Atawalipa Jalia, hapahapa duniani

Mimi mola namwachia, walimwengu kwaherini.

Ilimaliza barua ile katika namna ya kuhuzunisha na kugusa moyo ulio hai.

-

Ilimaliza barua ile, huku Inspekta Jamila akiwa makini akamtazama Eshe huku akimuhurumia sana, akamwambia.

“Nimeisoma hii barua na imenigusa sana, kiasi kwamba kwanza itanibidi nimuone huyo Mumeo aliekutwa na mkasa mzito kama huu, kisha nipembue ukweli upo wapi? Ndiyo nitajua nawezaje kumsaidia.”

“Hivyo naomba niandikie majina yake kamili, na sehemu mnayoishi, namba ya nyumba na jina la mjumbe wa eneo hilo. Kisha wewe nenda uje unione siku ya Jumamosi, ili ujue nilipofikia”.

Eshe akafanya kama alivyoagizwa na kisha akaagana na Inspekta Jamila huku akimuachia na ile Barua kutoka jela, akaondoka akiwa na matumaini kiasi.

Inspekta Jamila baada ya kuagana na Eshe aliendelea kukaa mle ofisini mwake, huku akiwa na mawazo tele, kwani ile barua ilimgusa kiasi ilimkosesha raha kwa wakati ule. Aliifungua tena karatasi ya barua ile na akairudia upya kuisoma, hatimae akakata shauri.

Aliangalia saa yake ya mkononi na kuona kuwa ni saa sita adhuhuri, hivyo alifungia baadhi ya vitu katika droo za kabati lake la pale ofisini, na kutoka nje ya ofisi yake akiazimia kwenda katika gereza la keko!

*******

Mwaduga Dingo akiwa na Ispekta Jamila, pamoja na askari magereza wa kiume, walikuwa wamekaa katika chumba maalum, Mwaduga akichukuliwa maelezo na kutakiwa amsimulie kila kitu anachokumbuka hadi yeye kuwa mahala pale akiwa ni Mahabusu!

Mwaduga Dingo alianza kufikiri, na kuanza kumuhadithia. Inspekta Jamila Tangu akodiwe na Bwana Mzava hadi Sinza, kisha alivyokuwa anarudi barabara ya Namnani alipomuona Masudi na yeye kupaki pembeni.

Akamuhadithia walivyokuja watu watatu wakiwa wamebeba Begi na viatu mikononi, na kuingia Garini kwake huku wakimwambia bei na sehemu wanayokwenda, hadi yeye alipomuaga Masudi, na hata tukio lililotokea pale kwa macheni jamaa walipokimbia na kuacha Begi ndani ya gari yake!

Pia kipigo alichokipata na kufungwa pingu hadi kituoni! Kiasi maelezo yake hayakupishana hata kidogo na barua aliyoiandika, ambayo Inspekta Jamila anayo na ameipa jina la Barua kutoka jela.

Inspekta Jamila aliyaandika yale maelezo na kisha kumtupia swali Bwana Mwaduga.

“Ehe baada ya kupelekwa Kituo cha Polisi nini kilifuata?.”

Mwaduga akamueleza. “Niliteswa sana ili niwataje wale abiria wangu, ambao polisi wakati wote wanawaita wenzangu waliokimbia! Ilihali ya kuwa mimi siwatambui! Baadae walikuja watu wa Habari na kunichukua picha za video, na picha mnato.”

“Baadae Tajiri yangu ambae ndio mmiliki wa gari akaja pale kituoni. Maaskari walimwita chemba na kuzungumza nae! Bila ya shaka walimtisha au kumwambia kuwa mimi ni Jambazi! Kwani hakutaka kuniuliza kilichotokea, sikwambii kuniona. Aliondoka huku akiwa amelowa kwa maneno aliyopakiwa.”

“Walikuja jirani zangu, Mke na jamaa wengine ili wanichukulie Dhamana ya Polisi, lakini dhamana ilikataliwa! Yakitolewa maelezo kwamba, kuna wahalifu wenzangu ambao wamekimbia! Hivyo nikiwa nje kwa dhamana nitaharibu upelelezi, na sasa wanasema sitoweza kupata dhamana, kwani mashtaka yanayonikabili kwa mujibu wa sheria za nchi, hayana dhamana hasa mauaji yakukusudia, na unyang’anyi wa kutumia silaha!”

Inspekta Jamila, alitingisha kichwa chake juu chini, akiafiki maneno ya Mwaduga, kisha akamtupia swali la kijinga, lakini lenye maana kubwa kwa muulizaji!

“Sasa hapa upo kwa kesi gani? yakukutwa na silaha kinyume cha Sheria au kuhusishwa na uhalifu wa kutumia silaha?!”

Mwaduga alijibu, “Hapa natuhumiwa na mashitaka manne!“

“Shitaka la kwanza, kupanga njama ya kutenda kosa. Shitaka la pili, kufanya kosa la unyang’anyi wa kutumia silaha. Shitaka la tatu kumiliki silaha kinyume cha sheria. Na shitaka la nne nashitakiwa kwa kosa la mauaji.”

Baada ya kusema hayo Mwaduga akaangua kilio. Inspekta Jamila akiwa makini zaidi akamuuliza tena Mwaduga swali lingine bila ya kujali kilio chake.

“Mada kesi imekujaje?! Au uliua mtu kupitia silaha zilizokamatwa na askari walikuta alama za vidole vyako, pamoja na ile silaha kuitambua?!”

Mwaduga akafuta machozi akaendelea kumjibu Inspekta Jamila.

“Katika uchunguzi wa Polisi ndani ya hii miezi miwili, wanadai walichogundua ni ile Bastola namba yake walipoifatilia, waligundua ni silaha iliyokuwa ikimilikiwa kihalali na mtu alietambulika kwa jina la Hamida Bartazal.”

“Sasa wale maaskari wakaniambia kwamba, huyo Hamida hivi sasa ni marehemu! Sababu ya kifo chake aliuwawa kwa kupigwa risasi na majambazi.”

“Na baadhi ya vitu vilivyoibiwa ilikuwa ni ile silaha iliyokutwa ndani ya gari yangu pale kwa Macheni. Ndipo nilipoelezwa, Kwa kuwa mimi ndiye niliyekutwa na ngozi, basi nitajua nyama ilipo!”

Inspekta Jamila alimuhoji vitu vingi Mwaduga, kiasi akajua wapi aanzie kufatilia mkasa ule mzito. Akaagana na Mwaduga kisha akashika njia akaenda zake akiwa na mawazo tele.

*****

Mkuu wa jeshi la polisi IGP akiwa ofisini kwake, alikuwa ameshika tama kwa mawazo.

“Mpenzi Samahani sana kwa hili ninalotaka kukwambia!” Hamida aliyasema maneno hayo, huku akiwa hana raha hata kidogo! bali anajilazimisha kuwa na furaha!

IGP aligundua hali hiyo na kumuuliza Hamida; “Vipi mbona unaonekana huna raha kabisa leo, ni mtu mwenye mawazo sana kulikoni?!”

Hamida alijichekesha kidogo na kusema, “Hapana nipo sawa tu, ila jana sikupata usingizi wa kutosha. Kwani nilikuwa najisikia vibaya sana, na kukupigia simu mtu na mkeo usiku umepumzika nikashindwa, nilichofanya nilimeza vidonge vya Diazapam nikaulazimisha usingizi! Nilipofumba macho kwa usingizi kulikuwa kumeshapambazuka!”

“Pole sana,je ulitaka kuniambia kitu gani?” IGP aliuliza.

“Nina mashaka kama nitachosema utaweza kukikubali!” Hamida aliyasema hayo huku akizidisha unyonge mara dufu.

“Sawa, sioni sababu ya wewe kuwa na mashaka, ikiwa kitu unachotaka kukisema ni cha kawaida!”

IGP alidadisi huku akiwa na shauku ya kutaka kujua jambo hilo!

“Kinaweza kikawa ni kitu cha kawaida kwangu, lakini kwako kikawa ni kitu kisichowezekana”. Alijibu Hamida.

“Sema nipo tayari kukisikiliza, kama kipo ndani ya uwezo wangu nitakupa”. IGP alimjibu hawara yake.

“Nashukuru kusikia hivyo ‘My Dear’. Kitu chenyewe ni, nahitaji kupiga picha na wewe ili unapokuwa kwa mkeo, na kwangu sura yako iwepo niwe naiangalia! Lakini pia Heshima ya kupiga picha na mtu mkubwa kama wewe, nadhani wanawake wenzangu wengi wangetaka kufanya hivyo!” Hamida alipokuwa akiyasema maneno hayo, alikuwa tayari yupo maungoni mwa IGP amemkumbatia!

“Duh! Sikutarajia kitu kama hicho, kwani nilidhani labda unataka nikununulie Gari!” IGP aliyasema hayo na wote wawili wakaangua kicheko cha chinichini.

“Mimi picha yako kwangu, ina thamani kuliko hata hiyo gari.”

“Sawa hilo lipo ndani ya uwezo wangu, piga picha utakazo!”

Kwa Camera ndogo Digital aina ya Olympus aliyokuwa nayo Hamida katika mkoba wake, akaitega Camera ile katika Automatic, na wakapata picha ya pamoja wote wawili wakiwa wanatabasamu.

IGP aligutushwa na simu yake ya mkononi iliyokuwa inaita, akaondosha mawazo yake na kuipokea ile simu.

*******

Inspekta Jamila alikuwa eneo la mikocheni jirani na Nyumba ya marehemu Hamida. akapiga hodi kwenye nyumba ya jirani, na kijana mmoja wa makamo, alifungua geti, nakumkaribisha ndani.

Baada ya kukaribishwa na kuketi, akajitambulisha na kuanza kumuhoji Bwana mmoja aliyemfahamu kama mwenye nyumba, aitwae Kiyarwenda Mwemezi.

Inspekta Jamila alianzisha mazungumzo baada ya kujitambulisha.

”Nipo hapa kwa ajili ya kufuatilia kifo cha aliyekuwa jirani yako Hamida, hivyo ninataka mchango wako wa mawazo, kama kuna chochote unachofahamu kuhusiana na kifo chake, na jinsi gani unavyomuelewa marehemu Hamida na tabia yake!”

Yule Jirani akafikiri kidogo kisha akajibu.

“Ooh ahaa Ok, mimi nipo hapa muda mrefu sana kabla marehemu Hamida hajanunuliwa nyumba hii na aliyekuwa marehemu mumewe!”

Inspekta Jamila alishituka kidogo akionekana kuwa makini zaidi, huku akimtupia swali la fadhaa jirani yule.

“Marehemu Hamida alikuwa na mume, na mazingira ya kifo chake yapoje huyo mumewe kadiri unavyofahamu?”

Yule jirani huku akimshangaa Inspekta Jamila alimjibu.

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

 Ili Kunipa Nguvu ya Kuendelea Kuwaletea Simulizi Shawishi Wapenzi wa Simulizi Wapakue(Install) App ya CnZ Media

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)