NIFANYE NAMIMI KAKA (7)

0
Mwandishi: Juma Hiza

SEHEMU YA SABA
ILIPOISHIA...
“Eva!” nilimuita lakini kutokana na ile kofia aina ya pama niliyokuwa nimeivaa hakuweza kuiona vizuri sura yangu kwa wakati ule. Alikuwa akinitazama tu bila kusema lolote kwa wakati ule.
SASA ENDELEA...
Wakati nilipokuwa nikiendelea kujitathmini mara simu yangu ikawa inaita, nilipoangalia nililiona jina la Eva likisomeka. Haraka niliyatupa macho yangu kwenye langu kuu la duka lake ili niweze kumuangalia. 

Nilimuona akiwa katika wakati wa kuweweseka hakujua ni wapi mtu huyo aliyekuwa akimpigia simu alipo. Nililifahamu hilo na hivyo sikutaka kuipokea, niliamua kuikata kwa makusudi kitendo ambacho kilimuudhu sana, nilimuona akitokwa na mfyonzo kisha akawa kama anayetaka kurudi ndani.

“Eva!” nilimuita lakini kutokana na ile kofia aina ya pama niliyokuwa nimeivaa hakuweza kuiona vizuri sura yangu kwa wakati ule. Alikuwa akinitazama tu bila kusema lolote kwa wakati ule.
“Eva!” nilimuita tena safari hii nilikuwa nikipiga hatua kumfuata pale alipokuwa amesimama, alikuwa amesimama karibia na mlango wa duka lile.
“Unaniita mimi?” aliniuliza huku akijinyooshea kidole.
“Ndiyo.”
“Unasemaje?”
“Umenisahau?”
“Nikukumbuke kwani we…..” kabla hajamaliza kusema sentensi yake niliamua kuitoka ile kofia na sasa aliweza kupata wasaa wa kunitazama kwa uzuri kabisa. Hakutaka kuamini macho yake kwa kile alichokuwa anakishukudia, kuniona kwa wakati tena katika duka lake hakika hakutaka kuamini kabisa.
“Dick ni wewe?” aliniuliza kisha akafyatuka kutoka pale alipokuwa amesimama na kuja kunikumbatia kumbato ambalo kiukweli lilinifanya nihisi kitu cha tofauti mwilini mwangu. Evadia alikuwa na joto la kipekee sana. Harufu yake ya manukato aliyokuwa akinukia yalizidi kunifanya niwaze mambo mengi sana mengine ambayo hata hayajulikani.
“Dick,” aliniita kipindi tulipokuwa tumekumbatiana.
“Niambie,” nilimwambia huku nikimpigapiga kwa utulivu mgongoni.
“Siamini kama nimekuona tena.”
“Amini sasa ndiyo umeshaniona,” nilimwambia kisha akajitoa katika lile kumbato halafu kazi iliyokuwa imebakia ni kuanza kunitazama. Alikuwa akinitazama mpaka kuna kipindi nilianza kuona aibu.
“Mbona unanitazama hivyo.”
“Siamini.”
“Huamininini sasa?”
“Kama ningekuona tena.”
“Hahahaha.”
“Mbona unacheka sasa.”
“Kwani wewe ulikuwa unamfuata nani sasa huku nje?”
“Kuna mjinga mmoja kaniambia nije kumchukua sasa natoka simuoni mpaka ameniudhi yani kama sio huyo mtu nadhani hata nisingekuona.”
“Hahaha! Mshukuru sasa.”
“Nimshukuru nani?”
“Huyo mtu ambaye amekufanya utoke nje.”
“Hahaha na kweli?”
“Dick.”
“Niambie Mrembo.”
“Yani hata sijui nianzie wapi kwanza hii sio sehemu nzuri kwa ajili ya mazungumzo embu kama hutojali twende sehemu hivi tukakae ili tuongee mawili matatu.”
“Na dukani je?”
“Kuna msichana nimemuajiri yeye ndiye anayenisaidia hivyo usijali.”
“Sawa.”
“Nisubiri basi ili nimuage.”
“Usijali,” nilimjibu kisha akaingia ndani na baada ya dakika kadhaa aliweza kutoka. Tuliongozana mpaka sehemu ya maegesho ya magari, aliniambia niingie katika moja ya gari aina ya Harrier kisha na yeye akaingia akawasha gari tukaondoka eneo lile. Safari yetu fupi ilikwenda kuishia katika moja ya Restaurant moja ambayo ilikuwa maeneo Mwananyamala na hapo tulikwenda kwa nia moja tu! ya mazungumzo.

Mpaka kufikia kwa wakati ule sikuwa nimemwambia ukweli kuwa mimi ndiye niliyekuwa nimempigia simu, niliamua kumficha huku nikiwa na maana yangu ya msingi.

Tulifika nje ya Restaurant moja iliyokuwa ikijulikana kwa jina la ‘Fast Food Restaurant’ maeneo ya Mwananyamala. Ilikuwa na mazingira mazuri sana, kwa macho ya haraharaka ilikuwa ni Restaurant yenye hadhi fulani, waliyokuwa wanaingia humo kwa ajili ya kupata chakula walikuwa ni watu wenye maisha ya kujiweza.
“Kwahiyo umesema tumekuja kufanyaje huku?” niliamua kumuuliza wakati alipokuwa akiegesha gari katika maegesho ya Restaurant ile.
“Tumekuja kuzungumza tu,” alinijibu huku akionekana kutojali lolote lile.

Nakumbuka mfukoni sikuwa na pesa kubwa zaidi ya nauli yangu ambayo niliamini ingeweza kunirejesha nyumbani salama kabisa bila bugdha yoyote. Kitendo cha kuingia katika Restaurant ile halafu mfukoni nilikuwa sina kitu hakika kiliniweka katika wakati wa mawazo sana, sio mimi tu hata kama ungekuwa ni wewe mpenzi msomaji ungekuwa katika wakati wa mawazo.

Mawazo ya harakaharaka yaliyonijia kwa wakati ule ni kumuona muhudumu akija na kuanza kunidai pesa baada ya kula. Niliuona ugomvi mkubwa pamoja na kudhalilishwa kukinijia mbele yangu.
“Dick!” sauti ya Evadia ndiyo iliyonishtua kunitoa katika dimbwi la mawazo kwa wakati ule.
“Naam,” nilimuitikia huku nikiwa kama niliyekuwa sifahamu lolote lile.
“Mbona umezubaa.”
“Hamna.”
“Ok tushuke basi.”
“Kwani ni lazima tukaongelee humu ndani?”
“Ndiyo hakuna shida pametulia sana.”
“Sawa,” nilijibu kinyonge kisha nikaanza kushuka kwenye gari kisha tukaingia ndani ya Restaurant ile tukakaa katika moja ya meza ambayo aliichagua Evadia na sasa tukawa tunatazamana.
“Unatumia nini?” aliniuliza Evadia, wakati huo mmoja wa wahudumu wa Resteurant ile alikuwa akitusikiliza tumuagize.
“Natumia kivipi?”
“Hahahaha! Umeanza utani wako.”
“Sasa natumia tumiaje?”
“Bhana ujue unamchelewesha Dada wa watu.”
“Dada wa watu kwahiyo mimi sokwe.”
“Hahaha! Embu acha bhana.”
“Ok mimi naomba uniletee maji ya baridi,” nilimuambia yule Dada ambaye alikuwa ni muhudumu.
“Maji?” aliniuliza Evadia huku akionekana kushangazwa sana kitendo cha mimi kuagiza maji.
“Ndiyo.”
“Embu kuwa serious bhana sasa maji utashiba nini?”
“We huoni hili jua na hili joto la Dar.”
“Hata kama lakini agiza kitu cha maana.”
“Huko nitokapo nimekula jamani utanipasua tumbo.”
“Hahaha sawa.”
“Na wewe Madam unaagiza nini?” aliuliza yule muhudumu huku akimuangalia Evadia ambaye swali lilikuwa likimlenga.
“Mimi niletee juice tu.”
“Sawa,” alijibu yule muhudumu kisha akaondoka kufuata vinywaji ambavyo tulikuwa tumemuagiza.

Nilikuwa nikimtazama muda wote, alionekana kuwa msichana mrembo sana, kila sehemu ya mwili wake ilikuwa imejaaliwa.

Labda nikukumbushe sifa alizokuwa nazo, Alikuwa ni msichana mrembo sana, kuanzia sura yake ya kuvutia, macho ya kungu ambayo muda wote yalikuwa yakirembua tu, umbo la namba nane, chuchu saa sita yani alikuwa ni mrembo kwelikweli.
“Niambie mrembo,” nilimwambia mara baada ya kuletewa vinywaji na sasa ulikuwa ni muda muafaka kwa ajili ya mazungumzo yetu.
“Safi tu.”
“Halafu hujaniambia unaishi wapi?”
“Mimi naishi Tabata.”
“Tabata.”
“Ndiyo.”
“Tabataaaa,” nilirudia kutamka huku nikijifanya kuitafuta ilikuwa ni Tabata ipi.
“Hahaha! Tabata Bima,” alinijibu.
“Oooh! Umepanga au?”
“Hapana naishi na wazazi wangu.”
“Kumbe bado hujakuwa.”
“Kwanini?”
“Mpaka umri huo bado unaishi tu kwa wazazi.”
“Wananipenda sana ujue hata lile duka baba ndiyo kanifungulia.”
“Kumbe kwenu maisha safi.”
“Hahaha! Kawaida mbona.”
“Sio kwa kawaida hiyo.”
“Ok na wewe unaishi wapi?”
“Mimi nipo Tanzania mkoa wa Daresalaam,” nilimjibu jibu lililomfanya atokwe na kicheko. Alijikuta anacheka bila kutegemea.
“Sasa mbona unacheka.”
“Ndiyo najua upo Tanzania tena Dar, nataka kujua sehemu unapoishi.”
“Tandale.”
“Tandale!”
“Ndiyo kwani vipi?”
“Tandale kule uswahilini?”
“Ndiyo ndanindani kabisa.”
“Unaishi na wazazi?”
“Hapana naishi peke yangu, niliamua kukimbia kwa wazazi mapema kuhofia usumbufu wa kutumwa vibandani na utuuzima huu.”
“Hahahaha! Haya bhana.”
“Sasa mbona unacheka?” nilimuuliza.
“Sicheki tena,” alinijibu kisha akawa anakunywa juice yake katika utaratibu, alikuwa akinywa kwa mapozi yasiyomithilika. Kichwani mwangu nilijaribu kumkumbuka msichana ambaye niliwahi kumuona akinywa kwa mapozi yale, kwa kweli kumbukumbu hiyo ilikataa kunijia kabisa ila nilichokumbuka kuwa mara yangu mwisho niliandika Chombezo kisha nikawa namuandika msichana mrembo ambaye alikuwa akila chakula katika mapozi ya hali ya juu.
“Nikwambie kitu,” nilimwambia huku macho yangu yakiendelea kumtazama katika namna ya ‘Nikubalie nikakupe leoleo.”
“Niambie,” aliniambia huku akijaribu kuzilamba lips zake ambazo zilimwagikiwa na juice.
“Kuna msichana unafanana naye sana yani kila kitu,” nilimwambia kisha nikawa kama namaanisha kile ambacho nilikuwa nakizungumza.
“Msichana yupi huyo?” aliniuliza, wakati huo nilikuwa nikipiga fundo la maji yaliyokuwa katika glass.
“Sijui hata nimuelezee vipi,” nilimwambia huku nikijifanya kuchanganyikiwa kutokana na kile nilichokuwa nataka kumwambia kwa wakati ule.
“Wewe niambie tu! nitakuelewa,” aliniambia huku akionekana kuwa makini kutaka kumsikia huyo msichana ambaye nilimwambia kuwa alifanana naye sana kwa kila kitu.
“Unataka kumfahamu huyo msichana?”
“Ndiyo niambie.”
“Ok msichana mwenyewe ni mhusika wa chombezo langu, yani amefana na wewe kila kitu,” 

Nilimwambia maneno ambayo yalimchekesha sana, hakutaka kuamini kama ule muda wote niliyokuwa namzungusha juu ya msichana ambaye alikuwa amefanana naye kuwa ningeweza kumwambia vile.

Maneno yangu yalizidi kumfurahisha sana Evadia kuna kipindi nilipokuwa nikizungumza naye alikuwa ananiambia kuwa alikuwa akijivunia kunifahamu katika maisha yake kwani nilikuwa nikimfanya kuwa na furaha kila wakati.

Nakumbuka nilizungumza naye mambo mengi sana kuhusu maisha, kazi na marafiki lakini sikutaka kumgusia kabisa suala la mapenzi. Niliamua kufanya hivyo kwa sababu Evadia alitokea kunichukulia kuwa kama rafiki yake au ule ukaribu aliyokuwa nao kaka na dada. 

Kwa kweli nilijikuta nashindwa nianzie wapi ili niweze kumteka kimapenzi, kila mtego niliyokuwa nikiutumia alikuwa akiutegua na ni hapa ambapo sikutaka kabisa kumueleza tukio nililokuwa nimelifanya la kumdanganya jina katika simu mpaka pale alipotoka nje na kukutana na mimi. 

Niliamua kuendelea kumficha huku katika kichwa changu nikijaribu kupanga mashambulizi mengine ambayo ningeweza kuyatumia katika kumpata Evadia msichana mrembo ambaye alikuwa akitokea katika familia ya kitajiri sana.

Nilizidi kuwa katika wakati wa mawazo sana, muda wote nilikuwa nikimfikiria Evadia msichana mrembo ambaye alitokea kuuteka moyo wangu, nilichokuwa nakitamani kwake ni kuona siku moja anakuwa wangu kisha naufahamu na utamu wake.

Niliporudi nyumbani kwangu, usiku wa siku hiyo hakukuwa na kazi nyingine zaidi ya kumfikiria Evadia tu, nilizidi kujilaumu sana kwa kushindwa kumpata katika Maisha yangu.
“Haiwezekani,” nilijisemea kisha nikapiga ngumi kwenye godoro kwa ghadhabu.

Niliamua kuichukua simu yangu na kisha nikaingia kwenye kitabu cha kuhifadhi majina, nilikuwa nikijaribu kupitia jina moja baada ya lingine huku nikiyafuta yale majina ambayo nilikuwa siwasiliani nayo kabisa. 

Ni katika zoezi hili fupi ambapo niliweza kukutana na jina la Mick. Mick alikuwa ni rafiki yangu mkubwa sana, alikuwa ni mtu ambaye niliweza kusaidiana naye mambo mengi sana, ulipokuwa unauzungumzia urafiki wa kweli wa kufa na kuzikana basi usingeacha kuuzungumzia urafiki wangu na Mick

KUNA MATANGAZO YANATOKEA KWENYE APPLICATION YETU HIVYO UKIYAONA NAOMBA BONYEZA HAPO NDIO UNANIPA SAPOTI MIMI, UKIBONYEZA UNAWEZA KUCANCEL SIO LAZIMA UENDELE ULIKOPELEKWA, KIKUBWA UBONYEZE HATA MARA 2-3 KILA UKIFUNGUA APP YETU

USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA

TAZAMA KICHEKESHO HIKI KISHA BONYEZA SUBSCRIBE ILIYOPO CHINI YAKE WAKATI TUKIELEKEA KWENYE MUENDELEZO

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)