
Mtunzi: Ibrahim Gama
SEHEMU YA TATU
ILIPOISHIA...
ILIPOISHIA...
“Marehemu Hamida alikuwa na mume, na mazingira ya kifo chake yapoje huyo mumewe kadiri unavyofahamu?”
Yule jirani huku akimshangaa Inspekta Jamila alimjibu.
IKIWA UNASOMA SIMULIZI NJE YA APP YA CnZ Media IPAKUE ILI USIPITWE NA SIMULIZI
ENDELEA...
“Ndiyo marehemu Hamida alikuwa na mume aliyekuwa anaitwa Bartazal Halim, alikuwa Tajiri kiasi yule Bwana na mtu mkarimu sana! Amefariki miaka miwili iliyopita kwa kilichosemekana ni shinikizo la Damu!”
Inspekta Jamila alishusha pumzi, na akawa anamuangalia yule bwana kwa utulivu mkubwa uliojaa udadisi na umakini wa hali ya juu!
Na yule Jirani akaendelea.
“baada ya kifo chake, siku chache ndugu wa marehemu walijitokeza kudai mali za ndugu yao, lakini ulitokea mshangao wa mwaka!
kwani miezi mitatu nyuma marehemu Bartazal inasadikiwa alimuandikisha mali zake zote mkewe Hamida!
Ndugu wa marehemu hawakuridhika na jambo hilo hata kidogo! kwani katika uhai wake, marehemu hata siku moja hakuwahi kuwaambia ndugu zake kama amemuandikia mkewe mali zote!
Lakini pia kaka yao hakuwahi kupata kuugua shinikizo la Damu katika maisha yake ya miaka hamsini na ushee!
Ila Daktari katika ripoti yake alisema, marehemu aliona au kusikia jambo la kushitua sana, na ndiyo ikapelekea kupata shinikizo la Damu nakusababisha kifo chake!”
Inspekta Jamila huku akimuangalia usoni jirani yule, akasema huku akiwa hana Raha hata kidogo!
“Nimekuja hapa kujua namna kifo cha Hamida kilivyotokea! Ila haya unayonipa nayo ni taarifa inayopaswa kufanyiwa kazi! Lakini je? Wewe uliyajuaje? Yote haya!”
Jirani wa Marehemu Hamida akamjibu.
“Marehemu Bartazal alikuwa ni rafiki yangu sana, na hata ndugu zake walipokuwa wakija kumuona, lazima aliwaleta kwangu au mimi kwenda kwake.
Na hao ndugu zake ndiyo waliokuwa wakinipa taarifa hizi zote!”
Inspekta Jamila akamtupia swali lingine Bwana Yule.
“Nikitaka kuwaona hao ndugu zake marehemu Bartazal naweza kuwaona wapi?”
Jirani yule alimkatisha tamaa kabisa jibu lake alipojibu.
“Marehemu Bartazal hana ndugu kwa sasa hapa Dsm, kwani baada ya mazishi, na kumalizika Arubaini, alikuja ndugu yake mmoja na kunieleza kwamba anasafiri, anakwenda kuishi Marekani. Yeye na familia yake, na nikawasindikiza hadi Uwanja wa ndege, na baada ya ndege kuruka mimi ndiyo nikaondoka!
Ila yule ndugu yake wa kike, nina mwaka sasa sijui wapi alipo, na kama yupo hai, au amekwishakufa. Kwa hapa nchini walikuwa wanaishi Arusha.”
Inspekta Jamila huku akitingisha kichwa kwa majibu yale muhimu katika kesi ile akamtupia swali linguine.
“Sawa. Turudi kwa marehemu Hamida, je baada ya kifo cha mumewe mliendelea kuwa majirani wema?”
Yule Jirani bila ya kusita wala kuuma maneno akajibu swali lile, huku akitikisa kichwa kwa masikitiko.
“Marehemu Hamida alinichukia ghafla sana akidai kwamba, mimi na ndugu wa marehemu mumewe, tuna njama za kumnyang’anya mali zake za urithi wa marehemu mumewe. Hivyo akanichukia toka siku ile!”
Inspekta Jamila akiwa na mawazo tele akamuangalia tena yule bwana kuanzia juu hadi Chini,kisha akamtupia swali jingine huku akiangalia ile “Tape Recorder” yake kama inafanya kazi yake sawa sawa!
“Sasa nataka kufahamu jambo lingine kutoka kwako, baada ya marehemu Bartazal, nani alikuwa mwanaume anayelala na kuamka na Hamida? na je tabia yake ilibaki kuwa ileile kama alipokuwa na marehemu mumewe au ilibadilika?!”
Jirani yule huku akionyesha kuchoshwa na kukerwa na maswali alijibu.
“Nikianza na Tabia, kwa kweli ilibadilika. Kwani alianza tabia za ulevi na kurudi usiku mwingi! Na kuhusu mwanaume, kwa kweli sina hakika na hilo, kwani mie huwaona wanaume tofauti tofauti. Na asilimia kubwa ni vijana wenye uwezo mkubwa kifedha, kwani magari yanayoingia humo ndani ni ya kifahari tupu!”
Inspekta Jamila alivutiwa na habari hiyo, kiasi ilimfanya akae vizuri na kumuuliza.
“Unaweza kuzikumbuka namba za magari zilizokuwa zikiingia na kutoka mara kwa mara kwa marehemu Hamida?!”
Jirani yule akionyesha kuchoshwa na maswali ya mfululizo alijibu.
“Mh kwa kweli huo ni mtihani, kwani kukaa kuchunguza namba za magari ya watu! Hapana hilo sikumbuki hata kidogo.”
-
Inspekta Jamila akamuwahi kwa swali lingine tena, safari hii akimkazia macho yake laini, kiasi badala ya kutisha yaliongeza urembo wake!
“Sawa na kifo cha Hamida, kilitokea baada ya kuvamiwa na majambazi nakupigwa risasi ya kichwa iliyotoa uhai wake. Je? Hufikirii ni jambo la kupangwa kwa ajili ya kisasi cha marehemu mumewe?”
Jirani yule sasa akiwa amechoka kabisa kujibu maswali mfululizo alijibu kwa mkato.
“Sina hakika, hiyo ni kazi yenu polisi kujua!”
Inspekta Jamila aliendelea kumuhoji jirani yule hadi aliporidhika kwamba amepata taarifa zote alizozitaka, akaagana na bwana Yule, huku akichukua namba ya simu ya jirani yule, akaondoka.
*******
Siku tatu Baadae! Ikapatikana taarifa ya ajali mbaya iliyochukua uhai wa mtu
katika Eneo la Bunju, kwenye Daraja la Mto Mpiji, mpakani mwa Mkoa wa Dsm na Mkoa wa Pwani Wilaya ya Bagamoyo.
Mtu aliefariki katika ajali ile, alitambuliwa kuwa ni Bwana Kiyarwenda Mwemezi, yule jirani yake marehemu Bartazal na marehemu Hamida aliyeongea na Inspekta Jamila siku tatu nyuma.
Alikutwa na kitambulisho chakupigia kura kwenye pochi yake, pesa tasilim shilingi elfu hamsini, iliyosalimika kuibiwa na vibaka labda, baada ya askari wa Usalama kufika eneo la tukio muda mfupi tokea ajali ile itokee, ambayo gari iliacha njia na kuingia mtoni ikichoma chini kwenye maji machache ya mto, yaliyokuwa yanaelekea Baharini!
Simu ya marehemu haikupatikana kwenye eneo la tukio. na hata Inspekta Jamila alipokuwa anaipiga tena na tena jibu lilikuwa ni lilelile.
“NAMBA UNAYOPIGA KWA SASA HAIPATIKANI TAFADHALI JARIBU TENA BAADAE!!”
Inspekta Jamila alichanganyikiwa kupita kiasi huku akizidi kupata shaka kwamba Kifo cha Hamida inawezekana ikawa ni kisasi cha marehemu mumewe! Lakini ikiwa ndugu hawapo je ni nani tena anaeendeleza mauaji haya?!
Na akiwa marehemu Hamida kweli alimuuwa mumewe kwa njia moja au nyingine, kwa nini afanye hivyo? Kama ikiwa ni kutaka mali mbona alishaandikishwa na mumewe?! Kijasho chembamba kikamtoka Inspekta Jamila!
****
Inspekta Jamila akiwa nyumbani kwa marehemu Hamida, akiwahoji ndugu wa marehemu Hamida wanaoishi mle ndani, kisha kama mtu aliegutushwa na kitu, akataka aletewe Albamu zote za picha za marehemu Hamida. Wale ndugu wakasema.
“vitu vyote vipo chumbani kwa marehemu.”
yule mwenyeji wake alikwenda katika chumba cha marehemu Hamida na kurudi na picha za marehemu Hamida zilizokuwa katika albam nne na kumkabidhi
Inspekta Jamila.
Inspekta Jamila alizipitia Albam zile moja baada ya moja, alipofika katika
Albam ya Tatu iliyoonekana ni mpya kidogo tofauti na zile zilizopo pale, ilimvutia kuitazama Inspekta Jamila, na picha ya tatu toka aanze kuifungua ile Albam alikutana na kijana mmoja wa kiume, aliyekuwa ameshika Glass ya Bia akimnywesha marehemu Hamida.
Inspekta Jamila Akaiangalia kwa makini kisha akaigeuza nyuma na kukuta imendikwa tarehe iliyopigwa ile picha na mahali ilipopigwa tu! Haikuwa na jina la yule mhusika katika picha ile wala la Hamida!
Inspekta Jamila akaichomoa na kuitumbukiza kwenye ‘HAND BAG’ yake na kuendelea kufungua picha zingine. Mara! hakuyaamini macho yake alipokutana na picha ya Bosi wake kwenye Albam ile, akiwa anapata chakula cha jioni katika Mgahawa mmoja maarufu, akiwa na Marehemu Hamida!
Inspekta Jamila akashusha pumzi ndefu huku akifikiri kwa undani zaidi kwani haelewi uhusiano wa mkuu wake wa kazi na marehemu Hamida, hata wakapiga picha ya pamoja. Na ataanzaje kumuhoji mkuu wake wa kazi kuhusu picha yake kuwa katika Albam ya marehemu Hamida, na hasa ukizingatia yeye Inspekta Jamila, hakukabidhiwa kesi hiyo na yeye anapeleleza kwa siri ili kupata ukweli wa mambo! Kwa mujibu wa BARUA KUTOKA JELA.
Mwisho ile picha nayo akaichukua na kuiweka ndani ya mkoba wake, akaendelea kupekua picha zingine. Kwa mara nyingine akapatwa na mshtuko wa mwaka, pale alipomuona Dokta Masawe akiwa amepozi na marehemu Hamida! Ndani ya gari nyekundu, aina ya TOYOTA CALDINA! na ni picha ambayo haikupigwa muda mrefu sana toka Hamida atoke kuwa KIZUKA. Kwa mujibu wa maandishi yaliyokuwa nyuma ya picha ile, tarehe, mwezi na mwaka. inavyosomeka!
Dokta Masawe ni daktari bingwa na maarufu kwa kuunga mifupa, na viungo vya mwanaadamu, anaefanya kazi katika hospitali ya rufaa ya Muhimbili kitengo cha Moi.
Inspekta Jamila akaichomoa na ile picha na kuitumbukiza ndani ya kibegi chake maarufu kwa jina la kipima joto, na alipoiangalia ile Albam ya nne haikuwa na picha za maana kwake. Hivyo Inspekta Jamila akawaambia wale wenyeji wake.
“Nimechukua picha tatu kwa upelelezi zaidi. Baada ya kukamilisha zoezi zima nitazirejesha!
Nashukuru kwa ushirikiano mlionipa, mungu akipenda nitarudi tena siku nyingine.”
Akachukua namba ya simu ya yule mdogo mkubwa wa marehemu Hamida aliejitambulisha kwake kwa jina la Neema, Akaaga na kutoka eneo lile huku akiwa na msongamano wa mawazo ukitembea katika kichwa chake, nakujuta kujiingiza katika kesi ile ambayo, inaonekana ni kubwa kuliko alivyofikiri yeye!
*******
Maeneo ya Mburahati Barafu, bwana Masudi akiwa amekaa na mkewe anakunywa chai, mara akasikia hodi. Naye akamwambia mkewe akamsikilize mgeni kwa kuwa ilikuwa ni sauti ya kike!
Mke wa masudi, anatambulika sana maeneo yale kwa jina la Mama chapati, kwa umaarufu wake wa kuchoma chapati ambazo ili uzipate chapati zake, itakubidi mtu udamke asubuhi na mapema sana. Kwa wale wenye usingizi wa pono, watazisikia kupitia kwa watu waliozinunua na kuzila!
Yule mwanamke mnene na mrefu wa wastani aliinuka, akafunga khanga yake vizuri kifuani na kufungua mlango.
Akakutana uso kwa uso na mwanamke mmoja mwenye sifa zote za kuitwa mrembo. Yule mgeni, alimsalimu mwenyeji wake, kisha akamuuliza.
“Samahani Dada, Bwana Masudi nimemkuta?”
Mke wa Masudi akajibu. “Ndiyo umemkuta na mimi ndiye mkewe, tukusaidie nini, na unashida gani na mume wangu?!”
Mke wa Masudi aliuliza maswali yaliyojaa wivu tele! “Nashukuru kukufahamu kuwa wewe ndiye mke wa Bwana Masudi, pia ninafurahi kusikia nimemkuta Bwana Masudi, kwani mguu huu ni wa kwake!”
Alijibu Yule mgeni bila ya khofu yoyote huku akijiamini nakumtazama yule mwanamke machoni bila kupepesa macho!
Kitendo kilichomshangaza sana mke wa Masudi.
Na mara Masudi akatokea pale, baada ya kusikia maneno ya wale wanawake wawili.
USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA
Ili Kunipa Nguvu ya Kuendelea Kuwaletea Simulizi Shawishi Wapenzi wa Simulizi Wapakue(Install) App ya CnZ Media