
Mtunzi: Ibrahim Gama
SEHEMU YA NNE
ILIPOISHIA...
ILIPOISHIA...
Kitendo kilichomshangaza sana mke wa Masudi.
Na mara Masudi akatokea pale, baada ya kusikia maneno ya wale wanawake wawili.
IKIWA UNASOMA SIMULIZI NJE YA APP YA CnZ Media IPAKUE ILI USIPITWE NA SIMULIZI
ENDELEA...
“Karibu”, Bwana Masudi akatamka, huku akimtazama kwa umakini yule mwanamke mwenye kutetemesha wanaume wengi kwa urembo wake.
“Aksante bila shaka wewe ndiye Bwana Masudi?”
Masudi akaitikia kwa kichwa, na yule mgeni akaendelea.
“Mimi ni mgeni wako na nimefurahi kukukuta, kiasi najiita ni mwenye Bahati kwa siku ya leo!”
Mke wa Masudi akamtazama mumewe huku akiwa amekasirika vibaya sana, akamwambia mumewe.
“Hivi huo umalaya wako unauleta hadi nyumbani? Umeona huko nje hakutoshi mpaka uniletee nyumbani wanawake zako? Tuseme huwaambii kama umeowa mpaka wakufate nyumbani tena asubuhi?!”
Yule mgeni akapigwa na butwaa! Akimsikitikia Mwanamke mwenzake alivyokuwa hajiamini!
Masudi akiwa ametaharuki kwa maneno ya mkewe pia akiona vibaya dhana mbaya ya mkewe, hatimaye akamwambia mkewe.
“Mke wangu vibaya namna hiyo. Huyu ni mgeni na hujui yupo hapa kwa ajili gani, hivyo si busara kutoa lugha ya namna hiyo! Msalie mtume mwanamke heh!”
“Ukiona hivyo huaminiki kwa mkeo ndiyo maana anakuwa hivyo”.
Akajibu Yule mgeni huku akitabasamu! Kitu ambacho kilimzidisha hasira mke wa Bwana Masudi mara mbili ya mwanzoni!. Naye Bwana Masudi akiwa anamtazama yule mwanamke huku akishangaa kwa ujasiri anaouonyesha kwenye nyumba yao.
“Okey mimi ninaitwa Inspekta Jamila kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi, nipo hapa kwa ajili ya mahojiano machache tu na wewe Bwana Masudi, kuhusu kesi inayomkabili jirani yako na Swahiba wako mkubwa Bwana Mwaduga Dingo.”
Inspekta Jamila aliyasema hayo huku akionyesha kitambulisho chake.
Mke wa Bwana Masudi akashika kichwa, kisha akakaa chini kwa hofu aliyoipata baada ya kuona mtu aliyekuwa akimtilia mashaka ya wizi wa mumewe, kumbe ni Askari mpelelezi.
Bwana Masudi nae macho yalimtoka pima akiwa hakutegemea kitu kama kile kutokea.
“Karibu Inspekta na samahani kwa yote yaliyojitokeza.” Hatimae Masudi akajibu.
Inspekta Jamila huku akiwa amemnyooshea mkono wake wa kulia, akiashiria kwa kiganja chake kuwa ameisamehe ile hali, akamwambia.
“Usijali ni mambo ya kawaida tu hayo, nishakutana na changamoto zaidi ya hizi nikiwa nipo kazini!”
Baada ya kuketi hatimaye mke wa Bwana Masudi alipata kauli ya kusema.
“Afande nisamehe kwa kukujibu vibaya.”
“Usijali, Usijali mambo ya kawaida hayo, ila mwanamke lazima ujiamini.”
Inspekta Jamila aliyasema hayo, Huku akimgeukia Bwana Masudi. Akatoa kalamu na kijitabu chake akiwa tayari kwa mahojiano!
“Bwana Masudi unakumbuka nini kilichomtokea jirani yako Mwaduga? Na mara ya mwisho kuonana na jirani yako akiwa huru? Ilikuwa katika mazingira gani na wapi?!”
Inspekta Jamila akaanza kwa maswali mfululizo.
Bwana Masudi akiwa katika hali ya huzuni iliyochanganyika na hofu, akafikiri kidogo kisha akasema.
“Nakumbuka kiasi cha miezi miwili nyuma nikiwa maeneo ya Sinza Madukani, katika mihangaiko yangu ya kila siku niliona gari ya jirani yangu anayoiendesha, na nilipomwangalia Dereva anayeendesha nikaonana uso kwa uso na Mwaduga!
Wote wawili tukatabasamu, na Mwaduga akapaki pengeni gari yake.
Nilipofika Karibu na gari ilipopaki, wakatokea jamaa watatu wakiwa wamebeba begi na viatu wameshika mikononi kama wamachinga wakaingia ndani ya gari, nami wakati huo nilishafika pale kwenye gari. Wale jamaa mmoja aliepanda mbele akasema tunazo Elfu tatu tupeleke Bar ya Macheni Magomeni! Mwaduga akanambia tutaongea nyumbani akaitoa gari nakuiweka barabarani huku anatabasamu!”
Inspekta Jamila akamkazia macho Bwana Masudi huku akiandika kwenye kitabu chake kidogo na akadakia kwa swali!
“Umesema wale jamaa watatu walipanda gari wewe ukiwaona na si kama Mwaduga alitoka nao sehemu kabla ya pale, Je?! Kwa nini basi alikuwa anatabasamu baada yakuwapakia wale jamaa? Na kama alisimama kwa ajili yako mbona alichosimamia hamjaongea yeye akaondoka?“
Bwana Masudi akajibu; “Wale jamaa wamepanda gari yake na mimi nikiwa pale, sio kama alikuja nao kwenye gari. Labda lililomfanya akatabasamu, ninahisi kwa vile yeye anapaki kule magomeni usalama na alikuwa anarudi tupu, sasa amepata abiria wanaomrudisha kijiweni kwake kwa shilingi 3000/ mtu yeyote angefurahia bila shaka!”
“Sawa je utapowaona tena watu wale unaweza kuwakumbuka?! Na unaweza kunipa wasifu wao namna walivyo?! Au hata nguo walizozivaa siku ile?”
Inspekta Jamila alimuuliza Masudi kwa shauku. Na Masoudi akajibu.
“Kwa kweli yule mmoja aliepanda mbele namkumbuka kwa sura. Jamaa ana kithethe anapoongea, kwani hata neno tunazo Elfu tatu, yeye alitamka TUNADHO ELFU TATU! Wale wengine wawili sikuwakariri sura zao sawasawa kwani gari ilikwisha ondoka! Ama nguo alizovaa yule jamaa aliepanda mbele, alivaa suruali ya jinzi na fulana moja nzuri sana iliyokuwa imeandikwa MKIMBIZI ikiwa na picha ya mwana dada mmoja akiwa kama anakimbia! Ile jinzi ilikuwa na Rangi nyeusi na fulana ya rangi nyeupe.”
Inspekta Jamila akamuhoji Masudi mambo mengi kiasi akaridhika kwa hatua aliyopiga. Na kiasi alianza kupata Mwanga kuwa, Mwaduga hakuwa anajua chochote katika mkasa unaomkabili, lakini ataihakikishiaje serikali ili ielewe kile anachosema?! Na kama Mwaduga si muhusika, je nani ataesimama akiwa ndiye muhusika halisi?
Inspekta Jamila. Akaagana na Masudi huku wakipeana mkono wa kwa heri yeye na mkewe, ambae sasa alikuwa ni mtulivu na mwenye nidhamu ya hali ya juu!
*****
-
Wapelelezi wawili walikuwa wamekaa kwa pamoja wakijadili hali ya upelelezi wao walioufanya katika kesi inayomkabili Dereva Taxi Mwaduga Dingo, kwani kesi ya mauaji inayomkabili, sasa jalada lake, upelelezi umeshakamilika, na mwendesha mashtaka wa serikali anatarajia kulipeleka jalada mahakama kuu kwa ajili ya kesi kuanza kusikilizwa. Baada ya kutajwa mara kadhaa katika Mahakama ya hakimu mfawidhi ya Kisutu, Mahakama ambayo haina uwezo wa kusikiliza kesi za mauaji kwa mujibu wa sheria za nchi.
Afande Kubuta ambae ndie mpelelezi, aliekabidhiwa kupeleleza kesi zinazomkabili Mwaduga Dingo, akiwa na mpelelezi mwenzake Afande Magane, walikuwa wanalipitia lile faili kwa kituo, ili liwasilishwe Mahakama kuu kwa kusikilizwa.
Afande Kubuta alianzisha mazungumzo. “Yule kijana kwa jinsi nilivyo muhoji na kumpa kibano lazima angesema kila kitu yule, lakini yule kijana kama ni sugu basi yule ni mwalimu wao! Kwani katika mkono wangu, haijawahi kutokea mualifu nimuweke katika kiti moto kisha asinieleze ukweli, ndiyo kwanza yule kijana amefanikiwa! Ameharibu CV yangu yule!”
Afande Magane akasema: “Inawezekana yule ameshawishiwa na wale jamaa akaingia katika mkumbo kwa tamaa ila wale jamaa hawajui wala nini!”
Afande Kubuta nae akasema. “Tulipokwenda kumpekua, nyumbani kwake hatukukuta vitu vya maana sana, ila kulikuwa kuna Tv moja aina ya Sony nchi 14 mpya kabisa, na nilipohitaji stakabadhi iliyonunulia Tv ile, nikahisi kuwa yule kijana anahusika kwa namna moja au nyingine. Kwa sababu stakabadhi ile tarehe yake ilikuwa inaonyesha kuwa, Tv ile imenunuliwa siku moja baada ya mauwaji ya Hamida kutokea! Na kwa kuwa Silaha ya Marehemu Hamida amekutwa nayo yeye, kisha Tv yake imenunuliwa siku moja baada ya kifo kile, hii wala haihitaji Digirii kutambua kwamba baada ya kijana yule kushiriki katika tukio lile la mauwaji, mafao yake ndiyo amenunulia Tv”
Hivyo Wakiwa katikati ya Mjadala ule simu ya Mkononi ya Afande Kubuta iliita na alipoiona namba ya simu iliyokuwa inaita, moyo wa Afande Kubuta uliruka sarakasi na kuipokea simu ile.
“Ndiyo Afande, sawa mkuu, nimekusoma Afande!” Kisha ilikatwa simu ile.
Afande Magane akamuuliza.
“Vipi ni mkuu wa kituo huyo aliepiga simu hiyo?!”
Afande Kubuta akamjibu “Hapana huyo ni IGP bwana, na sijawahi kupigiwa simu hata mara moja na IGP”
Afande Kubuta akamueleza yote aliyoongea bosi wao.
Afande Magane akashangaa sana kusikia habari hiyo, na akasema.
“Bila shaka kuna mtu amekwenda kwa IGP anayehusiana na mtuhumiwa, na kuongea na IGP! Sasa kama hivyo ndivyo basi kesi hii rafiki yangu, inabidi uwe makini sana. Kwani wewe ndiye mpelelezi wa kesi hii mwenye Jalada lake! Sisi wengine tunapewa amri tu, Fatana na afande fulani kwa upekuzi na majadiliano tunafanya hivyo! Duh hii hali sasa ishakuwa pevu, je? unayo ripoti iliyokamilika ya upelelezi wa kesi hii sasa? Kwani ndiyo inatakiwa ili ionekane bila shaka afande kama angetaka kujua angeuliza umefikia wapi kwenye upelelezi wa kesi hii. Ila hapa naona kuna kitu cha ziada kutoka kwa Bosi kwani Photo Albam na Note Books vya marehemu yeye vya nini? Okay sasa mimi naona twende Mikocheni kwanza kutekeleza amri ya Bosi kisha uvipeleke kama alivyoagiza, kisha tusikilize atakwambiaje kwani tunaweza kuumiza vichwa kumbe mambo yenyewe ni shwari tu!”
*******
Afande Kubuta na Afande Magane walibisha hodi nyumbani kwa marehemu Hamida, walipofunguliwa mlango wakajitambulisha ikiwa ni pamoja na kutoa vitambulisho vyao vya kazi.
Wakakaribishwa ndani, walipofika ndani wakaeleza walichokiendea pale. “Kama tulilvyokwisha jitambulisha, tupo hapa kikazi hivyo tunahitaji Photo Albam zote za marehemu Hamida pamoja na vitabu vyake vya kumbukumbu.”
Yule dada aliyewapokea akaanza kuvitafuta vitabu vyake vya kumbukumbu marehemu Hamida chumbani kwake kwani “photo albam” zilikuwa mezani chumbani mle.
Yule dada akawakabidhi “photo albam” nne afande Kubuta akazichukua na kuziweka kwenye mfuko wake wa ngozi alioushika mkononi, akifarijika angalau anachokitaka Bosi wake kutoka kwenye nyumba ile, kimoja amekwisha kipata. Iliwachukua kama nusu saa kuja kukiona kitabu cha kumbukumbu cha marehemu Hamida. Yule dada aliyejitambulisha kama mdogo wa Hamida, anayejulikana kwa jina la Neema, akawaambia askari wale.
“Jana alikuja afande mwenzenu wa kike aliyejitambulisha kwa jina la afande Jamila, amechukua picha tatu kutoka katika albamu hizo, na ameahidi kuzirudisha mara baada ya kukamilisha upelelezi wenu!”
“Whaat?!”
Afande Kubuta na mwenzake afande Magane walijikuta wakisema kwa pamoja huku wakiwa hawaamini masikio yao kwa kile walichokisikia kutoka kwa Neema!
“Umesemaje?!” Afande Kubuta akamuuliza Neema.
“Mbona mmeshituka sana, ina maana hamna taarifa za picha hizo kufika ofisini kwenu? Mimi nimejua mmekuja kuchukua nyingine ili mkamilishe huo upelelezi wenu!”
USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA
Ili Kunipa Nguvu ya Kuendelea Kuwaletea Simulizi Shawishi Wapenzi wa Simulizi Wapakue(Install) App ya CnZ Media